NA DIRAMAKINI
TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi imetoa kibali kwa taasisi na asasi za kiraia kushiriki katika utoaji wa elimu ya mpiga kura pamoja na uangalizi wa uchaguzi mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Ismani, Halmashauri ya Wilaya ya Iringa na uchaguzi wa Udiwani katika Kata ya 12, Tanzania Bara.
Hayo ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na Kaimu Mkurugenzi wa Uchaguzi, Juma I. Rahisi kwa niaba ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi.Uamuzi huo umetolewa kwa mujibu wa kifungu cha 10(1)(h) cha Sheria ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 292, kikisomwa kwa pamoja na kanuni ya 22(4) ya Kanuni za Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi za mwaka 2024.
Kwa kuzingatia masharti hayo ya kisheria, Tume imeridhia taasisi tatu (3) za kiraia kushiriki katika utoaji wa elimu ya mpiga kura katika maeneo husika.
Aidha, kwa kuzingatia kifungu cha 85(4) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani, Sura ya 343, pamoja na kanuni ya 13(4) ya Kanuni za Uchaguzi za mwaka 2025, Tume pia imetoa kibali kwa waangalizi wa uchaguzi kutoka taasisi za ndani ya nchi mbili (2) kushiriki katika zoezi la uangalizi wa uchaguzi huo mdogo.
Hatua hiyo inalenga kuimarisha uelewa wa wananchi kuhusu haki na wajibu wao wa kidemokrasia, sambamba na kuongeza uwazi na uaminifu katika mchakato mzima wa uchaguzi.
Aidha, taasisi zote zilizoidhinishwa zinapaswa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo iliyowekwa ili kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa haki, uhuru na amani.
