UWT tuendelee kuwa mfano bora katika chaguzi, tuchague viongozi waadilifu, wenye maono-Mama Kabaka

NA FRESHA KINASA

MWENYEKITI wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi Tanzania (UWT), Gaudencia Kabaka ameitaka jumuiya hiyo kuwa mfano bora kwa kuendela kufanya chaguzi zake kwa haki na kuwachagua viongozi waadilifu na wenye maono na uwezo wa kuongoza jumuiya hiyo kwa ufanisi kuanzia ngazi za chini.
Kabaka ameyasema hayo leo Juni Mosi, 2022 katika kikao cha Baraza la UWT Mkoa wa Mara kilichofanyika katika ofisi za Chama Cha Mapinduzi zilizopo Mjini Musoma mkoani Mara ambapo pamoja na mambo mengine amesema, jumuiya hiyo ina wajibu wa kuendelea kumsemea Rais Samia Hassan kwa wananchi kutokana na kazi nzuri anazozifanya za kuliletea maendeleo Taifa la Tanzania.

Amesema kuwa, jumuiya hiyo inapaswa kuendelea kufanya chaguzi za kuwapata viongozi wake kwa haki na kwamba kila mmoja ana haki ya kugombea nafasi ndani ya UWT na pia amesema upendo na mshikamano ndani ya jumuiya hiyo unapaswa kushamiri kwa kiwango cha juu. Huku akijivunia kupungua kwa makundi ndani ya UWT hivi sasa tofauti na miaka ya nyuma.
"Naomba tusianze kuhangaika na safu ya 2025 huwezi kujua kama utakuwa hai mpaka muda huo, kitakacho kubeba ni kazi yako ya miaka mitano si kupanga safu. Pia niombe tuzidi kuheshimiana na siyo kutumia lugha mbaya za kuchafuana niwaombe makatibu muendelee vizuri katika mchakato huu wa uchaguzi ndani ya jumuiya kwa chaguzi zinazofuata,"amesena Kabaka.

"Chaguzi zisitusambaratishe, zisitutenganishe, zisitugawe tuzithamini hizi chaguzi ili tupate uwezo wa kumchagua Rais Samia Hassan 2025 tunaenda kumpigia kura sasa Rais wa Awamu ya Sita mama yule ametubeba Kama wanawake, kwanza tukumbuke alivyopokea nchi katika hali ngumu,"amesema Kabaka.
"Tunachomshukuru Mungu alikuwa makamu wa Rais Mipango yote alikuwa anaifahamu akaendeleza miradi ya kimkakati na miradi hiyo ipo kwenye hatua nzuri sana na pia katika kata mbalimbali nchini Kuna miradi mingi inatekelezeka chini ya uongozi wake makini. Niwaombe UWT mseemeni Rais kwa kazi nzuri anazofanya hawezi kuzunguka kila sehemu kusema sisi tumsemeeni,"amesema Kabaka. 

Aidha, Kabaka amesisitiza wanawake wa jumuiya hiyo, kujisajili kwa mfumo wa kielekitroniki sambamba na kushiriki kikamilifu katika zoezi la Sensa ya watu na makazi itakayofanyika mwezi Agosti, mwaka huu ili kuiwezesha Serikali kupanga mipango yake kwa ufanisi ya Maendeleo kwa Watanzania.
Kwa upande wake Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Mara, Akyoo Langael amesema kuwa, Mkoa wa Mara unaendelea na uchaguzi ndani ya chama hicho na chaguzi zinaendelea vizuri kuwapata Viongozi halisi, ambapo waliochaguliwa amesema wamepita katika mchakato na kukubalika na uchaguzi huo amesema utafanyika kwa ufanisi mwanzo hadi mwisho.

Wegesa Hassan ni Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Mara ambapo amesema Rais Samia Hassan amewaheshimisha wanawake na Watanzania kiujumla kwa uongozi bora na kuwa kinara kwa kufanya mambo mengi ya manufaa kwa Wananchi.
"Rais Samia ameendelea kuimarisha miundombinu ya barabara, sekta ya elimu, afya pamoja na kutangaza sekta ya Utalii kimataifa ambayo itapaisha uchumi wa nchi yetu. Huyu ni kiongozi wa mfano katika nchi yetu na mataifa mengine kwa umahiri wake,"amesema Wegessa.

Katika kikao hicho, (UWT) Mkoa wa Mara imempa tuzo ya uongozi bora Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania Gaudencia Kabaka kwa kutambua na kuthamini uongozi wake thabiti Katika kuiongoza jumuiya hiyo kwa mafanikio makubwa.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news