NHC yatakiwa kuwekeza majengo ya makazi, biashara Kahama

NA MUNIR SHEMWETA-WANMM

SHIRIKA la Nyumba la Taifa (NHC) limetakiwa kufanya uwekezaji wa majengo ya biashara pamoja na nyumba za kupangisha katika mji wa Kahama mkoani Shinyanga kutokana na mji huo kuendelea kukua kwa kasi.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Angeline Mabula akizungumza katika moja ya kibanda cha biashara kinachoendelea kujengwa katika kituo cha mabasi katika halmashauri ya Manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga wakati wa ziara yake hivi karibuni. Dkt.Mabula amelitaka Shirika la Nyumba la Taifa kuwekeza miradi yake katika wilaya hiyo.

Kauli hiyo imetolewa hivi karibuni na Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula wakati wa ziara yake ya siku mbili mkoani Shinyanga kukagua utendaji kazi wa sekta ya ardhi na miradi inayosimamiwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).

Alisema, Kahama ni mji unaokuwa kwa kasi kubwa na kama Shirika la Nyumba la Taifa halijafikiria kuwekeza katika mji huo basi lijipange kuona namna gani linaweza kutumia fursa ya kukua mji huo kwa kufanya uwekezaji na kusisitiza kuwa hata kama hakuna uhitaji wa nyumba za kuuza Shirika linaweza kujenga majengo ya biashra yanayoweza kupangishwa.

“Uwekezaji wowote mtakaoufanya hapa Kahama kama hakuna walionesha dhamira ya dhati ya kununua basi jengeni nyumba za kupanga ili kuwa na nyumba za kutosha mji unakuwa haraka,”alisema Dkt.Mabula.

Kwa mujibu wa Naibu Waziri wa Ardhi, kila ambapo Shirika la Nyumba la Taifa limewekeza katika majengo ya kibiashara hakuna mahali ambapo limekosa wapangaji na kadri mji wa Kahama unavyokuwa kwa kasi bado NHC inaweza kufaidika.
Naibu Waziri wa Ardh Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dk. Angeline Mabula akizungumza na watendaji wa sekta ya ardhi na viongozi wa wilaya ya Kahama wakati wa ziara yake katika wilaya hiyo.

Alimuagiza Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa mkoa wa Shinyanga kufanya maamuzi ya haraka kwa lile eneo liloainishwa na Manispaa ya Kahama kwa kwa ajili ya uwekezaji na kusisitiza kuwa Kahama bado inazo fursa nyingi.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kahama ambaye ni Mkuu wa Idara ya Ardhi na Maliasili Clemence Nkusa alimuambia Naibu Waziri wa Ardhi Dkt Mabula kuwa, tayari halmashauri yake ilishatenga eneo kwa ajili ya Shirika la Nyumba la Taifa kufanya uwekezaji.

Kufuatia hatua hiyo Naibu Waziri Dkt Mabula amelitaka Shirika la Nyumba la Taifa kufanya maamuzi ya haraka na kufikia Desema mwaka huu Wizara ya Ardhi iwe imepata taarifa ya aina ya uwekezaji utakaofanyika.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt.Angeline Mabula akizungumza na mmoja wa wafanyabiashara aliyemkuta katika kituo cha mabasi katika halmashauri ya Manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga wakati wa ziara yake hivi karibuni. Dkt.Mabula amelitaka Shirika la Nyumba la Taifa kuwekeza miradi yake katika wilaya hiyo.

Vile vile, Dkt.Mabula ameitaka NHC kufikiria namna ya kufanya uwekezaji wa nyumba katika halmashauri ya wilaya ya Ushetu kutokana na halmashauri hiyo kuwa na uhitaji wa nyumba.

”Ni vizuri pia Shirika la Nyumba kuanza kufikiria kujenga nyumba katika halmashauri ya wilaya ya Ushetu maana kule kuna uhitaji mkubwa wa nyumba zikiwemo za watumishi,"alisema Naibu Waziri Mabula.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news