Wafikishwa mahakamani kwa kughushi nyaraka ili kujipatia manufaa

KILIMANJARO-Juni 10, 2026 Ofisi ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (TAKUKURU) Wilaya ya Rombo Mkoa wa Kilimanjaro imewafikisha mahakamani washtakiwa watatu ambao ni Bw.Louis Hilario Sunga ambaye ni Mhandisi na Msimamizi wa Mradi wa Ujenzi wa Nyumba ya Makazi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Rombo.
Wengine ni Afisa Ugavi Msaidizi katika Halmashauri ya Wilaya ya Rombo,Yusuphan Ally Nkanda na Paul Patrice Kavishe ambaye ni mfanyakazi katika duka la vifaa vya ujenzi la Joseph Ernest Swai, lijulikanalo kama “BABUU HARDWARE” lililopo Wilaya ya Rombo.

Washtakiwa hao wamefunguliwa kesi ya jinai namba 12954/2026 katika Mahakama ya Wilaya ya Rombo mbele ya Mhe. Herieth Mhenga, Hakimu Mwandamizi Mkuu wa mahakama hiyo.

‎‎Washtakiwa hao wameshtakiwa kwa makosa yafuatayo chini ya Kanuni za Adhabu Sura ya 16 Toleo la Mwaka 2022; Kughushi nyaraka kosa chini ya vifungu vya 333, 335(a), (d), (i), 337, 340 na 342, Kutotimiza wajibu wa kisheria kosa chini ya kifungu cha 123, Uzembe kazini kosa chini ya vifungu vya 121 na 35 na Kusaidia kutenda kosa chini ya vifungu vya 22(c) na 35.

‎Mwendesha Mashtaka wa Serikali kutoka TAKUKURU,Bi.Sophia Swalehe ameieleza kwamba, katika kipindi cha Aprili 17, 2025 hadi Juni 30, 2025 Bw. Sunga ambaye ni mshtakiwa wa kwanza alipewa fedha jumla ya Tsh. 5,000,000/= kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya ujenzi wa nyumba ya makazi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo pamoja na malipo ya fundi.

Baada ya kupokea fedha hizo, mshtakiwa wa kwanza alifika katika duka la “BABUU HARDWARE” na kuchukua 'Delivery Note' Namba 1348 na Invoice Namba 1046 kutoka kwa Bw. Paul ambaye ni mshtakiwa wa tatu.

Bi. Sophia ameendelea kuieleza Mahakama kuwa,mshtakiwa wa kwanza alizitumia nyaraka hizo kuainisha vifaa mbalimbali akionesha kwamba vimenunuliwa katika duka tajwa hapo juu, alisaini nyaraka hizo akijifanya kuwa mmiliki na muuzaji wa duka jambo ambalo si kweli.

Akiendelea kuielezea Mahakama Bi.Sophia amesema kuwa, mshtakiwa wa kwanza aliziwasilisha nyaraka hizo kwa Bw. Yusuphan ambaye ni mshtakiwa wa pili katika kesi hii naye aliingiza taarifa husika kwenye vitabu vya kumbukumbu (Store Ledger), akionesha kwamba vifaa hivyo vimenunuliwa, vimepokelewa na kutumika katika ujenzi wa nyumba ya makazi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo.

Kwa maafisa hao wa Serikali kufanya makosa waliyoyafanya, wamekiuka Kanuni ya 334 ya Kanuni za Ununuzi wa Umma ya Mwaka 2025 na Agizo Namba 59(1) la Kanuni za Usimamizi wa Fedha za Serikali za Mitaa ya Mwaka 2009.

Washtakiwa namba 1 na 2 wamekana mashitaka yote na wako nje kwa dhamana.

Aidha,mshtakiwa wa tatu amekiri shtaka la kusaidia kutenda kosa na kutiwa hatiani kwa kukiri kwake kosa.

Baada ya kuiomba mahakama impunguzie adhabu kwa kuwa ana wazazi ambao ni wagonjwa na tegemezi wadogo, mshtakiwa amehukumiwa kifungo cha nje kwa miezi 12.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

Know matter how large or small your business is, advertising here