DODOMA-Polisi wa Kata ya Ngh’ongh’ona, Mkaguzi wa Polisi Johanes Ndunguru, ametoa wito kwa vijana kuacha tabia ya kukaa vijiweni bila kujishughulisha na shughuli za uzalishaji, akisisitiza kuwa hali hiyo huchochea kujiingiza katika makundi ya uhalifu.
Akizungumza katika Mtaa wa Mhande jijini Dodoma, Mkaguzi Ndunguru aliwahimiza vijana kuelekeza nguvu zao katika kazi halali zitakazowawezesha kujipatia kipato na kukidhi mahitaji yao ya msingi, badala ya kupoteza muda katika mazingira yasiyo na tija.
Alieleza kuwa,uwajibikaji wa vijana katika shughuli za maendeleo ni nyenzo muhimu katika kujenga jamii salama na yenye ustawi.
Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuimarisha dhana ya ulinzi shirikishi, akibainisha kuwa usalama wa jamii unahitaji ushirikiano wa wananchi wote.
“Ni wajibu wa kila mwananchi kuwa mlinzi wa mwenzake. Ushirikiano huu utasaidia kuzuia vitendo vya uhalifu na kuimarisha amani katika maeneo yetu,” alisema.
Jeshi la Polisi linaendelea kutoa elimu kwa umma ili kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika kudumisha usalama, sambamba na kuwahimiza vijana kuchangamkia fursa za ajira na kujiajiri kama njia ya kujiepusha na mienendo hatarishi.
