Mahakama FC yawatoa jasho Kahama Veterani

NA EMMANUEL OGUDA-Mahakama

TIMU ya Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga ya mpira wa miguu wanaume (Mahakama FC) imetoana jasho na timu ya Veterani ya Mjini Kahama (Kahama Veterani) na kupoteza mchezo huo kwa tabu kwa kufungwa magoli 2 -1.
Wachezaji wa Mahakama FC ya Shinyanga wakipasha misuli kabla ya kuanza kwa mchezo wa kirafiki dhidi ya Kahama Veterani ya Mjini Kahama hivi karibuni.

Mchezo huo wa kirafiki wa kisisimua ulishuhudiwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe. Athumani Matuma. Kipindi cha kwanza kilianza kwa kasi huku Mahakama FC ikisakata kabumbu kwa uhakika na kulisakama lango la wapinzani wao mara kwa mara.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Shinyanga, Mhe. Athumani Matuma akisalimiana na wachezaji wa Mahakama FC kabla ya kuanza kwa mchezo wa kirafiki dhidi ya Kahama Veteran.

Hata hivyo, katika dakika ya 25 ya kipindi hicho, Kahama Veterani wakafanikiwa kupata bao kupitia mshambuliaji wao Denis Deocles. Baada ya kupachikwa bao hilo, Mahakama FC wakacharuka na kulishambilia lango la wapinzani wao kama nyuki.

Katika dakika ya 33 Mahakama FC waliweza kusawazisha goli hilo kupitia mshambuliaji wake machachari Patrick Mluge ambaye aliweka kimyani bao safi baada ya kupokea pasi mpenyezo kutoka kwa winga, hivyo hadi dakika 45 za kipindi cha kwanza zinakamilika timu zote mbili zilikuwa zimetoshana nguvu kwa kufungana goli 1 - 1.
Kikosi cha Mahakama FC katika picha ya Pamoja.
Kikosi cha Kahama Veteran katika picha ya Pamoja.
Kocha Mkuu wa Mahakama FC Abdulmuuminu Mbaraka akiongea na wachezaji (hawapo katika picha) wakati wa mchezo wa kirafiki dhidi ya Kahama Veterani.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi ambapo timu zote mbili zilionyesha uwezo mkubwa katika kushambuliana kwa zamu. Hata hivyo, katika dakika ya 77 ya kipindi hicho, mshambuliaji wa Kahama Veterani Miraji Kasimu aliachia shuti kali kwenye lango la Mahakama FC lililomshinda golikipa Novat Mgongolwa na kuandika bao la pili.

Katika dakika ya 85, Mahakama FC wakapata nafasi adhimu baada ya mchezaji wa Kahama Veterani kucheza faulo nje ya 18, nafasi ambayo Mahakama FC wakaipoteza. Hadi dakika 90 za mchezo zinakamilika Kahama Veterani waliibuka washindi dhidi ya Mahakama FC kwa kufunga mabao 2 – 1.
Mahakama FC wakiwa uwanja wa CCM Kambarage katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Kahama Veterani ya Mjini Kahama.

Akizungumza baada ya mchezo huo, Kocha wa Mahakama FC, Abdulmuuminu Mbaraka amesema kikosi chake kinaendelea na mazoezi na kujiimarisha na ameona makosa kadhaa ambayo ameahidi kuyafanyia kazi na kikosi chake kuendelea kuwa imara na thabiti wakati wote.

Awali akifungua mchezo huo uliochezwa ndani ya dimba la CCM Kambarage katika Manispaa ya Shinyanga, Mhe. Matuma aliwapongeza wanamichezo hao kwa kuandaa mchezo wa kirafiki kwani michezo ni afya, hujenga afya ya akili na kuboresha mahusiano baina ya wanamichezo hao. Aliwataka wanamichezo hao kuendelea kufanya mazoezi ili kushiriki katika michezo mbalimbali ndani ya Kanda.
Kapteni wa Mahakama FC Benedict Mtewa akitimiza wajibu wake ndani ya dimba la CCM Kambarage Shinyanga wakati wa mchezo wa kirafiki dhidi ya Kahama Veterani.
Kocha Mkuu wa Kahama Veterani Karume Songoro.

Naye mwakilishi wa wanamichezo kutoka timu ya Kahama Veterani aliyefahamika kwa jina moja la Gwamaka, aliwashukuru viongozi wa Mahakama FC kwa kuwaalika katika mchezo huo wa kirafiki ambao pia ni wa marudiano. 

Alisema kuwa, katika mchezo huo walikuwa wamejiandaa kulipa kikasi baada ya Mahakama FC kuwazabua Kahama Veterani 1-0 katika mchezo wa kirafiki uliopigwa Mjini Kahama mapema mwezi Machi, mwaka huu.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news