RC Pwani akagua viwanda vikubwa vya Lake, afunguka mambo mazito

NA ROTARY HAULE

MKUU wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge ameanza ziara ya kukagua viwanda mbalimbali vilivyopo mkoani humo huku akiahidi kushughulikia changamoto ya umeme inayowakabili baadhi ya wawekezaji wa viwanda hivyo.
Amesema,lazima wawekezaji wapate huduma ya umeme wa kutosha ambao utawasaidia katika kuendeleza uzalishaji wa bidhaa kwenye viwanda vyao kwa kuwa bila umeme hakuna uzalishaji.

Kunenge ametoa kauli hiyo leo katika ziara yake ya kutembelea viwanda vya Kampuni ya Lake vilivyopo Mjini Kibaha vinavyoshughulika na utengenezaji wa bidhaa mbalimbali.

Kunenge ameanza ziara hiyo kwa kutembelea kiwanda cha Aluminum Trailers Limited kinachotengeneza matenki ya kuhifadhia na kubebea mafuta, kiwanda cha mitungi ya gesi,matenki ya maji,bomba za plastiki,nondo na kiwanda cha Gypsum.
Aidha,katika ziara hiyo Kunenge alipokea changamoto ya kuwepo kwa umeme hafifu kutoka kwa wawekezaji hao wakieleza kuwa mara nyingi wanashindwa kuzalisha kutokana na umeme kuwa mdogo.

Kutokana na hali hiyo, Kunenge amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan inawajali wawekezaji kwa kuwa ndio chanzo cha mapato ya Taifa na hata ajira kwa Watanzania.

Amesema,suala la umeme tayari Serikali kwa kushirikiana na TANESCO wanaifanyia kazi changamoto hiyo na muda si mrefu ufumbuzi wake utapatikana na viwanda vitafanya uzalishaji kama ilivyokusudiwa.

"Binafsi niwapongeze kwa uwekezaji huu mkubwa katika mkoa wetu maana nimejionea kazi kubwa mnayofanya,na kazi hii inaleta tija katika Taifa letu ikiwemo ajira na hata kuongeza pato la nchi kwa hiyo niseme tu Serikali ipo pamoja nawe,"amesema Kunenge.
Amesema, uwekezaji uliofanywa na wawekezaji wa Kampuni ya Lake unatafsiri nia ya Serikali na inaonyesha Rais jinsi anavyofanyakazi na kwamba lazima wawekezaji hao wawekewe mazingira mazuri ya uzalishaji.

"Nimepita katika kiwanda hiki cha Lake Steel nimeona wanatengeneza nondo aina ya BS inayoendana na kiwango cha kimataifa na miradi mikubwa inayotekelezwa nchini nondo zote zimetoka hapa, kwa hiyo lazima tuwaunge mkono wawekezaji hawa,"amesema.

Amesema,kazi ya Serikali ni kutengeneza mazingira bora zaidi ili wawekezaji wapate kipato lakini hata Watanzania nao wapate ajira ndio Rais Samia anaendelea kusisitiza namna ya kuwajali wawekezaji waliopo nchini.

Kuhusu changamoto ya umeme, Kunenge amesema kuwa Serikali inafanya jitihada kubwa ili umeme huwe wa kutosha na kusababisha uwekezaji huwe bora zaidi huku akiwaomba kuwa na imani na Serikali yao.
Kunenge amewaomba Watanzania kuendelea kuwaunga mkono wawekezaji hao kwa kuhakikisha wananunua bidhaa zinazozalishwa na wawekezaji wa ndani ili kusudi wapate moyo wa kuzalisha zaidi.

Hata hivyo, Kunenge ametoa wito kwa taasisi za Serikali zilizopo ndani ya mkoa wake kuhakikisha wanaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji huku wawekezaji wafuate sheria za Serikali kwa kuwa kufanya hivyo itawafanya kuongeza mapato.

Afisa rasilimali watu wa kiwanda cha Aluminum Trailers Limited, Hussein Ally amesema kuwa, kiwanda chao kinazalisha tenki 15 kwa mwezi huku wakitoa ajira kwa Watanzania 90.

Ally ameishukuru Serikali kwa kutengeneza mazingira rafiki kwa wawekezaji wa Tanzania na huku akiomba Serikali ifanyie kazi changamoto zao ikiwemo umeme.

Naye Fadhili Msemwa,Afisa Uajiri wa kampuni ya Lake Group amesema, kampuni yake mpaka sasa imeajiri watu 400 ambapo hata hivyo amemshukuru Mkuu wa Mkoa kwa kufanya ziara hiyo kiwandani hapo na kuomba ziara hizo ziwe za mara kwa mara ili kuwapa nafasi ya kueleza changamoto zinazowakabili na baadae zifanyiwe kazi na Serikali.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news