NA DIRAMAKINI
RAIS wa Marekani,Donald J. Trump ametangaza hatua mpya ya kiuchumi inayolenga kuongeza ushuru kwa magari na malori yanayoingizwa nchini Marekani kutoka Umoja wa Ulaya.Kwa mujibu wa tamko hilo, ushuru huo utaongezwa hadi kufikia asilimia 25.
Katika taarifa yake, Rais Trump ameeleza kuwa, hatua hiyo inalenga kulinda viwanda vya ndani pamoja na kuhimiza uwekezaji wa moja kwa moja ndani ya Marekani.
Aidha, amebainisha kuwa,kampuni za magari kutoka Ulaya zitapewa fursa ya kuepuka ushuru huo iwapo zitaamua kuanzisha uzalishaji wa magari na malori ndani ya viwanda vilivyopo Marekani.
“Ni jambo linaloeleweka kikamilifu na kukubaliwa kwamba iwapo watatengeneza magari na malori katika viwanda vya Marekani, hakutakuwa na ushuru wowote,” amenukuliwa Rais Trump.
Hatua hiyo inatarajiwa kuwa na athari kwa biashara ya kimataifa, hususan katika sekta ya magari, ambapo Umoja wa Ulaya ni miongoni mwa wauzaji wakubwa wa magari katika soko la Marekani.
Aidha,wachambuzi wa uchumi wanaonya kuwa ongezeko la ushuru linaweza kusababisha mvutano wa kibiashara kati ya pande hizo mbili, pamoja na kuongeza gharama kwa watumiaji wa mwisho.
Hata hivyo, baadhi ya wadau wa viwanda vya ndani wanaona hatua hiyo kama fursa ya kukuza ajira na uzalishaji wa ndani, iwapo kampuni za kimataifa zitachagua kuwekeza moja kwa moja nchini humo.
