NA DIRAMAKINI
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan leo Agosti 10,2026 amekutana na kufanya mazungumzo na Maaskofu wa Kanisa Katoliki nchini Tanzania kupitia Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (Tanzania Episcopal Conference-TEC), Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma.
Hayo ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu,Bakari S. Machumu.
Mazungumzo hayo yalilenga kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na TEC na kujadili masuala mbalimbali ya kitaifa yanayoigusa jamii, yakiwemo ya kisiasa, imani na maendeleo, pamoja na kuimarisha amani, mshikamano na kujenga mustakabali mwema wa Taifa.
Aidha, mazungumzo hayo yaligusia umuhimu wa nafasi ya madhehebu na Viongozi wa Dini katika kulea jamii yenye maadili mema, uwajibikaji na mshikamano, ikiwa ni sehemu ya mchango wao katika ustawi na maendeleo endelevu ya Taifa.
Mheshimiwa Rais amewashukuru Maaskofu hao kwa kuona umuhimu wa kukutana na kujadiliana naye masuala yenye tija kwa Taifa na kuwahakikishia dhamira yake ya kuendeleza utamaduni wa kushauriana na kushirikisha Viongozi wa Dini na makundi mbalimbali katika jamii kuhusu masuala muhimu ya kitaifa kila inapohitajika.
Tags
Dr Samia Suluhu Hassan
Habari
Kanisa Katoliki Tanzania
Mazungumzo na Rais
Viongozi wa Dini
Viongozi wa TEC



