Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, amewaaga vijana 400 wa Kitanzania wanaokwenda kufanya kazi nje ya nchi, akisisitiza umuhimu wa kujiunga na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na kuchangia katika Mfuko huo ili kujihakikishia ulinzi wa kijamii na ustawi wa maisha yao ya sasa na baadaye.
Alisema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kuwaaga vijana hao, ambao pia walipata elimu ya hifadhi ya jamii kutoka NSSF ikiwa ni sehemu ya kuwaandaa kwa maisha na ajira zao nje ya nchi.
Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri Sangu alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake imara unaoendelea kuimarisha diplomasia ya ajira na kufungua fursa salama kwa Watanzania kufanya kazi nje ya nchi, hatua inayoongeza usalama na heshima ya wafanyakazi wa Kitanzania katika soko la ajira la Kimataifa.




















