WAZIRI BITEKO AUAGIZA MGODI KULIPA DENI LA KIJIJI NDANI YA SIKU 60

*Asisitiza ujenzi wa bwawa la kuhifadhia topesumu (TSF)

Na Steven Nyamiti, Mara

Waziri wa Madini, Doto Biteko ameuagiza uongozi wa kampuni ya uchimbaji wa madini ya Dhahabu MMG GOLD LIMITED unaomilikiwa kwa ubia kati ya Kampuni ya MMG na Polygon kulipa deni la kiasi cha shilingi milioni 36 zinazodaiwa na kijiji kwa mujibu wa mkataba wa uwekezaji.
Waziri wa Madini, Doto Biteko (wa pili kushoto) akikagua eneo la shughuli za uchimbaji katika mgodi wa Cata Mining ulipo wilaya ya Butiama Mkoani Mara tarehe 19 Julai, 2021.

Agizo hilo amelitoa Julai 19, 2021 wakati akiwa kwenye ziara ya kukagua shughuli za uchimbaji katika mgodi wa MMG GOLD LTD katika kijiji cha Seka kata ya Nyamlandililila wilaya ya Musoma Vijijini , Mkoani Mara.

Akizungumza na Mkurugenzi wa mgodi huo Yury Chernomorchenko, Waziri Biteko ametoa miezi miwili deni hilo liwe limelipwa na kampuni hiyo.

Biteko amesema kuwa, kampuni hiyo ilikuwa inadaiwa zaidi ya shilingi milioni 60 toka mwaka 2018 na Serikali ya kijiji kama ushuru, deni lililoachwa na menejimenti iliyopita ya MMG ambapo walilipa fedha kiasi na hadi sasa deni linalodaiwa ni shilingi milioni 36 na kijiji kwa mujibu wa mkataba wa uwekezaji.
Waziri wa Madini, Doto Biteko akishuhudia utiaji saini wa makubaliano ya kampuni ya MMG GOLD LIMITED ya kulipa Shilingi Milioni 36 ndani ya siku 60. Kushoto ni Mkurugenzi wa mgodi huo Yury Chernomorchenko akitia saini makubaliano hayo Mkoani Mara.

"Niwaombe Serikali za mitaa, Vijiji na Halmashauri, makubaliano yoyote wanayoingia na migodi ili yaweze kuwa na nguvu ya Kisheria kwa msimamizi wa migodi ni lazima wayasajili makubaliano hayo kwenye ofisi ya madini,"amesisitiza Biteko.

"Tunataka tuone haya manufaa ya mgodi huu yaweze kuonekana kwenye maisha ya kawaida ya wananchi kwenye miundombinu ya barabara, miundombinu ya elimu na afya,"amesema.

Pia, amemuagiza Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Mara Nyaisara Mgaya kuhakikisha anasimamia malipo hayo yanafanyika ndani ya muda hu ona endapo hayataliwa asimamishe shughuli zote katika mgodi mpaka deni litakapolipwa.

Akiwa kwenye mgodi wa uchimbaji Dhahabu wa Cata Mining Waziri Biteko ameagiza uongozi wa mgodi huo kuzingatia Sheria na Kanuni za madini zilizopo hapa nchini hususan wanapofanya ununuzi wa bidhaa mbalimbali na wanapotafuta kampuni za kufanyanazo kazi kwenye mgodi.

"Msipozingatia sheria za madini mtapigwa faini ya shilingi milioni 50 jambo ambalo Serikali ya awamu ya Sita haipendi, tunataka kuwalea ili mkue zaidi siyo kuwarudisha nyuma," amesema Waziri Biteko.

Akijibu swali la waziri kuhusu ajira kwa wazawa, Mkurugenzi wa Mgodi huo Johann Christoffel amesema hadi sasa wana watumishi 470 ambao ni wazawa jambo ambalo limepongezwa na Waziri Biteko.

Hata hivyo, amewashauri wanapoajiri wazawa watoe kipaumbele kwa wakazi wa maeneo yanayozunguka mgodi wa Cata ili kuweka mazingira mazuri ya kiuhusiano na jamii.

Waziri Biteko amefanya ziara ya siku moja Mkoani Mara na kutembelea migodi miwili ya MMG Gold Limited na Cata Mining. 

Mkoa wa Mara umebarikiwa kuwa na aina nyingi za Madini ambayo ni dhahabu, shaba, Silver, chuma, chokaa, soapstone na madini ya ujenzi. Kati ya hayo madini yanayopatikana kwa wingi zaidi ni madini ya dhahabu.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news