HGWT: Ni wajibu wetu kushiriki mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia

NA FRESHA KINASA

SHIRIKA la Hope for Girls and Women in Tanzania (HGWT) linalojishughulisha na mapambano ya vitendo vya ukatili wa kijinsia lenye makao makuu yake Mugumu Wilaya ya Serengeti mkoani Mara, limesema kila mwananchi anawajibu wa kushiriki mapambano ya vitendo vya ukatili wa kijinsia ili kutokomeza vitendo hivyo.
Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Kituo cha Nyumba ya Matumaini Mugumu kinachotoa hifadhi kwa wasichana waliokimbia vitendo vya ukatili wa kijinsia ikiwemo ukeketaji na ndoa za utotoni,Daniel Misoji.

Ni kituo ambacho kinamilikiwa na shirika hilo wakati akizungumza na DIRAMAKINI Blog kwa niaba ya Mkurugenzi wa shirika hilo, Rhobi Samwelly.
Misoji amesema kuwa, ili kumaliza vitendo vya ukatili wa kijinsia kila mwananchi kwa nafasi yake anapaswa kushiriki kikamilifu kupambana na vitendo hivyo ikiwemo kuwafichua mbele ya sheria watu wanaofanya vitendo hivyo bila kuwafumbia macho.

Ameongeza kuwa, pamoja na juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali pamoja na wadau mbalimbali yakiwemo mashirika, bado ushiriki wa wananchi katika kumaliza vitendo hivyo unahitajika sana kumaliza vitendo hivyo ambavyo ni kinyume cha sheria za nchi na haki za binadamu.

"Yapo matukio yanafanyika maeneo ya vijijini ili yafahamike lazima wananchi wayaripoti katika vyombo vya sheria wananchi wakikaa kimya vitendo hivyo haviwezi kuisha kwa haraka. Lazima jamii itambue ukatili ni kosa kubwa kisheria na wajue madhara ya kufanya ukatili,"amesema Misoji.

Ameongeza kuwa,shirika hilo linaendelea na utoaji wa elimu ya madhara ya vitendo vya ukatili wa kijinsia maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Serengeti ikiwemo shuleni, mikutano ya hadhara lengo ni kufikisha elimu hiyo kwa wananchi katika makundi yote na wao wawe mabalozi wema wa kuelimisha wengine katika maeneo yao juu ya madhara ya vitendo vya ukatili wa kijinsia.
Amesema, vitendo vya ukeketaji na ndoa za utotoni vinapaswa kupingwa kwa juhudi zote kwani mila hizo ni potofu na zinawanyima fursa Watoto wa kike kufikia malengo yao na pia madhara yake ni makubwa havipaswi kufumbiwa macho.

"Mtoto wa kike akikeketwa anapata kovu sehemu za siri jambo ambalo ni hatari kwa usalama wake wakati wa kujifungua linaweza kuchanika na kuleta madhara makubwa sambamba na kutokwa damu nyongi, pia ukeketaji unaathari kubwa kisaikolojia kwa binti aliyekeketwa na pia kuna hatari ya kupata magonjwa ya kuambukiza hii ni kutoka na utumiaji wa zana moja kwa watu zaidi ya mmoja wakati wa kukeketa ninaiomba jamii ipige vita ukeketaji una madhara,"amesema Misoji.

"Watoto wa kike wasomeshwe kusudi waje watoe mchango wa maendeleo, tunashuhudia viongozi katika ngazi za mikoa, wilaya, mashirika, wizara, majeshi wakihudumu vyema kwa sababu walisomeshwe na kwa sasa ni tegemeo. Niishauri jamii kuweka mkazo katika elimu kwa watoto wa kike wana nafasi kubwa ya kuleta mapinduzi chanya ya maendeleo,"amesema Misoji.
Aidha, Misoji ameishukuru na kuipongeza Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka mkazo thabiti kwa Watanzania kuachana na vitendo vya ukatili wa Kijinsia. Ambapo amesema hatua hiyo itasaidia kwa kiwango kikubwa kuongeza ufanisi katika kutokomeza vitendo hivyo hapa nchini.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news