Ushauri wa AG Feleshi kuhusu bodi huru ya wanahabari unavyotoa mwanga

NA MWANDISHI WETU

MWANASHERIA Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi anaamini kwamba, uundwaji wa Bodi ya Ithibati ya Wanahabari iliyo huru, kwa kiwango kikubwa kunaweza kurejesha tabasamu kwa tasnia ya habari na wamiliki wa vyombo hivyo.

Anaamini kwamba, Bodi ya Ithibati ya Wanahabari iliyo huru, inaweza kusimamia tasnia ya habari nchini na kuleta mabadiliko makubwa katika sekta hiyo.

Mei 13, 2021 Innocent Bashungwa, alipokuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo (kabla ya tasnia ya Habari kuhamishiwa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari) alisema, Serikali inaendelea na taratibu za kuanzisha Bodi ya Ithibati itayokuwa na jukumu la kutoa ithibati na vitambulisho kwa wanahabari wenye sifa.

Bashungwa alisema hayo wakati akiwasilisha makadiro ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2021/2022.

Alisema, Sheria ya Huduma za Habari ya mwaka 2016, inaelekeza kuanzishwa kwa Bodi ya Ithibati, Baraza Huru la Habari pamoja na mfuko wa mafunzo kwa wanahabari. 
“Kwa sasa wizara inaendelea na taratibu za kuanzisha bodi hii,” na kuongeza “Baraza Huru la Habari litaundwa baada ya Bodi ya Ithibati kuanza kazi.” alisema.

Tofauti na mtazamo wa Serikali, Jaji Feleshi alipokutana na wadau wa habari ofisini kwake bungeni jijini Dodoma, tarehe 13 Juni 2022 alisema, tasnia ya habari inapaswa kuwa na bodi yake inayotokana na wanahabari wenyewe ili kusimamia maadili na miiko ya wanahabari.

Namnukuu, “ni vizuri tasnia ya habari ikiwa na bodi yake itakayotumika kuhakikisha inasimamia maadili ya wanahabari...naona muwe na 'regulator', bodi yenu moja, ili mmoja wenu akienda kinyume na maadili (ya uandishi wa habari), mnamshughulikia nyinyi wenyewe.”

Ushauri wa Jaji Feleshi ulibebwa na shauku ya mwanasheria huyo kutaka kuona bodi ya wanahabari ikifanya kazi ya kusimamia wanahabari kwa uhuru na bila kuingiliwa na yeyote nje ya wanahabari.

Na hivi ndivyo ilivyo katika kada zingine nchini ikiwemo Bodi ya Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Bodi ya Uhasimu na zingine.

Ushauru wa Jaji Feleshi ndio hasa tamanio la wadau wa habari nchini, ambapo moja ya mambo yanayotia hofu ni pendekezo la muundo wa bodi ya wanahabari isioendana na ridhaa ama matakwa ya wanahabari.

Bodi ya Wanahabari ili iweze kufanya kazi yake, inapaswa kuundwa na kusimamiwa na wanahabari wenyewe.

Ikiwa kada zingine nchini zimeunda bodi zao zinazotokana na wanataaluma na wa kada hizo, kwa nini isiwezekani tasnia ya habari ikaunda Bodi ya Habari inayotokana na wanataaluma pekee wa tasnia hiyo?.

Ni kwa muda sasa tasnia ya habari imekuwa ikivuja jasho kutokana na kuelemewa na sheria kandamizi, uundwaji wa sheria hizo kwa kiwango kikubwa umekuwa ukilenga kumshambulia mwanahabari na taaluma hiyo.

Utitiri wa vyombo vingi vilivyoelekezwa kusimamia tasnia ya habari kwa mujibu wa Sheria ya Huduma ya Vyombo vya Habari 2016, unaongeza mashaka kuhusu lengo la kutungwa kwa sheria hiyo. 

Katika sheria hiyo Sehemu ya III na vifungu vyake 11, 12, 13, 14, 15, 16,17,18, 19, 20,21,22 na 23, pia Sehemu ya IV na vifungu vyake vyake 24, 25, 26, 27, 28, 29, 30, 31, 32, 33 &34 ambavyo vinazungumzia uundwaji wa Bodi ya Ithibato na Baraza Huru la Habari.

Sehemu hizi za sheria zina vifungu ambavyo vinatoa mamlaka kwa vyombo viwili ambavyo majukumu yake yangeweza kutekelezwa na chombo kimoja. Kuwa na chombo kimoja kwa kiwango kikubwa, kunaweza kupunguza gharama za uendeshaji.

Uundwaji wa chombo kimoja cha Bodi ya Ithibati kinachotokana na wanahabari wenyewe, kinaweza kutekeleza majukumu yaliyomo katika vifungu vya sehemu ya tatu na ya nne ya sheria iliyopo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news