DODOMA-Wizara ya Madini na Taasisi ya CRDB Bank Foundation jana Mei 14, 2026 zilikutana na kujadili fursa za ushirikiano katika kuendeleza mnyororo wa thamani wa madini nchini, katika kikao kilichofanyika Makao Makuu ya Wizara ya Madini, Mtumba jijini Dodoma.

Katika kikao hicho, Ujumbe wa Wataalamu wa Wizara ya Madini uliongozwa na Kamishna wa Madini Msaidizi anayeshughulikia Uchimbaji Mdogo, Eng. Moses Kongola, huku ujumbe wa CRDB Foundation ukiongozwa na Baraka Kiyalo, Meneja wa Ruzuku wa Taasisi ya CRDB Bank Foundation.
Kupitia kikao hicho, pande hizo mbili zilijadili maeneo mbalimbali ya ushirikiano ikiwemo kusaidia upatikanaji wa mitaji kwa wachimbaji wadogo kupitia programu ya Wizara ya Mining for a Brighter Tomorrow (MBT) na Crdb Bank Foundation kupitia “Imbeju Program” kwa ajili ya utoaji wa elimu ya kifedha na ujasiriamali, pamoja na uwezeshaji wa matumizi ya teknolojia bora za uchimbaji mdogo wa madini.
Aidha, mashirikiano hayo yanalenga kuhakikisha kuwa, vijana, wanawake, na watu wenye mahitaji maalum wananufaika ipasavyo na fursa zilizopo katika Sekta ya Madini. 

Majadiliano hayo yanaakisi dhamira ya Serikali na sekta binafsi katika kuhakikisha rasilimali za madini zinachangia zaidi ukuaji wa uchumi na ustawi wa wananchi kupitia ushirikiano jumuishi na endelevu








