Meli ya Kimarekani ya Wanamaji ya USS Hershel “Woody” Williams yawasili Tanzania

NA DIRAMAKINI

MELI ya Kimarekani ya Wanamaji iitwayo USS Hershel “Woody” Williams imewasili katika ziara ya bandari ya Dar es Salaam, Agosti 13, 2022.
Ziara hii ya siku tatu itatoa fursa ya kukutana na viongozi wa jeshi la Tanzania na viongozi wa serikali, ikiwemo pia kutembelea meli na maonyesho ya uwezo, pamoja na shughuli inayohusiana na wanawake, amani na ulinzi. Aidha, ziara hii itatoa fursa kwa wafanamaji hao kujumuika na jamii.

“Tanzania ni mshirika muhimu wa Marekani katika kukuza amani na utulivu wa kikanda Afrika Mashariki nzima,” alisema Kept. Chad Graham, Afisa Mkuu wa Hershel “Woody” Williams. “Tunaishukuru sana Tanzania kwa kuturuhusu kufanya ziara hii ya bandari wakati tukiendelea na shughuli katika pwani nyingine.”

Hii ni ziara ya kwanza ya meli ya Kimarekani katika bandari baada ya zaidi ya muongo mmoja. Balozi wa Marekani nchini Tanzania Donald Wright alisema ziara ya USS Hershel “Woody” Williams inaonyesha uimara wa ushirikiano wa kiulinzi kati ya Marekani na Tanzania.
“Ushirikiano wa kiulinzi ni nguzo ya mahusiano ya Marekani na Tanzania. Tanzania inaongoza katika kukuza amani na ulinzi kikanda, na tunashukuru kwamba majeshi yetu yana ushirikiano wa karibu wenye tija,” Wright alisema.

Tanzania ni mshirika muhimu katika kudumisha amani na utulivu Magharibi mwa Bahari ya Hindi. Aidha, Tanzania ilishiriki katika zoezi la Cutlass Express, Februari 2022, zoezi la wanamaji linaloshirikisha mataifa mbalimbali lililofanyika Afrika Mashariki na Magharibi mwa Bahari ya Hindi. Aina hii ya mazoezi huimarisha ushirikiano miongoni mwa nchi na kufanya kazi kwa karibu zaidi katika changamoto za pamoja za kimataifa.
USS Hershel “Woody” Williams ni meli ya kwanza ya kivita yenye shughuli za kudumu katika Jeshi la Marekani Kamandi ya Afrika.

Marekani ina maslahi ya pamoja na mataifa ya Afrika katika kuhakikisha ulinzi, usalama na uhuru wa safari katika maji yanayolizunguka bara, kwa sababu maji haya ni muhimu kwa ustawi wa Afrika na kuyafikia masoko ya dunia.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news