ARUSHA-Jeshi la Polisi Kikosi cha Kuzuia wizi wa Mifugo (STPU) katika doria ya pamoja kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi limefanikiwa kumkamata mtuhumiwa mmoja aliyekuwa akisafirisha mifugo 100 kwenda nchi jirani kwa njia za magendo.
Akizungumza leo Julai 20, 2026 Kamanda wa Polisi Kikosi cha Kuzuia Wizi wa Mifugo Nchini (STPU) Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Simon Pasua, amesema kuwa mtuhumiwa huyo amekamatwa katika Kijiji cha Eworiendeke, Kata ya Kimokouwa, Wilaya ya Longido mkoani Arusha akiwa anatorosha mifugo hiyo ambayo ni Mbuzi na Kondoo.
Aidha Kamanda Pasua amesema kuwa uchunguzi wa awali umebaini kuwa mtuhumiwa huyo alikuwa ametoka na mifugo hiyo katika mnada wa Oldonyosambu uliopo Wilayani ya Arumeru Mkoani humo, huku akisema kuwa uchunguzi zaidi wa tukio hilo unaendelea kwa hatua zaidi za kisheria.
Hata hivyo kamanda Pasua ametumia fursa hiyo kutoa wito kwa Wafugaji na Wafanyabiashara wa Mifugo kuwa wazalendo kwa kufuata sheria na taratibu za usafirishaji wa mifugo, na kuwaomba Wananchi hususani wanaoishi mipakani kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kutoa taarifa za uhalifu wa mifugo ikiwemo utoroshwaji kwa njia za magendo.
