Jaji Mfawidhi azindua Anuani za Makazi Mahakama Kuu Kanda ya Songea

NA BRIAN HAULE-Mahakama

JAJI Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. Yose Mlyambina jana tarehe 10 Juni, 2022 amezindua anuani ya makazi katika Jengo la Mahakama Kuu Songea na kuwahimiza Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama zote za Hakimu Mkazi na Wilaya kutekeleza agizo la Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Khamis Juma la kuwekaji vibao vya anuani hizo katika Mahakama zao. 
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. Yose Mlyambina (kushoto) akiwa na Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Upendo Madeha (kulia) wakati wa uzinduzi wa kibao cha anuani ya makazi katika jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea.

Akiongea katika hafla ya uzinduzi huo, Jaji Mfawidhi alisema, “Ni rai yangu kuwa tutashiriki kikamilifu kwenye utekelezaji wa anuani za makazi kwa maendeleo yetu na jamii kwa ujumla. Tukumbuke pia hili ni agizo la Jaji Mkuu wa Tanzania alilolitoa katika ziara yake ya Mahakama, Kanda ya Tanga. 

"Hivyo nami naagiza Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songea na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya Songea, Tunduru, Namtumbo, Mbinga na Nyasa kutekeleza hili kwa haraka na kuhakikisha Headed letters (vichwa vya barua) zetu ziwe na anuani za makazi,” alisema. 
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. Yose Mlyambina (picha ya juu na mbili chini) akiongea na watumishi wa Mahakama Kanda ya Songea wakati wa uzinduzi wa anuani ya makazi katika jengo la Mahakama Kuu Songea. 

Aidha, Mhe.Mlyambina aliwaeleza watumishi wa Mahakama waliohudhuria hafla hiyo kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iko katika utekelezaji wa mchakato wa anuani za makazi nchi nzima, hivyo kutokana na umuhimu wa zoezi hilo Mahakama ya Tanzania nayo ni sehemu ya taasisi ambazo zinapaswa kuwa na anuani ya makazi kwa sababu ya faida mbalimbali. 

Alizitaja faida hizo kama utambulisho wa maeneo kwa urahisi, kufikiwa kwa maeneo mengi, ikiwemo Mahakama kwa ajili ya huduma mbalimbali kwa wadau, upangaji na usimamizi wa mipango ya kutoa huduma kwa wananchi, utoaji wa huduma za dharura kwa wananchi na kukabiliana na maafa mbalimbali, kurahisisha mawasiliano baina ya taasisi, wadau na wananchi kwa ujumla, kuimarisha ulinzi na usalama na vyombo vya dola kufuatilia endapo kuna changamoto yoyote, kufahamu athari inayoweza kujitokeza endapo ataingia mgeni, kuepusha migogoro ya mipaka na majirani na upatikanaji wa hati za viwanja. 
“Tukiwa tunaelekea kwenye Mahakama Mtandao, anuani za makazi zitarahisisha malengo yetu kufikiwa kwa wakati kwani kutakuwa na urahisi wa kufikiwa, lakini pia anuani za makazi zinakwenda sambamba na upangaji na usimamizi wa mipango ya maendeleo na utoaji huduma, zikiwemo za mawasiliano kama vile usambazaji wa Mkonga wa Taifa,” alisema Jaji Mfawidhi huyo. 

Mhe. Mlyambina alitumia fursa hiyo kuwaasa watumishi wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Songea kuendelea kuchukua tahadhari ya ugonjwa wa Uviko-19. “Niwaombe watumishi wenzangu tuendelee kujitahadhari na ugonjwa wa Uviko-19 kwani kinga ni bora kuliko tiba,” alisema.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news