Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro yasikia kilio cha madiwani Karatu

NA SOPHIA FUNDI 

MADIWANI Halmashauri Wilaya ya Karatu mkoani Arusha wamelaani vikali kauli chafu zinazotolewa na maaskari wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro pale wanapoarifiwa kuhusu wanyama wanaoshambulia wananchi. 
Madiwani hao walisema kauli hiyo wakati wakijadili hoja ya wananchi waliouawa na mnyama aina ya mbogo katika Kijiji cha Oldiani wilayani Karatu katika kikao cha Baraza la Madiwani.

Walieleza masikitiko yao kwa wananchi waliopo pembezoni mwa Hifadhi ya Ngorongoro kushambuliwa na wanyama na kuuawa ambapo wameomba Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kuweka uzio wa umeme ili kuzuia wanyama wakali wanaotoka hifadhini na kuingia kwenye maeneo ya wananchi na kuwashambulia wananchi na kuwaua.

Akichangia hoja, Diwani wa Kata ya Oldian, Peter Mmassy amesema kuwa ni jambo la kusikitisha ndani ya mwezi mmoja wananchi watatu wanauawa na mbogo katika kata yake na kuacha hofu ya maisha ya wananchi wa maeneo ya pembezoni mwa hifadhi.
Akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Karatu, John Lucian amewataka wananchi kuwa watulivu kwani uongozi wa wilaya umeweka mikakati mbalimbali ya kuwadhibiti wanyama wakali wanaotoka hifadhini na kuingia kwenye makazi ya watu ikiwemo Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kuweka uzio wa umeme ili kuwazuia wanyama hao.

Amesema kuwa, mikakati hiyo wameweka kwenye kikao cha pamoja cha wadau wakiwemo wenye mashamba ya mikataba yaliyopo pembezoni mwa hifadhi kufyeka maeneo yao ambayo hayatumiki kwani wanyama wakitoka hifadhini wanajificha kwenye maeneo hayo.

Kwa upande wake mwakilishi wa Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka ya Hifadhi ambaye ni afisa mhifadhi daraja la 2, Mlungwana Mchomvu aliwaomba madiwani kushirikiana katika kuwakabili wanyama wanaotoka hifadhini kwani wanyama hawana mipaka.

Akizungumzia suala la kauli alisema kuwa watafuatilia suala hilo kwa maaskari wanaofanya hivyo na watachukuliwa hatua.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news