Dawa za kulevya zilivyoacha kilio kwa Mtumishi wa Umma Shirika la Posta-3

NA GODFREY NNKO

"Nikaenda hivyo hivyo na wizi unaendelea ilipofika mwaka 2011 kwenda 2012 tukio lililonifukuzisha kazi nikiwa Mtumishi wa Shirika la Posta, nilifoji cheki na mshikaji wa CRDB, nilipata ishu ya cheki ila kwa mara ya kwanza tulifanya vizuri tukagawana hela, nyingi tu. Nikaenda kununulia unga (heroine).

"Mara ya pili nikakamatwa walishtukia na kuweka mitego kwenye mtandao nikanaswa, ikanipelekea nikasimamishwa nikiwa kazini, lakini nikawa naenda kazini ninasaini ninaondoka na mshahara ninapewa kama miezi mitatu, wenyewe wako kwenye vikao vya nidhamu na uchunguzi."... Endelea sehemu ya tatu...

Bw.Yohana Komba ambaye aliwahi kuwa mtumishi wa umma kupitia Shirika la Posta ofisi ya Tabora na kuachishwa kazi kutokana na matumizi ya dawa za kulevya yaliyomshawishi hadi kujiingiza katika masuala ya wizi anasema, baada ya kuachishwa kazi alianza kuchunguzwa.

Uchunguzi

"Usalama walikuwa wanakuja kunihoji kutoka Dar es Salaam na kuondoka, walikuwa kwenye uchunguzi na tayari zikaanza kusambaa sambaa taarifa kuwa, huyu jamaa kasimamishwa kazi anajihusishwa na madawa (dawa za kulevya). Kwa hiyo kazi zikapungua (waliokuwa wanamtumia kuwatengenezea kompyuta mpakato na programu nyinginezo) wakakosa uaminifu kwangu, hatimaye nikafukuzwa kazi mwaka 2012 inaenda 2013.

Kanuni za maadili zinasemaje?

Kwa mujibu wa Kanuni za Maadili ya Utendaji katika Utumishi wa Umma ambazo zinatungwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma kwa mujibu wa mamlaka aliyopewa katika kifungu cha 34 cha Sheria ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2002 pamoja na Kanuni ya 65 (1) ya Kanuni za Utumishi wa Umma za Mwaka 2003, Bw.Yohana Komba inaonekana kutokana na mienendo, tabia na matendo yake alivuka mipaka ya utumishi, ndiyo maana alifukuzwa kazi.

Mfano Kanuni ya 6 (4) kutoka Kanuni za Maadili ya Utendaji katika Utumishi wa Umma 2005 inaeleza wazi kuwa, "Watumishi wa umma wanapaswa kuwa waaminifu na kutumia muda wa kazi kutekeleza wajibu wao. Hawaruhusiwi kutumia muda wa kazi kwa shughuli zao binafsi au kwa mapumziko isipokuwa kama wamepewa idhini ya kufanya hivyo.

Kanuni ya 6 (7) inaeleza kuwa, "Watumishi wa umma wanapaswa kuepuka tabia ambayo inavunja heshima ya utumishi wao kwa umma hata wanapokuwa nje ya mahali pa kazi.

"Tabia inayoweeza kuvunja heshima ya utumishi wa umma ni pamoja na matumizi ya madawa (dawa) ya kulevya, ulevi, kukopa kwa kiwango ambacho kawawezi kurejesha, mwenendo mbaya wa kujihusisha na vitendo vyovyote viovu mbele ya jamii,"mwisho wa kunukuu sehemu ya maelezo ya kanuni hizo.
Bw.Yohana Komba anaendelea kueleza kuwa, "Basi mzee wangu akapewa taarifa kijana wako amesimamishwa kazi, kwa hiyo tunampa cheki yake arudi nyumbani akaendelee na mambo mengine, kweli wakaandaa cheki yangu ikawa tayari, lakini mzee wangu akawambia wasinipe anakuja kuifuata yeye mwenyewe, lakini hapo walishamwambia maneno mengi sana kuwa, mimi ni mwizi,jambazi kibaka maana niliokuwa nakaa nao walikuwa wanafanya hizo mambo na baba alikuwa ameamini kila kitu ila nilikiwa sijafikia hiyo stage".

Baba amfuata Tabora

"Basi baba yangu alikuja kunifuata kutoka Dodoma kuja Tabora, ila simu yangu ilikuwa imezima akafika ofsini,sipo wakampa cheki yangu akaenda hotelini na baadae simu ikawashwa nikapigiwa, nikaambiwa ninahitajika ofisini nikaenda nikaambiwa baba yako amefika kunichukua ila wakampigia simu akaja kunichukua tukaenda hotelini.

"Tulipofika tukakaa wee...ameshachukua room (chumba) yake na ya kwangu, baadae nikamuomba baba yangu anisaidie elfu ishirini, maana mambo yangu yalikuwa sio mazuri nilikuwa nategemea mshahara tu sina tena marupurupu na matumizi yangu yalishakuwa makubwa.

Baba apigwa 'mzinga'

"Basi aliponipa pesa yangu nikaenda kuchukua unga wangu (heroine) kama lisaa limoja nikarudi nao, nimeshavuta na mwingine nikaweka mfukoni, nikijua kesho yake ninasafiri, hivyo ninapaswa niwe na unga wa kutosha wa kuvuta maana unga ukikaa masaa kumi bila kuvuta unaweza kutokwa hata na haja kubwa kwenye gari.

"Nilipofika baba yangu, hakuamini maana aliponipa pesa yake alijua ninaweza kuwa nimetoroka nimeenda moja kwa moja, maana si alishapewa taarifa kibao kuhusu mimi,basi nilipofika nikaoga tukaingia mezani kula, akaanza kuniambia nilijua umekimbia, nikamwabia mimi siwezi kukimbia".

Safari kurudi Dodoma

"Basi kesho yake tukajiandaa, tukaanza safari mpaka nyumbani Dodoma, tukaoga na kuingia mezani kula tukaendelea kupiga stori, akaniambia mwanangu nilipofika Tabora niliambiwa mambo mengi kuhusu wewe na mpaka nilikuja nikiwa na bastola nikijua kunaweza kuwa na fujo, nilishtuka na hata nilipokupa ile hela nilijua haurudi tena, nilikuwa na wasiwasi. Itaendelea chapisho lijalo hapa DIRAMAKINI BLOG.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news