Majaji vituo jumuishi Kinondoni, Temeke wahimiza huduma bora na uadilifu kazini

NA MAGRETH KINABO-Mahakama

JAJI Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania katika Kanda ya Dar es Salaam, Mhe.Jaji Amir Mruma amewataka watumishi na viongozi wa Kituo cha Utoaji wa Haki (IJC) Kinondoni kuendelea kutoa huduma bora za haki na zilizotukuka kwa wananchi ili kuweza kukidhi matarajio na kujenga imani yao juu Mahakama.
Baadhi ya watumishi wa Kituo cha Utoaji wa Haki (IJC) Kinondoni wakimsikiliza Jaji huyo.

Akizungumza hivi karibuni wakati akifungua mafunzo ya siku tano ya Huduma kwa Mteja ya awamu ya pili yanayowashirikisha watumishi na viongozi wa IJC hiyo ambayo yanafanyika katika Kituo hicho jijini Dar es Salaam, Jaji Mruma alisema upatikanaji wa haki ni imani kwa wananchi.

“Niwaombe watumishi wote kuzingatia mafunzo na maelekezo yote yatakayotolewa na tuyatafsiri kwa kila moja wetu kwa kutoa huduma kwa weledi na kwa kiwango cha hali juu ili huduma zetu ziendane na ubora wa jengo lenyewe. Hivyo kila mtu anaowajibu wa kuhakikisha haki inatendeka,” alisema na kuwasihi waendesha mashtaka na mawakili nao kuisaidia Mahakama ili iweze kutekeleza jumkumu lake kikamilifu.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma (katikati) akizungumza na baadhi ya watumishi na viongozi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji wa Haki (IJC) Kinondoni hivi karibuni wakati akifungua mafunzo ya Huduma kwa Mteja ya awamu ya pili.(Kulia) ni Mtendaji wa kituo hicho, Bw. Beatus Benedictus na (kushoto) ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Victoria Nongwa.

Aliwaambia watumishi hao kuwa ikiwa kila mmoja atatimiza wajibu wake katika kutoa huduma atakuwa amejiinua yeye mwenyewe, atainua kituo cha IJC na huduma za Mahakama za Tanzania kwa ujumla.

“Uboreshaji wa Mahakama unamlenga mwananchi ambaye ni mteja wetu na namna Mahakama inavyomhudumia. Kwa hiyo, kipaumbele cha Mahakama kinakuwa ni kutoa huduma bora zitakazofanya wananchi kuwa na imani na chombo hiki cha haki pamoja na kuwaweka karibu na Mahakama. Kwa dhamira hii, Mahakama inatutaka kubadili fikira zetu ili kuondokana na kutoa huduma kwa mazoea.

“Badala yake kupitia mafunzo haya tunakumbushwa kuwa kila mmoja wetu katika nafasi yake kuhakikisha anaunga mkono juhudi hizi za Mahakama kwa kutoa huduma bora zitakazoendana na ubora na ukisasa wa jengo na mazingira yote tunayofanyia kazi zetu.’’ alisisitiza.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Amir Mruma (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya watumishi na viongozi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji wa Haki (IJC) Kinondoni. Kushoto wa kwanza ni Mtendaji wa kituo hicho, Bw. Beatus Benedictus na wa (pili kushoto) ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Victoria Nongwa. Kulia wa pili ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Kivukoni, Kinondoni Mhe. Mhe. Franco Kiswaga (wa kwanza kulia) ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kinondoni, Mhe. Jacqueline Rugemalila.

Alifafanua kuwa huduma bora zitakwenda sambamba na matumizi ya teknolojia ya kisasa ambayo Mahakama imeipa kipaumbele cha hali ya juu. Mahakama ina mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mwasiliano(TEHAMA) ambapo matumizi yake katika kutoa huduma za kimahakama imeshika kasi.

“Hivyo Kinondoni tutaendelea na juhudi hizi ambazo tayari tunazitumia na kamwe hatutarudi nyuma. Nawahimiza watumishi wote kuhakikisha mnajitoa katika kutumia TEHAMA ili wote tuweze kuendana na kasi na tusiache mtu nyuma,’’ alisema.

Alisema teknolojia hiyo inawezesha kuchukua ushahidi popote pale mtu alipo na kupunguza gharama za mteja na kwa Mahakama kupunguza gharama za uendeshaji.

Jaji Mruma alisema kwamba, mafunzo hayo ni nafasi ya kipekee iliyowakutanisha kupata uelewa wa pamoja katika azma ya kuboresha zaidi utendaji wa kazi, hivyo ni nafasi adimu ambayo itawafanya washiriki wote wa mafunzo hayo kutoa huduma zilizo bora na kwa kiwango cha juu zaidi ili kumfanya mwananchi aweze kufurahia sio tu majengo na miundo mbinu mizuri bali pia kupata huduma bora na kwa wakati.
Alizitaja faida za mafunzo hayo kuwa ni kuboresha utendaji wa kazi, kupata maarifa mapya, kujenga mahusiano mazuri na makundi tofauti na kupata marafiki wapya na kubadilisha mtazamo wa utendaji kazi.

Mafunzo hayo ni njia ya kuondoa changamoto na kukupa mwelekeo katika kuendeleza juhudi kwa yale yaliyofanikiwa zaidi au kwa kutafuta njia mbadala za kutatua changamoto zilizojitokeza. Hivyo ni matarajio yake kuwa mafunzo hayo yataboresha uwezo wa watumishi wote.

Wakati huo huo katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Temeke, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Ilvin Mugeta amefungua mafunzo ya namna hiyo ambayo yamelenga kuwafahamisha watumishi maana ya vituo hivyo na kuwaandaa kifikra na kisaikolojia ili wawe na utayari wa kutoa huduma kama iliyokusudiwa.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Temeke, Mhe. Ilvin Mugeta (kushoto) akifungua mafunzo ya Huduma kwa Mteja kwa watumishi wa kituo hicho. Kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Mhe. John Utamwa.

Jaji Mugeta ambaye ndiye Mfawidhi wa Kituo hicho alisema kwamba uboreshaji wa utoaji huduma katika nyanja zote yanatokana na mipango ya mikakati madhubuti, uongozi imara pamoja na utayari na uthubutu wa watumishi wote.
Baadhi ya watumishi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki, Temeke, jijini Dar es Salaam wakisikiliza mada.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Mhe. John Utamwa akitoa mada kuhusu maadili na tamaduni za Mahakama ya Tanzania.
Mwezeshaji Bi. Betty Jones akitoa mada ya saikolojia.

Aliongeza kuwa kwa kuwa wapo tayari wanaweza kuthubutu, hivyo amewahimiza kubadilika kwa kutekeleza majukumu yao kiuadilifu,weledi na kuwajibika ili wananchi waweze kuwaamini.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news