Rais Dkt.Mwinyi atoa hotuba ya kihistoria leo, yagusia maeneo 20

NA GODFREY NNKO

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt.Hussein Ali Mwinyi amewashukuru wananchi kwa kuendelea kudumisha umoja, mshikamano na amani nchini kwani hiyo ndiyo misingi ya kuiwezesha nchi na wananchi wake kupiga hatua kiuchumi.
Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi ameyasema hayo leo Januari 11, 2022 Ikulu jijini Zanzibar wakati akitoa hotuba yake kuelekea kilele cha sherehe za Maadhimisho ya Miaka 58 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar

Amesema, moja ya mafanikio waliyoyapata na wanayopaswa kujivunia ni kudumisha na kuendeleza amani, umoja na mshikamano. 

"Kwa hakika hii ndiyo misingi muhimu inayotuwezesha kuzidi kupiga hatua katika sekta zote za maendeleo. Natoa shukrani zangu za dhati kwa viongozi wa kisiasa, viongozi wa dini na asasi za kiraia, viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama vya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na wananchi wote kwa kuendelea kudumisha amani na utulivu nchini kwa faida ya kizazi cha sasa na baadae. 

"Nawahakikishia wananchi na wageni wote wanaotutembelea kwamba, nchi yetu ipo salama na kwamba Serikali zetu zote mbili zitaendelea kutekeleza wajibu wake wa kikatiba na kisheria katika kulinda amani, utulivu na maisha ya wananchi wote na mali zao,"ameeleza Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi. 

Amesema, wakati tukielekea katika kilele cha Maadhimisho ya Sherehe za Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari, 12 mwaka 1964 yatakayofanyika kesho tarehe 12 Januari, 2022 katika uwanja wa Amani jijini Zanzibar ni jambo la la kumshukuru Mwenyezi Mtukufu, Mwingi wa Rehma kwa kutujaalia uhai na afya njema na kutuwezesha kufikia siku ya leo.

"Tunasherehekea na kuadhimisha kutimia miaka 58, tangu wananchi wa Zanzibar tulipojikomboa na kuondokana na unyonge wa kutawaliwa kwa miongo kadhaa. Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ni mwanzo wa safari ya maendeleo kwa wananchi wa Zanzibar kwa kupata mamlaka ya kujiamulia wenyewe mambo yetu ya msingi kwa mustakabali wa maisha yetu. 

"Ni dhahiri kuwa, mafanikio tuliyoyapata katika sekta mbali mbali kwa kipindi cha miaka 58, yametokana na uongozi thabiti wa Waasisi wa Taifa letu na viongozi wote wa awamu za Uongozi zilizotangulia. Ni wajibu wetu kuhakikisha tunayalinda na kuyadumisha Mapinduzi Matukufu ya mwaka 1964 pamoja na Muungano wa Tanzania tukijuwa kwamba hizi ni tunu muhimu tulizoachiwa na waasisi wetu.

"Ndugu wananchi,tunapoadhimisha siku ya Mapinduzi kila mwaka, tuna wajibu wa kuwakumbuka Waasisi wetu wakiongozwa na Marehemu Mzee Abeid Amani Karume pamoja na viongozi wetu wote waliotangulia mbele ya haki, ambao walijitoa muhanga kwa ajili ya Taifa letu na kuitumikia nchi yetu kwa moyo, ujasiri na uzalendo. Tunamuomba Mwenyezi Mungu awalaze pema peponi. Na wale walio hai, Mola awape afya njema na umri mrefu tuendelee kunufaika kwa hekima na busara zao katika safari yetu ya maendeleo. 

"Haya ni Maadhimisho ya pili kwangu tangu kuchaguliwa kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Mwaka jana nilieleza kwamba sote tuna kazi ya kutafsiri kivitendo Malengo ya Mapinduzi kwa kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi ili kustawisha maisha ya Wazanzibari. Tumedhamiria kushirikiana kujenga uchumi mpya wa Zanzibar kwa umoja, mshikamano na maridhiano ili kila Mzanzibari apate fursa ya kuchangia maendeleo na kunufaika na matunda ya Mapinduzi kwa misingi ya usawa. 

"Katika shamra shamra za Maadhimisho haya ya miaka 58 ya Mapinduzi yenye kaulimbiu; Uchumi wa Buluu kwa Maendeleo Endelevu, jumla ya miradi 30 imefunguliwa na 13 imewekewa mawe ya msingi. Nawashukuru sana wananchi kwa kujitokeza kwa wingi katika shughuli zilizopangwa ikiwa ni ishara nzuri za kuunga mkono jitihada zetu za kuleta maendeleo.

"Kwa hakika, miaka 58 ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kipindi kirefu. Katika kipindi hicho tumepata mafanikio mengi na vile vile tumekabiliana na changamoto kadhaa katika utekelezaji wa mipango yetu ya maendeleo,"amefafanua kwa kina Rais Dkt,Mwinyi.

Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, "ni utamaduni uliojengeka na tuliourithi kutoka kwa viongozi wa awamu zilizopita, kutumia sherehe za Mapinduzi kwa kutathmini na kutafakari mafanikio tuliyoyapata katika kujenga nchi yetu pamoja na kudumisha na kuendeleza amani, umoja na mshikamano. 

"Vile vile, huwa tunatumia wakati huu kwa kuzitathmini changamoto mbali mbali zilijitokeza kwa nyakati tofauti na kupanga mikakati ya kuzitafutia ufumbuzi. Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Awamu ya Nane itaendeleza utamaduni huu muhimu kwa maendeleo yetu. 

"Kwa msingi huo, ni vyema tukaendelea kutathmini maendeleo tuliyoyapata katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2020, MKUZA Awamu ya 3, Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2050 pamoja na Mipango ya maendeleo ya Kimataifa katika mwaka 2021 uliomalizika,"amefafanua Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi.

Uchumi

Rais Dkt.Mwinyi amebainisha kuwa, kuwepo kwa hali ya amani na ya utulivu nchini kumewezesha kutekeleza mipango ya maendeleo, ingawa sio kwa kasi waliyoitarajia kutokana na kuwepo kwa janga la maradhi ya UVIKO- 19, ambalo limeathiri sana hali ya kiuchumi ya mataifa yote duniani. 

Amesema, katika mwaka 2021, kasi ya ukuaji wa uchumi iliimarika ikilinganishwa na mwaka 2020, ambapo athari za Maradhi ya UVIKO, zilikuwa kubwa zaidi. 

"Katika robo ya kwanza ya mwaka 2021 (Januari Machi) uchumi wa Zanzibar ulikuwa kwa wastani wa asilimia 2.2 ikilinganishwa na asilimia 1.8 ya kipindi kama hicho kwa mwaka 2020. Kwa kipindi cha robo ya pili (Aprili -Juni) uchumi umeendelea kuimarika zaidi na kufikia ukuaji wa wastani wa asilimia 6.5 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 1.4 kwa kipindi kama hicho mwaka 2020. 

"Katika robo ya tatu ya mwaka 2021, (Julai -Septemba) uchumi wetu ulikua kwa asilimia 8.8 ikilinganishwa na asilimia 3.3 kwa kipindi kama hicho katika mwaka 2020. Ongezeko hilo limechangiwa na kuongezeka kwa miradi ya uwekezaji, kuimarika sekta ya utalii pamoja na shughuli za biashara,"ameeleza Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi. 

Pia amesema kuwa, juhudi kubwa zimefanywa na Serikali za kudhitibiti mfumuko wa bei, ikiwa ni pamoja na kuweka bei elekezi kwa baadhi ya bidhaa muhimu. 

Amesema kuwa, kasi ya mfumuko wa bei kwa kipindi cha Januari hadi Novemba 2021 ilifikia wastani wa asilimia 1.7 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 3.4 kwa kipindi kama hicho cha mwaka 2020.

Makusanyo

Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, kwa kipindi cha Januari- Novemba 2021, Serikali ilikusanya jumla ya Shilingi billioni 745.1, sawa na ongezeko la asilimia 22 ikilinganishwa na makusanyo ya Shilingi bilioni 610.5 zilizokusanywa kwa kipindi cha Januari hadi Novemba 2020. 

Amesema, ongezeko hilo limechangiwa na kuimarika kwa uchumi pamoja na kuanza kutumika kwa mifumo ya kielektroniki ya ukusanyaji wa mapato iliyoanzishwa. Mifumo hiyo inaziunganisha taasisi mbali mbali za Serikali, baina ya Taasisi za Serikali na wafanyabiashara. 

Vile vile,amesema Serikali imefanya marekebisho ya sheria za kanuni za kodi kwa lengo la kuondoa malalamiko ya kuwepo kwa utitiri wa kodi na ada. 

"Ni matumaini yangu kwamba, hatua hiyo itashajiisha ulipaji wa kodi kwa hiari, kukuza ajira na kuongeza usimamizi na ukusanyaji wa mapato ya Serikali. Vile vile, marekebisho ya sheria tuliyoyafanya yamesaidia kutoa unafuu wa ushuru wa stempu kwa wafanyabiashara wadogo na wakati kwa kupunguza viwango maalum kutoka Shilingi 200,000 hadi Shilingi 100,000, kutoka Shilingi 732,000 hadi Shilingi 200,000 pamoja na kupunguza kiwango cha ushuru wa stempu kutoka asimilia 3 hadi asilimia 2 kwa mwaka,"amefafanua Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi. 

Uwekezaji

Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, kwa kipindi cha Novemba 2020 hadi Disemba 2021, Serikali kupitia Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA), imesajili jumla ya miradi 120 yenye mtaji wa Dola za Kimarekani Milioni 787. 

Miradi hiyo amesema, inatarajiwa kutoa zaidi ya ajira elfu saba. Pia amesema, tayari wawekezaji wamejitokeza katika visiwa 10 vilivyotangazwa kukodishwa. 

Amesema, jumla ya Dola za Kimarekani Milioni 261 zitawekezwa kwenye visiwa hivyo ikiwa ni uwekezaji wenye hadhi ya juu. 

Aidha, ZIPA imefanikiwa kukusanya Dola za Kimarekani Milioni 14 ikiwa ni malipo ya awali (Lease Acquisition Cost) kutoka kwa wawekezaji hao.

Vile vile,Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi amesema, huduma za uwekezaji zinazotolewa katika Kituo cha Huduma kwa Wawekezaji (One Stop Centre) zimeimarishwa, ambapo hivi sasa mwekezaji hupatiwa cheti cha uwekezaji ndani ya siku tatu na kibali cha kazi hupatikana ndani ya siku moja. 

Kadhalika, huduma za Usajili wa Kampuni, usajili wa TIN, VAT, kibali cha Kazi na Ukaazi, na ushauri wa kimazingira zinapatikana katika kituo hicho. 

"Kwa lengo la kuimarisha uwekezaji nchini, Serikali imekamilisha mapitio ya Mpango Mkuu wa Matumizi ya Ardhi katika Maeneo Huru ya Uchumi Fumba. Hatua hiyo, imelenga kupanga matumizi sahihi ya ardhi na kuimarisha haiba ya eneo hilo,"amesema. 

Fedha za Mkopo

Wakati huo huo, Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyin amezungumzia kuhusu matumizi ya fedha za mkopo kutoka Shirika la Fedha Duniani (IMF) na mkakati maalum wa kuondoa mdororo wa uchumi.

"Kama nilivyoeleza kwenye hotuba niliyoitoa kwenye sherehe za maadhimisho ya kutimia mwaka mmoja tangu Serikali ya Mapinduzi ya Awamu ya Nane ilipoingia madarakani, Serikali inaendelea kupanga na kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha uchumi. 

"Tumefikia hatua nzuri hivi sasa ya kuanza kutekeleza miradi tuliyoipanga kutekelezwa kwa kutumia fedha zilizotolewa na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) kwa njia ya mkopo kwa ajili ya kukabiliana na athari za Ugonjwa wa Uviko-19.

"Fedha hizo zenye thamani ya Shilingi bilioni 231 sawa na (Dola za Kimarekani milioni 100) zitatumika katika Miradi ya Afya, Elimu, Uwezeshaji, Maji na Nishati, kama nitakavyoelezea wakati nitakapozizungumzia sekta hizo,"amesema Rais Dkt.Mwinyi. 

Aidha, Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, Serikali iko katika mazungumzo ya kukopa fedha nyingine zenye thamani kama hiyo Shilingi bilioni 230 kwa ajili ya kuziingiza kwenye uchumi wa nchi kwa lengo la kuondoa mdororo wa uchumi uliopo. 

"Mazungumzo na taasisi za fedha kwa ajili ya utelezaji wa lengo hilo yanaendelea na tumefikia hatua nzuri. Tuendelee kumuomba Mwenyezi Mungu atuondolee janga la maradhi ya UVIKO 19, ili malengo haya ya kuimarisha uchumi wetu yaweze kutekelezeka kwa ufanisi na kuyafanya maisha ya wananchi kuwa bora zaidi,"amesema Rais Dkt.Mwinyi. 

Utalii

Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, Serikali imeendeleza juhudi mbalimbali za kuimarisha sekta ya utalii na kuitangaza Zanzibar. 

Amesema, Serikali imeandaa na kurahisisha ushiriki wa taasisi za Serikali na kampuni binafsi katika maonesho, mikutano na makongamano ndani na nje ya nchi. 

"Juhudi zetu hizo zimetuwezesha kuongeza idadi ya watalii kutoka 260,644 mwaka 2020 hadi kufikia 393,512 Mwaka 2021, sawa na ongezeko la asilimia 50.97.

"Vile vile, zimetuwezesha kuongeza idadi ya Kampuni za Ndege zinazofanya safari za kuja Zanzibar kutoka 27 hadi 34. Ndege hizo zilizoongezeka zinakadiriwa kuleta zaidi ya watalii 50,000 kwa mwaka. 

"Katika kuhakikisha kwamba, wageni na watalii wanaotutembelea wanakuwa katika mazingira yaliyo salama, Serikali imeanzisha Kikosi maalum cha Askari wa Utalii ambacho nikimekizindua rasmi tarehe 19 Novemba, 2021. 

"Aidha, tumetekeleza mipango maalumu ya kuhifadhi na kuendeleza Mji Mkongwe na majengo ya kihistoria ya daraja la kwanza ambayo ni Beit al-Ajaib na Makumbusho ya Kasri la Wananchi yaliyopo Forodhani. Jengo la Beit Al Ajaib ujenzi rasmi unatarajiwa kuanza mwezi Februari mwaka huu, 2022,"amesisitiza Rais Dkt.Mwinyi. 

Biashara

Amesema, katika mwaka 2021, mwenendo wa biashara ulikuwa ni wa kuridhisha. Bidhaa za chakula, vifaa vya ujenzi na nyingine muhimu kwa maisha ya wananchi wa Zanzibar zimeweza kupatikana katika hali ya kawaida, licha ya kuwepo kwa changamoto mbali mbali duniani zilizosababishwa na janga la maradhi ya UVIKO 19.

"Kuimarika kwa uzalishaji wa baadhi vya viwanda vya ndani kumechangia sana upatikanaji wa uhakika wa baadhi ya bidhaa hizo. 

"Upatikanaji wa unga wa ngano umeimarika kutokana na kuongezeka kwa uzalishaji wa bidhaa hiyo katika Kiwanda cha Zanzibar Milling, ambapo jumla ya tani 43,883 zilizalishwa na tani 9,656.75 zimeagizwa kutoka nje ya Zanzibar kwa mwaka 2021. Vile vile, jumla ya tani 7, 000 za sukari zimezalishwa na Kiwanda cha Sukari Mahonda ambapo jumla ya tani 28,704 ziliingizwa kutoka nje ya nchi,"amesema Rais Dkt.Mwinyi. 

Kwa upande wa biashara ya karafuu, Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, Serikali imeendelea kununua karafuu kutoka kwa wakulima kwa bei ya Shilingi 14,000 kwa kilo moja ya karafuu kavu za daraja la kwanza, Shilingi 13,000 kwa daraja la pili na Shilingi 12,000 kwa karafuu za daraja la tatu. 

Jumla ya tani 7,645.61 zenye thamani ya Shilingi bilioni 99.446 zilinunuliwa. Vile vile, jumla ya tani 1,658.75 za makonyo zenye thamani ya Shilingi bilioni 2.487 zimenunuliwa kutoka kwa wakulima. 

Kwa upande wa mauzo, amesema Serikali imeuza jumla ya tani 6,585 za karafuu zenye thamani ya Dola za Kimarekani 49,387,500. Vile vile, katika kipindi cha mwaka 2021 (Januari- Disemba), Serikali imelipa madeni ya muda mrefu ya wanunuzi wa karafuu yenye thamani ya USD 2,894,550, sawa na Shilingi bilioni 6,657,465,000.

Kuhusu biashara ya zao la mwani, Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa,katika kipindi cha Januari hadi Disemba 2021, Serikali imenunua kutoka kwa wakulima tani 43.95 za mwani kwa gharama ya TZS 37,995,600.00; ambapo kwa mwani aina ya Cottonii Serikali ililipa Shilingi 1,800 kwa kilo moja na bei ya Shilingi 700 kwa kilo moja aina ya Spinosum. Viwanda

Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, Serikali imeendelea kufanya juhudi za kuhakikisha kwamba, sekta ya viwanda inaimarika. Mchango wa sekta ya viwanda katika pato la Taifa umeongezeka kutoka asilimia 18.1 mwaka 2020 hadi kufikia asilimia 19.6 mwaka 2021.

Katika mwaka 2021, amesema kuwa, jumla ya viwanda ya sita vimezinduliwa na vitatu kuwekewa mawe ya msingi. Viwanda hivyo vinatarajia kutoa wastani wa ajira zipatazo 400. Mafanikio haya yanaonesha njia katika juhudi zetu za kuendeleza sekta ya viwanda hapa Zanzibar. 

"Serikali imeshawekeza jumla ya Shilingi bilioni 1.04 katika eneo la Viwanda la Chamanangwe - Pemba kwa kulipa fidia za wananchi wenye mashamba. Juhudi za kuweka miundombinu muhimu katika eneo hilo zinaendelea,"amesema Rais Dkt.Mwinyi. 

Uchumi wa Buluu ( Uvuvi Mafuta na Gesi)

Katika utekelezaji wa mpango mkakati wa Uchumi wa Buluu, Rais Dkt. Mwinyi amesema, Serikali imeshakamilisha na kutunga sheria ya sera muhimu kwa maendeleo ya uchumi huo. Serikali imeandaa mpango endelevu wenye thamani ya Shilingi bilioni 149 kwa ajili ya kuwawezesha wadau wa sekta ya Uchumi wa Buluu wakiwemo wavuvi na wafugaji wa mazao ya baharini Zanzibar. 

Amebainisha kuwa, awamu ya kwanza ya mpango huo tayari imeshatengewa jumla ya Shilingi bilioni 36.5, ikiwa ni sehemu ya Fedha za Mkopo kwa ajili ya kuimarisha uchumi baada ya kuathirika kutokana na maradhi ya UVIKO 19. 

Aidha, taratibu za manunuzi ya jumla ya boti 577 za Uvuvi, boti 500 za wakulima wa mwani na vifaa mbali mbali zimekamilika. Kazi inayoendelea hivi sasa ni kuwapatia mafunzo wadau wa sekta ya Uvuvi ili waweze kuzitumia vizuri nyenzo muhimu watakazopatiwa.

"Awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mpango wa kuwawezesha wadau wa sekta ya Uvuvi utawanufaisha moja kwa moja jumla ya wananchi 26,000 mpango huo utawajumuisha wavuvi 5,777, wakulima wa mwani 5,000, wafugaji wa samaki 400, wafugaji wa kaa 110, wafugaji wa majongoo bahari 160 na wastani wa wajasiriamali wa madagaa wapatao 10,000. Aidha, faida za ujumla za mpango huo zinatarajiwa kuwafikia wananchi wapatao 130,000,"amesema. 

Miundombinu ya kiuchumi

Rais Dkt.Mwinyi amefafanua kuwa, jitihada zimefanywa katika kuimarisha miundombinu ya kiuchumi nchini. 

Amesema, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na Serikali ya Japan kupitia Shirika la Maendeleo la Japan (JICA) inakamilisha ujenzi wa diko na soko jipya la samaki katika eneo la Malindi kwa thamani ya Shilingi bilioni 24. 

Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi amebainisha kuwa, fedha hizo zimechangiwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ambayo imetoa jumla ya Shilingi bilioni 3.6 na Serikali ya Japan imetoa Shilingi bilioni 21.4. 

Aidha, soko hilo la kisasa litawekewa miundombinu ya mitambo ya barafu na litaweza kuhudumia wafanyabiashara na wananchi wasiopungua 6,500 kwa wakati mmoja. 

Vile vile,amesema Serikali imefanikiwa kupata jumla ya Dola za Marekani Milioni 8.8 kati ya Dola za Kimarekeani milioni 58.8 zilizotolewa na Shirika la Kimataifa la Maendeleo ya Kilimo (IFAD) kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. 

Fedha hizo amesema, zitatumika kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa kuweka miundombinu ya usarifu wa samaki, kuendeleza zao la mwani, kujenga vituo viwili vya kutoa taaluma ya uvuvi Unguja na Pemba pamoja na kununua meli za uvuvi nne ili kuongeza uzalishaji wa samaki nchini. 

Mafuta na gesi 

Kwa upande wa sekta ya mafuta na gesi, amesema, mwekezaji amekamilisha awamu ya kwanza ya utafutaji wa mafuta na gesi asilia kwa njia ya 2D na sasa yupo katika mchakato wa kuendelea na utafutaji mafuta na gesi asili kwa njia ya 3D katika maeneo ya bahari na nchi kavu katika visiwa vya Unguja na Pemba. 

Sambamba na hatua hiyo,Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, Mamlaka ya Usimamzi ya Udhibiti wa Utafutaji na Uchimbaji wa mafuta na gesi asilia (ZPRA) imeendelea na matayarisho ya ugawaji wa vitalu vipya kwa ajili ya kufungua maeneo mapya ya uwekezaji. 

"Katika kipindi cha mwaka 2021, Serikali imefanya juhudi kubwa katika kuendeleza miundombinu ya barabara. Ujenzi wa barabara ya Kinduni Kichungwani Kitope (km 4) na barabara ya Sharifu msa- Mwanyanya- Bububu skuli (km 3.8) umefanywa kwa kiwango cha lami. Aidha, barabara za Kwahajitumbo - Mlandege hadi Mbuyu Taifa na barabara ya Hospitali ya Global Mnazi mmoja zimefanyiwa matengenezo makubwa.

"Aidha, Serikali imeingia mkataba na mkandarasi wa ujenzi wa barabara za ndani zenye urefu wa km. 300 na mkataba wa ujenzi wa barabara ya Wete Chake (km 22.1). Vile vile, kazi ya upembuzi yakinifu imekamilika kwa ajili ya ujenzi wa barabara mbalimbali zikiwemo za Kitogani Paje (km. 11), Mahonda Donge Mkokotoni (km .13), Dunga Kipilipini Pongwe hadi Chwaka Spur (km.30) na Kinyasini- Kiwengwa (km.13). Nyengine ni barabara ya Mshelishelini Pwani Mchangani (km.7.5), Muyuni- Nungwi (km.12) na Kizimkazi Makunduchi (km. 13). Hatua ya kutafuta fedha kwa ajili ya barabara hizo kutoka kwa washirika wa maendeleo inaendelea,"amefafanua Rais Dkt.Mwinyi.

Akizungumzia kuhusu bandari na usafiri wa baharini,Rais Dkt.Mwinyi amesema jitihada kubwa zimefanywa na Serikali katika kuhakikisha bandari zinaongeza ufanisi na mchango wake wa mapato katika uchumi. 

Rais Dkt.Mwinyi amesema, Serikali imeendeleza mpango Mkuu wa Ujenzi wa Bandari jumuishi ya Mangapwani, ambao upo katika hatua ya mapitio kwa ajili ya kuanza kwa mchakato wa kuwapata wawekezaji wa ujenzi wa bandari hiyo kubwa ya kisasa. Aidha, ujenzi wa gati katika bandari ya Mkokotoni umekamilika.

Vile vile, Mamlaka ya Usafiri Baharini Zanzibar (ZMA) imeruhusiwa tena kusajili meli za Kimataifa baada ya kukosekana kwa muda kwa fursa hiyo ambayo inachangia mapato ya Serikali na kutoa fursa kwa mabaharia wa Zanzibar kuweza kupata ajira katika meli tunazozisajili.

"Katika kuimarisha viwanja vya ndege na usafiri wa anga, kazi ya ujenzi wa jengo jipya la abiria la Uwanja wa Ndege wa Abeid Amani Karume Terminal 3 imekamilika na Serikali imesaini mkataba na Kampuni ya DNATA ya Dubai kwa ajili ya kuendesha uwanja huo.

"Hatua hii ya Serikali ina lengo la kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora uwanjani hapo zinazoendena na viwango vya Kimataifa, na kuongeza mapato Serikalini. Kuhusu uwanja wa ndege wa Pemba, hatua ya kufanya upembuzi yakinifu imekamilika. Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango tayari imeshatiliana saini (MoU) na Kampuni ya PROPAV ya Hispania ambayo imeonesha nia ya kujenga uwanja huo.

"Kwa lengo la kuimarisha huduma na kuwa na uhakika wa nishati ya umeme, Serikali imeingia makubaliano na Benki ya Dunia kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi wa Uimarishaji na Uboreshaji wa Sekta ya Nishati Zanzibar. 

"Mradi huo utakaogharimu jumla ya Dola za Kimarekani Milioni 142, utajumuisha ujenzi wa laini ya umeme yenye uwezo wa 132 KV. Vile vile, utahusisha miundombinu ya kuzalisha umeme wa jua MW 18 ambapo maeneo ya vijiji vya Makunduchi, Paje na Matemwe kwa Unguja na Mwambe na Micheweni kwa Pemba, yanapendekezwa kujengwa vituo vya kuzalisha umeme huo. Utekelezaji wa mradi huo utakuwa na mchango mkubwa katika kueneza huduma za umeme katika maeneo na vijiji ambavyo bado havijafikiwa na huduma hiyo. 

"Kadhalika, Serikali imetenga jumla ya TZS bilioni 11.00 kati ya Fedha za Mkopo wa IMF kwa lengo la kuzitafutia ufumbuzi changamoto zilizojitokeza kwenye sekta ya umeme. Fedha hizo zitatumika kwa ajili ya kuwapunguzia wananchi gharama za uvutaji umeme. 

"Wastani wa wateja elfu thelathini (30,000) wanatarajiwa kufikiwa na kunufaika na mpango huo. Mpango huu utajumuisha ujengaji wa miundombinu ya umeme mkubwa pamoja na ununuzi wa vifaa mbali mbali vitakavyotumika katika kazi hizo. 

"Katika mpango huu, muombaji wa umeme atachangia Shilingi 200,000 badala ya Shilingi 600,000. Gharama zilizobaki, zitafidiwa na Serikali. Lengo la uamuzi huu wa Serikali ni kuwapunguzia wananchi wetu gharama hizo na kuweza kumudu huduma hiyo muhimu kwa maisha ya kila siku,"amefafanua kwa kina Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi.

Ardhi na Makazi

Mheshimiwa Rais Dkt. Mwinyi amesema kuwa, kwa lengo la kuimarisha matumizi bora ya ardhi na utekelezaji wa mipango miji, Serikali imeyaorodhesha baadhi ya maeneo na kuyaweka katika ardhi ya akiba kwa ajili ya matumizi maalum ya baadae. Hatua hiyo, imelenga kupunguza migogoro ya ardhi, uvamizi wa maeneo, utunzaji wa mazingira na kuimarisha haiba ya miji na vijiji vyetu. 

"Maeneo ambayo yameshapimwa kwa malengo hayo hasa makaazi yapo Kibele kwa Unguja na Mfikiwa na Finya huko Pemba. Aidha, Serikali imeshapima na kutenga maeneo maalum kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda vidogo na vya kati; Dunga hekta 61 na Pangatupu hekta 135. 

"Vile vile, katika kufanikisha dhana ya Uchumi wa Buluu, Serikali tayari, imeshatenga eneo kwa ajili ya bandari huko Kizimkazi lenye ukubwa wa hekta 24 na maeneo ya Viwanda vya kusarifu samaki huko Fungurefu lenye ukubwa wa hekta 6.

"Kwa lengo la kukabiliana na migogoro ya ardhi, katika mwaka 2021, jumla ya migogoro ardhi 197 imepatiwa ufumbuzi na Mahakama ya Ardhi na migogoro 301 imeshughulikiwa na Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makaazi. Aidha, Serikali imeunda Tume maalum kwa ajili kushughulikia migogoro ya ardhi kwa ufanisi zaidi. Kwa pamoja, tuipe Tume hiyo ushirikiano unaohitajika ili iweze kutekeleza majukumu kwa ufanisi,"amesema Rais Dkt.Mwinyi. 

Kilimo

Amesema, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika sekta ya Kilimo ni miongoni mwa mambo yaliyozingatiwa na serikali katika mwaka 2021, imefanikiwa kutekeleza kwa asilimia 85, mradi wa ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji katika hekta 1,053 kwa mabonde 6 ya Unguja na Pemba. 

Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, mradi huo wa ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji maji ni Mkopo kutoka EXIM Bank ya Korea na unatarajiwa kukamilika mwezi Aprili, 2022.

"Utekelezaji wa miradi huo umelenga kuongeza uzalishaji wa mpunga hapa Zanzibar kwa kuondokana na kilimo cha kutegemea mvua. 

"Shughuli za utafiti zinaendelea kutiliwa mkazo kwa lengo la kuchochea mapinduzi katika sekta ya kilimo. Ni taarifa njema kuwa mtafiti wetu wa Taasisi ya Utafiti wa kilimo Zanzibar, Ndugu Salum Faki Hamadi ametunukiwa Tuzo ya Kimataifa ya Mwana sayansi bora kwa uzalishaji wa mbegu za mpunga kutoka Shirika la Nguvu za Atomiki lenye makao makuu yake Vienna- Austria. Tunampongeza kwa mafanikio hayo na kuitangaza nchi yetu kimataifa,"amesema. 

Huduma za kijamii 

Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, uimarishaji wa huduma za jamii zikiwemo elimu, afya na maji safi na salama ni miongoni mwa vipaumbele vya Serikali ya Awamu ya Nane kwa kuendeleza jitihada zilizoanzishwa na uongozi wa Awamu zilizotangulia katika kuhakikisha wananchi wa Zanzibar wanapata huduma hizo.

"Kwenye sekta ya elimu, katika kukabiliana na tatizo la uhaba wa madawati katika skuli zetu, Serikali imenunua jumla ya seti za viti na meza 35,610 kutoka nchini China. Seti hizo zimeshawasili nchini na zinatarajiwa kusambazwa Unguja na Pemba ili kutatua tatizo la uhaba wa vikalio katika Skuli za Sekondari za Serikali. 

"Kadhalika, Serikali imenunua jumla ya kompyuta 1,364 na kuzisambaza katika vituo 22 vya ubunifu kwa lengo la kushajiisha ufundishaji na matumizi ya TEHAMA.

"Kwa lengo la kuzifanyia kazi changamoto ziliopo katika sekta ya elimu, Serikali imetenga jumla ya Shilingi bilioni 69.0, sawa na Dola za Kimarekani bilioni 30 za mkopo shirika la IMF za UVIKO - 19.

"Kwa kutumia fedha hizo, Serikali itakamilisha ujenzi wa madarasa 425 yaliyoanzishwa kwa nguvu za wananchi. Shughuli hii itagharimu jumla ya Shilingi bilioni 7.656. 

"Vile vile, tumepanga kujenga madarasa mapya 706 katika Wilaya zote 11 Unguja na Pemba kwa ngazi ya Maandalizi, Msingi na Sekondari. Madarasa haya yanajumuisha ujenzi wa madarasa mapya na yale ambayo yatajengwa kupitia ujenzi wa skuli mpya 35 zikiwemo skuli 22 za maandalizi (skuli 2 kwa kila Wilaya) na skuli 13 za Msingi na Sekondari Unguja na Pemba.

"Skuli saba (7) kati ya hizi zitakuwa ni za ghorofa na zitajengwa katika maeneo ya Mwanakwerekwe, Mtopepo, Bweleo na Kwahani kwa Unguja na Mwambe, Kwale na Makangale kwa Pemba. Aidha, skuli mbili zitajengwa eneo la Jendele kwa Unguja na Chake chake kwa Pemba ambazo zitakuwa ni maalum kwa ajili ya elimu mjumuisho. Maeneo mengine ya ujenzi wa skuli hizi ni Mpendae, Kipapo, Pujini na Mgelema. Ujenzi huu utagharimu jumla ya Shilingi bilioni 43.973.

"Vile vile, tumeamua kuelekeza jumla Shilingi bilioni 6.871 kwa ajili ya ujenzi wa vyoo 1,693 vya wanafunzi katika ngazi zote za elimu. Kadhalika, jumla ya Shilingi bilioni 7.898 zitatumiwa kwa kufanya ukarabati wa skuli 22. Skuli zitakazofanyiwa matengenezo makubwa ni skuli ya Haile Sellasie, Chaani, Mlimani, Matemwe na Uzini kwa Unguja na Skuli ya Konde, Chasasa na Kiwani Mauwani kwa upande wa Pemba,"amefafanua Rais dkt.Mwinyi.

Pia amesema, watanunua madawati 8,000 (madawati ya wanafunzi watatu) kwa ajili ya skuli za msingi yatakavyogharimu jumla ya Shilingi bilioni 2. 

"Pia, tutajenga jumla ya nyumba 10 za walimu katika maeneo ya visiwa vidogo vidogo vikiwemo Tumbatu, Uzi, Njau, Kokota na Ngambwa. Ujenzi huo utagharimu jumla ya Shilingi milioni 600.

"Serikali itatumia wakandarasi wakubwa wa daraja la I, II na III kuhakikisha ujenzi huu unakuwa wenye ubora mzuri. 

"Taratibu za kuwapata wakandarasi hao zinaendelea. Aidha, gharama zote za ujenzi kwa kila skuli pamoja na michoro ya majengo imekamilika. Serikali ina matengemeo makubwa ya mafanikio ya utekelezaji wa miradi yote hii na hatimae kuweza kutoa elimu bora kwa watoto wetu ambao ndio warithi wa Taifa letu. 

"Katika hatua nyingine, Serikali imeamua kurudisha tena darasa la saba kama zamani kwa kuzingatia maoni ya wadau wengi wa elimu na wazazi hali ambayo itawapa fursa watoto wa Zanzibar kupata elimu ya msingi kama ilivyokuwa zamani. Vile vile, hatua hiyo inalenga kuwapa fursa nzuri Zaidi wanafunzi ya kujitayarisha na mitihani ya Taifa.

"Kwa lengo la kuimarisha uwezo wa wahitimu wa Chuo Kikuu cha SUZA na kiwango cha elimu kinachotolewa na chuo hicho, Serikali kwa ufadhili wa Benki ya Dunia inaendelea na hatua za kuimarisha miundombinu ya Chuo hicho. Mradi huo utagharimu jumla ya Dola za Kimarekani Milioni 20.

"Jitihada zimefanywa ili kuhakikisha hudumba za afya zinatolewa katika Hosptali na vituo vya afya zimekuwa bora. Serikali imeimarisha miundombinu ya afya. upatikanaji wa dawa na vifaa tiba pamoja na kuongeza idadi ya madaktari, wauguzi na wataalamu wengine wa sekta hiyo. 

"Kwa lengo la kutatua changamoto zinazoikabili sekta ya afya na kuweza kuimarisha vyema sekta hii, tumetenga jumla ya Shilingi bilioni 69, zinazotokana na Shilingi bilioni 230 za Mkopo wa IMF. Tumepanga kutumia kiwango hicho kutekeleza miradi ya kuimarisha miundombinu ya afya ikiwemo ujenzi wa hospitali mpya ya ngazi ya Mkoa katika Mkoa wa Mjini Magharibi katika eneo la Lumumba. Hospitali hiyo itakuwa na uwezo wa kulaza wagonjwa 200 kwa wakati mmoja na itakuwa ya ghorofa tano.

Hospitali hiyo itawekwa vifaa tiba vya kisasa, ikiwa ni pamoja, CTscan, MRi, Huduma za Uchunguzi wa Maabara za Kisasa na huduma za afya za dharura. Aidha, itakuwa na uwezo wa kutoa huduma mbali mbali za kibingwa pamoja na huduma za macho na meno. Itakuwa na kliniki na wodi za kulaza wagonjwa mbali mbali kwa nia ya kuongeza wigo wa kutoa huduma bora na kupunguza idadi ya watu wanaokwenda Hospitali ya Mnazi Mmoja ambayo nayo itaendelea kuboreshwa kupitia msaada wa Benki ya Jumuiya ya Nchi za Kiarabu- (BADEA) ili ikidhi hadhi yake ya kuwa Hospitali ya Rufaa. Ujenzi wa Hospitali mpya ya Lumumba utagharimu jumla ya Shilingi bilioni 14. Ujenzi huo utaanza mara moja.

Sambamba na hilo, Serikali imeamua kwa makusudi kutumia fedha hizo za IMF kuiboresha kwa kuipatia vifaa vya kisasa na madaktari wataalamu wa kutosha Hospitali ya Abdalla Mzee iliopo Mkoani Pemba na kuipandisha hadhi kuwa ni Hospitali ya Mkoa ili iweze kutoa huduma bora kwa wananchi wa Mkoa wa Kusini na Kisiwa cha Pemba kwa ujumla.

Pamoja na ujenzi huo, Serikali itajenga hospitali 10 katika ngazi ya Wilaya zenye uwezo wa kulaza wagonjwa 100 kwa wakati mmoja kila moja, pamoja na kujenga nyumba za wafanyakazi zitakazotosha kuhudumia familia 16 kwa gharama ya Shilingi bilioni 22.00. Hospitali hizo zitajengwa katika Wilaya zote Unguja na Pemba isipokuwa kwa Wilaya ya Mkoani ambapo itahudumiwa na Hospitali ya Mkoa. Hatua za ujenzi wa hospitali hizi zimeshaanza katika maeneo mbali mbali ya Wilaya zote.

Hospitali hizi zitatoa huduma za uchunguzi kwa kutumia vifaa vya kisasa (X-ray ya kijiditali, Utrasound, na maabara za kisasa). Huduma zitakazopatikana katika Hospitali hizi ni za ICU au wodi maalum kwa wagonjwa wanaohitajia uangalizi wa karibu, magonjwa ya wanawake, upimaji wa mimba, uzazi wa kawaida na huduma za upasuaji.

Kadhalika, Serikali itanunua gari 12 za kubeba wagonjwa (ambulances). Gari hizo zitasambazwa katika hospitali zote za Wilaya na mbili za Mkoa. Vile vile, Serikali itanunua gari 5 za kusambazia dawa katika hospitali na vituo vya afya Unguja na Pemba kutoka Bohari ya Dawa. Huduma hii itaondosha gharama zinazotumika hivi sasa za kukodi gari za kampuni binafsi kwa kufanya kazi hiyo na pia kuhakikisha usalama wa dawa na vifaa tiba vinavyosafirishwa.

Aidha, Serikali itanunua mitambo ya kuchomea taka za Hospitali (Incinerators) kwa hospitali zote za Wilaya na Mikoa. Aidha, kati ya mitambo hiyo, miwili itakuwa ni yenye uwezo mkubwa wa kuchoma taka hatarishi nyingi kwa wakati mmoja na itafungwa katika hospitali za Mikoa ili iweze kutoa huduma kwa hospitali za karibu za Serikali na pia sekta binafsi.

Huduma za damu salama zitaimarishwa kwa kupatiwa vitendea kazi muhimu vinavyoendana na mahitaji husika ili kuweza kutoa huduma muda wote, hali ambayo kwa sasa, kitengo cha damu salama hakina vifaa hivyo. Uwepo wa vifaa hivyo utaongeza upatikanaji wa damu wa kuridhisha iliyopimwa na kuwa tayari kupewa wagonjwa wanaohitaji.

Serikali itanunua pia mitambo miwili katika Hospitali za Pangatupu na Abdalla Mzee ya kuzalisha gesi tiba (oxygen), kila mmoja ukiwa na uwezo wa kuzalisha mitungi 400 kwa siku, itakayotumika kwenye hospitali nyengine Unguja na Pemba zitakazohitaji huduma hii.

Matarajio yetu ni kwamba faida zitakazopatikana baada ya kukamilika miradi hii ni kuwa na huduma za Afya zilizo bora karibu na wananchi. Vile vile, tutaweza kutekeleza dhamira yetu ya kupunguza idadi ya wagonjwa wanaosafirishwa nje ya Zanzibar kwa kufuata matibabu.

Katika mwaka 202I, Serikali imeongeza kasi katika mapambano dhidi ya maradhi ya UVIKO 19. Huduma za chanjo dhidi ya maradhi hayo zilianza kutolewa rasmi tarehe 17 Juni, 2021. Juhudi kubwa zimefanywa ya kusogeza vituo vinavyotoa huduma hiyo karibu na wananchi na meneo ya utalii, ambapo hadi hivi sasa jumla ya vituo vituo 41 vimeshafunguliwa; kati ya hivyo 29 viko Unguja na 12 viko Pemba. Kwa mara nyengine, nawahimiza wananchi tuendelee kuchukua hadhari dhidi ya maradhi ya UVIKO 19 ambayo bado yanaendelea kuwa ni tishio kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii duniani kote. 

Katika mwaka uliopita, jumla ya wafanyakazi wa kada mbali mbali za afya 243 wamemaliza masomo na kurejea kazini. Aidha, jumla ya wafanyakazi 135 wameajiriwa kwa njia ya mikataba. Wafanyakazi hawa watasaidia sana kupunguza tatizo la uhaba wa wafanyakazi wa sekta ya afya na kuimarisha upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi. 

Mafanikio yameendelea kupatikana nchini katika kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi kutokana na Serikali kuchukua hatua za kuziimarisha huduma hizo. Vifo vinavyotokana na uzazi vimepungua na kufikia 120 kwa kila vizazi hai 100,000 kwa mwaka 2020 ikilinganishwa na vifo 166 kwa kila vizazi hai 100,000 kwa mwaka 2019. Takwimu zinaonesha kuwa asilimia ya waja wazito wanaojifungulia katika vituo vya afya imeongezeka kutoka 65.8 mwaka 2019 hadi asilimia 66.3 mwaka 2020. 

Upatikanaji wa huduma za maji safi na salama ni miongoni mwa vipaumbele vya Serikali kwa kuzingatia kuwa maji ni uhai. Serikali imeanza utekelezaji wa Mradi wa Uhuishaji wa Mfumo wa Usambazaji Maji Zanzibar.

Mradi huu unagharimu jumla ya Dola za Kimarekani Milioni 92.18 ambazo ni mkopo kutoka Benki ya Exim ya India. Mradi huu ambao utekelezaji wake ushaanza, unatarajiwa kukamilika baada ya kipindi cha miezi 18 na utakuwa na jumla ya visima vya maji 64, matangi ya chini ya ardhi 7 na matangi ya juu 8. Mradi huu unatekelezwa katika Wilaya tatu ambazo ni Magharibi A, Magharibi Bna Wilaya ya Kati na utawanufaisha wananchi wa Shehia 36. 

Katika kipindi hiki, Serikali kupitia ZAWA imefanikiwa kurudisha huduma ya maji safi na salama katika maeneo 25 sawa na asilimia 89 ya malengo ya kufikia maeneo 28. Hatua hii imefikiwa baada ya kununua na kufunga pampu mpya 50 katika visima vilivyokuwa na hitilafu. 

Kwa kutumia fedha za mkopo nafuu kutoka IMF, tumetenga jumla ya Shilingi bilioni 34.2 kwa ajili ya kuimarisha sekta ya maji. Fedha hizo zitatumika kwa uchimbaji na uendelezaji wa visima, ununuzi wa pampu na vifaa pamoja na ujenzi na ukarabati wa matangi katika sehemu mbali mbali za Unguja na Pemba. 

Wito wangu wananchi waendelee kuwa na subira wakati jitihada za kukabiliana na changamoto ya huduma ya maji safi na salama zinaendelea. Aidha, nawaomba wananchi kuwapa ushirikiano wakandarasi wa miradi ya maji wakati huu ambao shughuli mbali mbali zinaendelea kutekelezwa katika maeneo yenu ya makaazi,"amesisitiza Rais Dkt.Mwinyi. 

Utumishi na utawala bora

Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, atika kipindi cha mwaka mmoja, Serikali imechukua hatua mbali mbali za kuimarisha utawala bora. 

"Tumeendeleza mapambano dhidi ya rushwa na ubadhirifu wa mali ya umma na kuweka mkazo katika nidhamu ya matumizi ya fedha ya Umma. Serikali imechukuwa hatua dhidi ya watuhumiwa wa fedha za Serikali wasio zingatia matakwa ya kisheria na taratibu.

Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu wa Uchumi Zanzibar (ZAECA) imepokea tuhuma 289 za makosa ya rushwa na uhujumu wa uchumi katika mwaka 2021. Majalada 29 ya kesi hizo yamefikishwa kwa Mkurugenzi wa Mashataka (DDP) na kesi 4 zimetolewa maamuzi. 

Kazi ya uchunguzi kwa kesi nyengine zilizobakia inaendelea. Vile vile, katika kipindi hiki, jumla ya Shilingi 341,666,695 zinazohusiana na makosa mbali mbali zimeokolewa na kurejeshwa Serikalini kutoka Mamlaka ya kuzuia Rushwa na Uhujumu wa Uchumi Zanzibar.

Katika kuimarisha mazingira ya kufanyia kazi ya muhimili wa Mahakama, Serikali imekamilisha mradi wa jengo la Mahakama Kuu lilioko Tunguu ambalo nimelizindua rasmi tarehe 9 Januari, 2022. Jengo hilo ni kichocheo cha kuimarika kwa ubora na ufanisi wa kazi za Mahakama na litarahisisha upatikanaji wa haki za kisheria kwa wananchi. 

Aidha, kwa lengo la kukabiliana na tatizo la udhalilishaji Serikali imeanzisha Mahakama maalumu ya kusikiliza kesi zinazohusiana na udhalilishaji,"amesema.

Hifadhi ya jamii na kuyaendeleza makundi maalum

Serikali imeendeleza utaratibu wa kuwapatia posho wazee wote waliofikia umri wa miaka 70. Hadi kufikia mwezi Disemba 2021, Rais Dkt. Mwinyi amesema kuwa, jumla ya wazee 28,953 wamesajiliwa na kulipwa pencheni. Aidha, kupitia Mpango wa kunusuru kaya maskini (TASAF III) kwa upande wa Zanzibar, katika kipindi cha mwaka uliomalizika, jumla ya Shilingi 4,541,763,530 zilizotolewa kwa walengwa Unguja na Pemba. 

"Kuhusu hifadhi ya jamii dhidi ya udhalilishaji, kati ya Januari hadi Septemba 2021, jumla ya matukio ya ukatili na udhalilishaji kijinsia 928 yameripotiwa katika vyombo vya sheria. 

"Idadi hiyo imepungua ikilinganishwa na matukio 1,363 yaliyoripotiwa katika kipindi kama hicho mwaka 2020. Nawasihi wananchi tuendelee kushirikiana katika kukomesha vitendo hivyo vya aibu. Serikali itaendelea kuchukua hatua za ufuatiliaji wa kesi katika vituo vya Polisi na Ofisi za Mkurugenzi wa Mashtaka, kutoa ushauri nasaha kwa waathirika na kuhakikisha Mahakama maalum iliyoanzishwa dhidi ya vitendo vya udhalilishaji inafanya kazi kwa ufanisi,"amesema Rais Dkt.Mwinyi.

Kuhusu mapambano dhidi ya dawa za kulevya,Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, tayari Baraza la Wawakilishi limejadili na kupitisha mswada wa Sheria ya kuundwa kwa Mamlaka yenye nguvu za kisheria za kuchunguza, kukamata, na kushtaki Mahakamani washukiwa wote wa dawa za kulevya Zanzibar.

Amesema, hatua hii ina lengo la kuokoa maisha ya vijana wetu dhidi ya matumizi ya dawa za kulevya kutokana na athari kubwa tunazozipata ikizingatiwa kuwa vijana ndio tegemeo la nguvu kazi ya Taifa. 

Mazingira

Pia amesema, katika hifadhi ya mazingira na athari zinazotokana na mabadiliko ya tabia nchi, hatua mbalimbali zimechukuliwa na Serikali katika kukabiliana na hali hiyo. 

Serikali imechukua hatua za kuhami maeneo yaliyoathiriwa kwa mmononyoko wa fukwe na uingiaji wa maji ya chumvi katika maeneo ya kilimo na makaazi ya watu. 

Amesema, kwa sasa, kazi ya ujenzi wa ukuta wenye urefu wa mita 500, inaendelea katika ufukwe wa bahari ya Msuka Pemba. Vile vile, ujenzi wa tuta lenye urefu wa mita 450 unatarajiwa kuanza karibuni katika eneo la bonde la kilimo la Tovuni Mkoa wa Kaskazini Pemba. 

"Katika kuzingatia haki za makundi maalum na kuwasaidia kimaisha, Serikali imeendelea kusimamia haki na fursa za watu wenye Ulemavu Zanzibar. 

"Katika kufikia azma hiyo, Serikali kupitia Mfuko wa uwezeshaji wananchi Kiuchumi imeamua kuwajumuisha Watu wenye Ulemavu kuwa ni miongoni mwa makundi yatakayonufaika na uwezeshaji huo. Aidha, katika kipindi cha mwaka mmoja uliomalizika, jumla ya visaidizi 532 vya aina mbali mbali vimetolewa kwa watu wenye ulemavu,"amesema.

Uwezeshaji wananchi kiuchumi

Amesema, kwa upande wa uwezeshaji wa wananchi wa makundi mbali mbali kiuchumi, ni miongoni mwa hatua za utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM, 2020 na ahadi walizozitoa katika kampeni za uchaguzi wa 2020. 

"Serikali inafahamu kwamba mahitaji ya wananchi ya kuwezeshwa kiuchumi ni makubwa zaidi ya uwezo wa Mfuko wa Uwezeshaji tangu ulipoanzishwa. 

"Kupitia Mfuko huo wa Uwezeshaji, jumla ya mikopo 1,080 yenye thamani ya Shilingi bilioni 1.3 imetolea kwa mwaka uliopita. Jumla ya ajira 11,045 zimezalishwa katika shehia mbali mbali za Unguja na Pemba kupitia mikopo hiyo. 

"Kwa lengo la kukuza ujasiriamali na kuondokana na tatizo kubwa la upatikanaji wa mitaji liliopo, Serikali imeamua kutenga jumla ya Shilingi bilioni 81.8, kwa ajili ya kuwaweza wajasiriamali na wafanyabiashara mbali mbali kwa kutumia fedha za Mkopo wa Shirika la Fedha la Dunia za UVIKO 19. 

"Hatua ya kwanza ya kuvihakiki vikundi vya ujasiriamali imeshafanyika, ambapo jumla vikundi 3,494, Unguja na Pemba, vimehakikiwa. Katika uhakiki huo imebainika kwamba jumla ya vikundi 2.907 vina sifa za kufaidika na mkopo huo na vikundi 587 vinahitaji kujengewa uwezo zaidi ili viweze kukopesheka. 

"Zoezi la kufanya usajili na utoaji wa mafunzo ni endelevu ili kutoa fursa kwa wananchi ambao wanataka kujishughulisha na ujasiriamali. 

"Kwa lengo la kuimairisha mazingira ya kufanya biashara, Serikali imewajengea soko la muda wafanyabiashara wadogo wadogo katika eneo la kibanda Maiti ambapo jumla ya watu 1,558 wataweza kuendesha shughuli zao katika eneo hilo. 

"Kadhalika, Serikali inaendelea na maandalizi ya ujenzi wa masoko mawili makubwa katika eneo la Chuini kwa Nyanya na Jumbi ambapo mikataba ya miradi itasainiwa mwezi huu. Vile vile, mradi wa ujenzi wa maduka ya kisasa kwa ajili ya wajasiriamali wadogo katika eneo la Darajani utaanza baada ya kukamilika kwa hatua ya kusaini mkataba na muwekezaji hivi karibuni. Tayari hatua za kulisafisha eneo hilo la ujenzi zimeanza.

Kadhalika,Serikali ilizindua mfumo wa usajili wa wajasiriamali tarehe 23 Septemba,2021 kwa lengo la kuondoa usumbufu wa tozo za mara kwa mara na kuwatambua rasmi wajasiriamali waliopo katika maeneo mbali mbali ya Unguja na Pemba. Hadi kufikia tarehe 17 Disemba 2021 , jumla ya wajasiriamali 14,118 wameshasajiliwa na kupatiwa vitambulisho vyao,"amefafanua Rais Dkt.Mwinyi. 

Habari, Michezo na Utamaduni

Katika sekta ya habari,Mheshimiwa Rais Dkt.Mwinyi amesema kuwa, Serikali kupitia Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) imeendelea kuwapatia wasikilizaji na watazamaji, habari za matukio mbali mbali ya Kitaifa na Kimataifa. 

Hatua hiyo imewawezesha wananchi kufahamu na kupata uelewa wa masuala mbali mbali ya kijamii, kiuchumi, kisiasa, michezo na burdani.

Katika kuendeleza shughuli za utamaduni na muziki, amesema matamasha mbali mbali ya utamaduni yameratibiwa kwa mafanikio yakiwemo Tamasha la 26 la Utamaduni wa Mzanzibari, Tamasha la ZIFF, Sauti za Busara, Tamasha la Mwaka Kogwa na Tamasha la Kimataifa la Muziki wa Taarab. 

Vile vile, Serikali kupitia Afisi ya Haki miliki imeendelea kusimamia haki za wasanii ambapo kazi 1,028 za wasanii zimesajiliwa. Pia, Mirabaha yenye thamani ya Shilingi Milioni 95.5 imekusanywa kutoka kwa watumiaji wa kazi zilizosajiliwa ambapo fedha hizo zimegawiwa na kuwanufaisha wasanii 1,500. 

Kwa upande wa sekta ya Michezo, amesema Serikali iliyaratibu kwa mafanikio mashindano ya Kombe la Mapinduzi katika maadhimisho ya miaka 57. 

Kadhalika, katika maadhimisho haya ya miaka 58, mashindano ya Kombe hilo yameandaliwa kwa mara nyingine kwa ufadhili wa wadau wa michezo. Napenda niwapongeze wadhamini wa Mashindano haya kwa kuonesha moyo wa uzalendo na kuhakikisha yanazidi kupata msisimko na kuwa moja wapo wa matukio muhimu katika sherehe hizi muhimu kwa Taifa.

"Nalipongeza Shirika Utangazaji Zanzibar (ZBC) kwa kuendelea kuyaratibu Mashindano yaliyopata umaarufu mkubwa ya Yamle Yamle na mashindano ya watoto ya Mapinduzi. 

"Mashindano hayo yana mchango mkubwa katika kukuza na kuendeleza vipaji. Kadhalika, kwa mara nyengine tumeweza kufanya Bonanza la Kitaifa la kuhamasisha kufanya mazoezi kwa mafanikio na kushirikisha wanamichezo zaidi ya elfu saba kutoka vikundi mbali mbali vya Zanzibar na Mikoa ya Tanzania Bara,"amesema Rais Dkt.Mwinyi.Sensa

Amesema, moja kati mambo muhimu waliyoyatekeleza katika mwaka 2021 ni matayarisho ya Sensa ya Watu na Makaazi ya 2022. 

Hadi kufikia Disemba 2021, matayarisho hayo yalikuwa yamefikia asilimia 65 ya kazi yote, ambapo zoezi la majaribio lilifanyika mwezi Septemba 2021 katika maeneo 10 yaliyochaguliwa Unguja na Pemba na kazi ya uchambuzi inaendelea. 

"Natoa wito kwa wananchi sote tuhakikishe tunashiriki zoezi hilo wakati litakapofanyika kwa kutoa taarifa sahihi ili tuweze kupanga na kutekeleza mipango yetu ya maendeleo kwa uhakika na ufanisi zaidi,"amebainisha. 

Uhusiano na diplomasia

Amesema kuwa, wakati nchi inaadhimisha miaka 58 ya Mapinduzi ya mwaka 1964, "tunafurahia kuendelea kuimarika kwa Muungano wetu wa Tanzania kwa kufanikiwa kudumisha uhusiano wetu wa kihistoria na wa damu wa wananchi wa pande hizi mbili za Jamhuri ya Muungano. Serikali zetu kwa jitihada kubwa zimekuwa zikichukua hatua mbali mbali za kukabiliana na changamoto za Muungano.

"Kadhalika, katika kipindi cha mwaka mmoja wa Serikali ya Awamu ya Nane tumeimarisha uhusiano kwa kufanya mazungumzo na wageni mbali mbali wakiwemo Mabalozi, Wawakilishi wa Serikali na Taasisi za Kimataifa pamoja na watu mashuhuri, wanamichezo na wasanii. 

"Wageni wote hawa wamevutiwa na hali ya usalama iliopo na wameonesha utayari wao wa kushirikiana na Zanzibar katika masuala mbali mbali ya maendeleo na ustawi wa jamii. Aidha, tumeweza kupata ushirikiano mzuri miongoni mwa wana Diaspora kwa kuonesha dhamira yao ya kusaidia maendeleo ya Zanzibar. Serikali itaendelea kutoa ushirikiano kwa Serikali za Mataifa mbali mbali, taasisi na wadau wote wa maendeleo kwa lengo la kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia."Nichukue fursa hii kutoa shukurani zangu kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutuongoza vizuri, na kwa kunipa ushauri katika masuala muhimu ya maendeleo yetu. 

"Vile vile, natoa shukurani kwa viongozi wa ngazi zote, watendaji na watumishi wa Serikali pamoja na wananchi wote kwa jitihada zenu katika kuleta maendeleo ya nchi yetu. 

"Ni vyema tuongeze kasi katika kutekeleza wajibu wetu kwa misingi ya haki, uadilifu, mapenzi na mshikamano. Sote tuamini kuwa mafanikio na maendeleo tunayoyadhamiria yanategemea mchango wa kila mmoja wetu kutekeleza wajibu wake ipasavyo.

"Natoa shukurani kwa Halmashauri ya Sherehe na Maadhimisho inayoongozwa na Makamu wa Pili wa Rais, Mheshimiwa Hemed Suleiman Abdulla, Wajumbe wake wote, Makamanda na wapiganaji wa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama, watendaji mbalimbali wa Serikali na taasisi binafsi, waandishi wa habari, wanamichezo na wasanii kwa mchango wa kila mmoja wao katika kufanikisha sherehe za maadhimisho ya miaka 58 ya Mapinduzi. 

"Shukurani maalumu nazitoa kwa wananchi kwa kuonesha furaha na kushiriki katika matukio mbalimbali yaliyoandaliwa katika maadhimisho haya.Wito wangu tuendelee kuwa pamoja katika siku ya kilele kesho kwenye uwanja wa Amani na ili tudhihirishe kuyathamini, kuyaenzi na kuyadumisha Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964,"ameeleza Rais Dkt.Mwinyi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news