NA DIRAMAKINI
MABINGWA wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara, Young Africans SC (Yanga SC) wameanza kampeni yao ya msimu wa 2026/27 katika Ligi ya Mabingwa barani Afrika kwa sare ya bao 1-1 dhidi ya Gaborone United ya Botswana.
Yanga SC ililazimika kusubiri hadi dakika za nyongeza kupata bao la kusawazisha katika mchezo huo wa kwanza wa raundi ya awali.Manage huo umepigwa Septemba 5,2026 katika Dimba la Taifa la Botswana (Botswana National Stadium) jijini Gaborone nchini Botswana.
Gaborone United walikuwa wa kwanza kuliona lango baada ya Obry Ambrosius kuifungia timu hiyo bao katika dakika ya 32, hali iliyowafanya wenyeji kuingia mapumzikoni wakiwa mbele kwa bao 1-0.
Hata hivyo, Yanga haikukata tamaa na juhudi zake zilizaa matunda katika dakika ya 90+5, baada ya Selemani Mwalimu kusawazisha na kuifanya timu hiyo ya Tanzania kurejea nyumbani ikiwa na sare muhimu kabla ya mchezo wa marudiano.
Matokeo hayo yanaifanya Yanga kuwa na nafasi ya kuamua hatma ya safari yake katika mchezo wa pili utakaochezwa Septemba 12, 2026.
Tags
Botswana National Stadium
Gaborone United
Habari
Kombe la Klabu Bingwa barani Afrika
Michezo
Yanga SC