RUKWA-Vyombo vya ulinzi na usalama mkoani Rukwa vimefanya mazoezi ya pamoja ya matembezi na kukimbia mbio za pole (jogging) ikiwa ni sehemu ya kuimarisha mshikamano baina ya taasisi hizo na kuongeza ushirikiano katika kudumisha amani, ulinzi na usalama wa wananchi.
Mazoezi hayo yamefanyika Julai 17, 2026, yakianzia katika Ofisi ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa na kupita katika maeneo mbalimbali ya Manispaa ya Sumbawanga. Yameongozwa na Katibu Tawala wa Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga Gabriel Masinga aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga.
Mbali na vyombo vya ulinzi na usalama, wananchi mbalimbali walishiriki mazoezi hayo, jambo lililoonesha mshikamano na kuimarisha uhusiano kati ya wananchi na vyombo vyao vya ulinzi na usalama. Ushiriki huo umeendelea kujenga imani, ushirikiano na dhana ya usalama shirikishi katika jamii.



