MAJALIWA:TUTAANZISHA MAMLAKA YA MAJI CHEMBA

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema Serikali inapanga kuanzisha Mamlaka ya Maji Chemba hivi karibuni.

Ametoa kauli hiyo leo Septemba 13, 2020 wakati akizungumza na wananchi katika eneo la Mnadani, Kijiji cha Kelema, Kata ya Paranga, wilaya ya Chemba mkoani Dodoma kwenye mkutano wa kumuombea kura Rais Dkt. John Pombe Magufuli na mgombea ubunge jimbo la Chemba, Mohammed Moni na wagombea udiwani wa CCM.

Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwahutubia wananchi wa kijiji cha Kelema, kata ya Paranga, wilayani Chemba , katika mkutano wa kampeni, Septemba 13, 2020. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

“Wilaya hii haina mamlaka ya maji. Kwa hiyo tutaanzisha Mamlaka ya Maji ili watumishi wawepo wilayani. Wasimamie kwa karibu na waweze kufuatilia vyanzo vya maji kutokea hapa Chemba wakati tukiendelea kutatua tatizo la maji wilayani hapa. Tutaunda Mamlaka ya maji hivi karibuni.”

Amesema Serikali ilitoa sh. bilioni 1.688 za kutafuta vyanzo vya maji huko Orada, Kisanga, Moi, Mondo na Ndaki. “Pia Serikali ya Awamu ya Tano imetoa sh. milioni 677 za kuchimba visima huko Mondo, Mrijo Juu, Chambalo, Hamai na Chemba.”

“Tuna uhakika tukipata lita za maji za ujazo 4,700 zinatosha kabisa kujenga mtandao wa maji. Kazi ya kuboresha miundombinu ya maji inaendelea. Zimetengwa fedha nyingine, sh. milioni 150 za kusambaza maji Kelema, Msaada na Bumbu.”

Akizungumzia sekta ya afya, Mheshimiwa Majaliwa amesema zimetolewa sh. bilioni 1.8 za kujenga hospitali ya wilaya ya Chemba ili wananchi wapate huduma za tiba wakiwa hapohapo badala ya kwenda Kondoa kama ilivyokuwa awali.

Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimkabidhi nakala ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2020-2025 mgombea ubunge wa CCM wa jimbo la Chemba, Mohammed Moni, katika kijiji cha Kelema Kata ya Paranga wilayani Chemba , kwenye mkutano wa kampeni, Septemba 13, 2020. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

“Nia yetu ni kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma hukohuko aliko kwa kuweka zahanati katika kila kijiji, vituo vya afya kwa kila kata. Wakimaliza ujenzi, tumetenga shilingi milioni 500 za vifaa vya hospitali kwa majengo yote saba.”

“Tumepeleka sh. milioni 400 za kituo cha afya kule Hamai, shilingi milioni 500 kule Mrijo na shilingi milioni 400 kule Kwa Mtoro. Kazi ya ujenzi ikiisha, kila kimoja kitapata shilini milioni 250 za vifaa vya tiba.”

Ninawaomba mumpe kura Rais Dkt Magufuli, Mbunge na madiwani wa CCM ili tukamilishe kazi hizi kwa sababu Serikali hii ni ya watekelezaji. Tunasema na tunatenda.”

Wakati huohuo, Mheshimiwa Majaliwa amesema Rais Magufuli anataka umeme usambazwe kote nchini na ndiyo maana akaamua kupunguza bei ya kuunganisha umeme.

“Rais wetu kasema anataka kuona kila nyumba ya Mtanzania inawaka umeme. Amepunguza gharama za kuunganisha umeme kutoka shilingi 380,000/- hadi shilingi 27,000/-. Rais wetu kasema ni marufuku kulipia nguzo za umeme. Mwananchi hutakiwi kulipia nguzo yoyote ile. Atakayekuuzia nguzo, mwambie akupe risiti, leta risiti tumlipue huyo Afisa., amesisitiza.Mheshimiwa Majaliwa anaendelea na mikutano ya kuomba kura wilayani Kondoa.



Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news