TCCIA yaanika faida lukuki za Mara International Business Expo 2022

NA FRESHA KINASA

MWENYEKITI wa Chama cha Wafanyabiahara Kilimo na Viwanda (TCCIA) Mkoa wa Mara, Boniphace Ndengo amesema kupitia maonesho ya Kimataifa ya Mara International Business Expo yanayotarajia kufanyika Mkoa wa Mara kuanzia Septemba 2 hadi 11, 2022 ambayo yatawakutanisha washiriki 50,000 hadi 100,000 yatachochea kuufanya Mkoa wa Mara uwe eneo jipya la uwekezaji kwa kuzitangaza fursa mbalimbali za kiuchumi kimataifa na kuchagiza maendeleo ya wananchi, mkoa na taifa kwa ujumla. 
Ndengo ameyasema hayo leo Julai 19, 2022 wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Uwekezaji uliopo Mjini Musoma mkoani humo kuelezea maandalizi ya maonesho hayo.

Maonesho ambayo yatafanyika katika uwanja wa Kumbukumbu ya Karume Mjini Musoma. Ambapo yanatarajia kuufungua mkoa kiuchumi kutokana na washiriki mbalimbali watakaofika na kuziona fursa zilizopo na waweze kuzitumia kwa tija kuwekeza na hivyo kuzalisha ajira na fursa mbalimbali ambazo zitaleta mchango mkubwa wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii. 

"TCCIA Mkoa wa Mara inakusudia kuendelea kushirikiana na wafanyabiashara mbalimbali duniani ili kuwaambia uzuri wa mkoa na kwamba wakiwekeza watapata tija kubwa kiuchumi na kuwanufaisha pia wana Mara kiuchumi kupitia sekta muhimu za uzalishaji za viwanda, biashara, kilimo bora na kutumia uwepo wa Ziwa Victoria na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kuchochea uchumi wa mkoa na taifa letu," amesema Ndengo. 

"Maonesho haya yatawakutanisha pia wafanyabiashara wengi kutoka mataifa mbalimbali na yataleta muingiliano wa watu wakiwemo wajasiriamali wadogo, makampuni, sekta za umma na mashirika,, wafanyabiashara wakubwa tunatarajia baada ya maonesho kutakuwa na makongamano na majukwaa mbalimbali yatafanyika kuja kuonesha jinsi gani mkoa sasa unaendelea. Sambamba na kupunguza migogoro Kati ya wawekezaji na Wananchi ili kujenga mahusiano bora na habari kubwa iwe ukuzaji wa biashara na Viwanda katika Mkoa wetu,"amesema Ndengo. 

Aidha amesema, katika maonesho hayo chemba mbalimbali za wafanyabiashara zimealikwa kutoka Uganda, Kenya, Kongo, Burundi na zimesema zitaleta washiriki. 
"Na pia Balozi mbalimbali tumealika na Zimbabwe imethibitisha kushiriki na Balozi zingine mbalimbali zikiwemo Marekani, China, India, Canada, na pia maonesho hayo yatashirikisha wadau muhimu na pia mategemeo ni kuzalisha ajira kwa vijana waipende sekta binafsi badala tu ya kutaka ajira Serikalini na kuacha fursa zinazowazunguka bila kuzifanyia kazi,"amesema. 
Mbunge wa Jimbo la Musoma Mjini, Mheshimiwa Vedastus Mathayo amesema kuwa, kila mwananchi wa Mkoa wa Mara maonesho hayo yanamhusu, hivyo analo jukumu la kuhakikisha anafanya uhamasishaji ili watu wengi waweze kujitokeza kushiriki kuonesha bidhaa zao na kuona fursa mbalimbali zitakazooneshwa katika maonesho hayo. 

Awali Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Mara,Dkt.Noel Crispine amesema, maonesho hayo pia yatawezesha kuwatangaza wafanyabiashara wa Mkoa wa Mara na wajasiramali pamoja na bidhaa zao sambamba na kutangaza vivutio mbalimbali na fursa za kiuchumi zilizopo mkoani humo kwa wafanyabiashara na makampuni ya kigeni yatakayoshiriki katika maonesho hayo na kujenga ushirikiano mzuri wa kibiashara miongoni mwao.

Ameongeza kuwa, Mkoa wa Mara umeandaa mwongozo unaoainisha fursa zilizopo ikiwemo sekta ya utalii, kilimo, viwanda na kwamba mkoa umebarikiwa kuwa na fursa ya Hifadhi ya Serengeti na Ziwa Victoria. Hivyo kazi ya serikali ni kutafsiri fursa hizo ili ziwaletee maendeleo wananchi na kwamba, sekta binafsi ni muhimu ikashirikishwa kwa upana kuchagiza maendeleo ya kiuchumi na kijamii mkoani humo. 
Amesema, kupitia maonesho hayo mkoa unaweza kuinukaa na kufahamika zaidi na hivyo kuwavuta wawekezaji toka sehemu mbalimbali za Dunia waje walete mageuzi chanya ya kiuchumi ndani ya Mkoa wa Mara na kuzitumia fursa zilizopo mkoani humo kwa tija. 

Aidha, Dkt.Noel amewataka wananchi, wajasiriamali,wafanyabiashara wa Mkoa wa Mara kujitokeza kwa wingi katika maonesho hayo ambayo amesema yatakuwa na chachu kubwa ya kuleta mageuzi na maendeleo thabiti ndani ya Mkoa wa Mara.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news