ANKARA-Wabunge Wawakilishi wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) wamekutana katika Kikao cha Jukwaa la wanawake ambalo limefanyika nchini Uturuki mapema hii leo.
Wawakilishi hao wametumia jukwaa hilo kuitangaza Tanzania na kuwakaribisha washiriki wa Mkutano kuhudhuria kwa wingi Mkutano wa 153 unaotarajia kufanyika nchini mwezi Oktoba, 2026.
Akizungumza kwa niaba ya Wawakilishi wenzake Balozi Dkt. Pindi Chana amewahakikishia washiriki hao kuwa Tanzania ni salama chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Kuhusu ajenda za wanawake, Balozi Dkt. Pindi Chana amesema Serikali ya Tanzania imeweka jitihada kuhakikisha wanashiriki katika shughuli za kiuchumi, kijamii na ngazi mbalimbali za maamuzi.
Katika hatua nyingine Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Daniel Sillo amesema kuwa Bunge La Tanzania Linaunga Mkono Azimio la kulipa Bunge la Kiarabu hadhi ya mwangalizi kwenye Mtandao wa Kibunge wa Nchi Zisizofungamana na Upande Wowote (NAM -PN).
Sillo amesema hayo wakati akihutubia Mkutano wa 5 wa Mabunge Wanachama wa Mtandao huo nchini Uturuki akiwa amemuwakilisha Spika wa Bunge Mussa Hassan Zungu.
Katika azimio hilo, mabunge wanachama yametambua umuhimu wa msingi wa kuendeleza uhusiano na taasisi nyingine za kimataifa kama sehemu muhimu ya ujenzi wa kitaasisi na uendeshaji wenye ufanisi wa NAM-PN.



