KMC FC KUWAFUATA MBEYA CITY NA WACHEZAJI 21 KESHO

NA MWANDISHI DIRAMAKINI

KIKOSI cha Timu ya KMC FC kitaondoka jijini Dar es Salaam kesho kuelekea jijini Mbeya kwa ajili ya mchezo wa Ligi Kuu ya NBC soka Tanzania Bara dhidi ya Mbeya City utakaopigwa siku ya Jumamosi ya Novemba 27,2021 katika uwanja wa Sokoine jijini humo.

Hayo ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Novemba 23,2021 na Christina Mwagala ambaye ni Ofisa Habari na Mawasiliano wa KMC FC.
Msafara huo wa Timu ya Manispaa ya Kinondoni utahusisha wachezaji 21, benchi la ufundi pamoja na viongozi ikiwa ni katika kuhakikisha kwamba timu inakwenda kupata matokeo mazuri katika mchezo huo licha ya kuwa KMC FC itakuwa ugenini.

"Hadi sasa maandalizi yanaendelea vizuri tangu kumalizika kwa mchezo wa mzunguko wa sita wa Ligi ya NBC dhidi ya Azam uliochezwa Novemba 21 katika uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam na kuibuka na ushindi wa magoli mawili kwa moja Timu iliendelea na maandalizi jana jioni.

"Licha ya kwamba mchezo huo utakuwa na ushindani mkubwa,lakini Benchi la ufundi linaloongozwa na kocha Mkuu John Simkoko na wasaidizi wake Habibu Kondo pamoja na Hamadi Ally linaendelea kujiimarisha zaidi kuelekea katika mchezo huo na kwamba malengo na mikakati nikupambania timu iweze kupata ushindi muhimu.

“Tunaenda kwenye mchezo wenye ushindani tukiwa ugenini, kikubwa hatuangalii tunaenda kucheza nyumbani au ugenini,tunachokifanya nikujiandaa kwa mchezo wetu muhimu, Mbeya City ni Timu mzuri na tumeona walipata matokeo mazuri, kwa hiyo tunalijua hilo hivyo kwenye maandalizi yetu tunaenda kupambania alama tatu,"imeeleza taarifa hiyo.

"Lakini pia zaidi tunamshukuru Mungu kuwa katika mchezo uliopita hatukupata mchezaji mwenye majereha, kwa hiyo kikosi chote kipo imara na morali pia ipo juu, kikubwa mashabiki zetu waendelee kutusapoti kama ambavyo sikuzote wamekuwa wakifanya, tunahitaji kupambana zaidi ilikutoka kwenye nafasi ambazo tupo kwa hivi sasa,"imeongeza taarifa hiyo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news