Mapato ya utalii nchini yapaa huku watalii wakiongezeka, Waziri Mkuu asema Royal Tour imejibu

NA MWANDISHI WETU

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema takwimu za mwaka 2021 zinaonesha kuwa watalii wanaokuja nchini Tanzania wameongezeka kwa asilimia 48.6 kutoka watalii 620,867 mwaka 2020 na kufikia watalii 922,692 mwaka 2021.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza wakati alipomuwakilisha Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwenye ufunguzi wa Mkutano wa 65 wa Shirika Utalii Duniani - Kamisheni ya Afrika uliofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Gran Melia jijini Arusha, Oktoba 5, 2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Mheshimiwa Majaliwa amesema mbali na kuongezeka kwa idadi ya watalii nchini, pia mapato yatokanayo na utalii yameongezeka kwa asilimia 81.8 kutoka Dola za Marekani milioni 714.59 mwaka 2020 na kufikia Dola za Marekani bilioni 1.3 mwaka 2021.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo Jumatano, Oktoba 5, 2022 alipomuwakilisha Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwenye ufunguzi wa Mkutano wa 65 wa Shirika la Utalii Duniani - Kamisheni ya Afrika unaofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Gran Melia Jijini Arusha.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Naibu Waziri Mkuu wa Mauritius, Louis Steven Obeegados (kushoto) kabla ya kufungua Mkutano wa 65 wa Shirika la Utalii Duniani – Kamisheni ya Afrika kwa niaba ya Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan uliofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Gran Melia jijini Arusha, Oktoba 5, 2022. Wa pili kushoto ni Katibu Mkuu wa Shirika la Utalii Duniani, Zurab Pololikashvili. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

“Pia takwimu za mwaka 2022 zinaonesha kuwa Sekta ya Utalii inazidi kuimarika zaidi hususan baada ya uzinduzi wa Programu Maalumu iliyotekelezwa na Mheshimiwa Rais Samia ya The Roya Tour iliyozinduliwa rasmi Aprili 2022 katika soko letu la utalii la kimkakati nchini Marekani.”

Amesema kuwa mafanikio hayo ni matokeo ya mwongozo mzuri uliotolewa na Shirika la Utalii Duniani kwa nchi wanachama ikiwemo Tanzania katika kukabiliana na athari za UVIKO - 19. 

“Kwa msingi huo, ninatumia fursa hii kulishukuru Shirika la Utalii Duniani hususan, kwako Mheshimiwa Zurab Pololikashvili, Katibu Mkuu wa Shirika la Utalii Duniani kwa kuiongoza vema sekta ya utalii katika kipindi chote cha janga hilo.”
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Naibu Waziri Mkuu wa Mauritius, Louis Steven Obeegados kabla ya kufungua Mkutano wa 65 wa Shirika la Utalii Duniani – Kamisheni ya Afrika kwa niaba ya Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan uliofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Gran Melia jijini Arusha, Oktoba 5, 2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Hata hivyo, Waziri Mkuu amesema lengo la Serikali ni kuendelea kuongeza idadi ya watalii wanaoingia nchini hadi kufikia watalii milioni tano na mapato ya Dola za Marekani bilioni sita ifikapo mwaka 2025.”Utajiri wa vivutio vya utalii tulivyonavyo umeifanya sekta ya utalii kuwa muhimili muhimu wa uchumi wa nchi yetu.”

Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa ametumia fursa hiyo kutoa rai kwa mashirika na taasisi za kimataifa kuendelea kuiamini Tanzania na kuichagua kama sehemu sahihi ya kufanyia shughuli mbalimbali ikiwemo mikutano adhimu kama hii.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiongozana na Naibu Waziri Mkuu wa Mauritius kwenda kwenye ukumbi wa mikutano wa Gran Melia jijini Arusha kufungua Mkutano wa 65 wa Shirika Utalii Duniani – Kamisheni ya Afrika kwa naiba ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan , Oktoba 5, 2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Naye, Katibu Mkuu wa Shirika la Utalii Duniani, Zurab Pololikashvili amesema kuwa baada ya mlipuko wa janga la UVIKO 19 nchi nyingi duniani ziliathirika kwa kiasi kikubwa katika sekta ya utalii, hivyo watahakikisha wanaendelea kuweka mikakati ya kurejesha sekta hiyo katika hali yake ya kawaida.

“Wiki iliyopita tulisherehekea siku ya utalii duniani iliyokuwa na kaulimbiu ya Rethinking Tourism, ambayo tunaamini itasaidia kuirejesha sekta hiyo katika hali yake ya kawaida na kuendelea kusaidia kutoa mchango katika ukuaji wa uchumi na kuongeza idadi ya ajira.”
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimkabidhi zawadi ya picha ya Mlima Kilimanjaro Katibu Mkuu wa Shirika la Utalii Duniani, Zurab Pololikashvili baada ya kufungua Mkutano wa 65 wa Shirika la Utalii Duniani – Kamisheni ya Afrika kwa niaba ya Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan uliofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Gran Melia jijini Arusha, Oktoba 5, 2022. Kulia ni Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Dkt. Pindi Chana. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Amesema kuwa Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo zina vivutio bora vya kutembelea kwa ajili ya utalii na watu wengi duniani wameitambua kupitia filamu maarufu ya The Royal Tour. “Ninafurahi sana kuwa miongoni mwa watu walioshuhudia filamu hiyo ambayo imeniwezesha kuona tamaduni na vivutio vilivyopo katika ardhi hii ya Uhuru na Umoja.”

Awali, Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Dkt. Pindi Chana alisema kuchaguliwa kwa Tanzania kuwa mwenyeji wa mkutano huo ni matokeo ya ushirikiano mzuri kati ya nchi yetu pamoja na jumuiya ya Kimataifa katika masuala mbalimbali yakiwemo ya utalii. Mkutano huo umehudhuriwa na washiriki kutoka nchi 33 wanachama wa Shirika la Utalii Duniani - Kamisheni ya Afrika.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news