Mawaziri wa Kisekta watembelea maeneo ya hifadhi na chanzo cha maji yaliyovamiwa Katavi

NA MUNIR SHEMWETA-WANMM

KAMATI ya Mawaziri wa Wizara za Kisekta imetembelea maeneo ya hifadhi na chanzo cha maji katika Mkoa wa Katavi kujionea hali ya uvamizi wa maeneo hayo na kuelekeza wananchi waliovamia maeneo hayo kutofanya maendelezo mpaka hapo timu ya wataalamu itakapokamilisha kazi yake kuhusiana na mgogoro wa matumizi ya ardhi kwenye maeneo hayo.
Munekano wa eneo la chanzo cha maji cha Milala katika Manispaa ya Mpanda mkoani Katavi.

Kamati hiyo inayohusisha wizara nane za kisekta Oktoba 12, 2022 ilitembelea eneo la hifadhi la mito miwili lilipo Kitongoji cha Kasekese wilayani Tanganyika pamoja na chanzo cha maji cha Milala kilichopo Kata ya Misunkumilo Manispaa ya Mpanda mkoani Katavi.

Kiongozi wa Kamati ya Mawaziri wa Kisekta katika ziara hiyo, Mhe.Mashimba Ndaki aliwaeleza wananchi wa Kisekese kuwa, uamuzi wa mwisho kama eneo hilo liendelee kuwa hiadhi au maeneo ya kuishi watu itajulikana baada ya kupata majibu kutoka kwa wataalamu.
Kiongozi wa Kamati ya Mawaziri wa Wizara za Kisekta, Mashimba Ndaki (Kulia) akizungumza na Naibu Waziri Maliasili na Utalii, Mary Masanja wakati wakitoka kutembelea eneo la hifadhi la Kasekese wilayani Tanganyika Mkoa wa Katavi Oktoba 12, 2022.

‘’Ndugu wananchi naomba mnielwe eneo hili mnalolikalia halijaeleweka kama ni makazi yenu na vizuri tuelewe ingawa ukweli wenyewe mgumu, lakini ni vizuri kuelewa kwa sababu lina sura mbili ni eneo la hifadhi au kupita wanyama, lakini ninyi mpo mmekaa,’’amesema Ndaki.

Amewataka wananchi hao kuwa wavumilivu wakati wataalamu wanafanyia kazi suala hilo na kamati yake ikishapa majibu kuhusiana na suala hilo basi uamuzi kamili wataelezwa kati ya mambo mawili ambayo ni ama eneo hilo ni hifadhi au eneo la kupita wanyama.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Ridhiwani Kikwete akisisitiza jambo kwenye eneo la chanzo cha Maji cha Milala katika Manispaa ya Mpanda Mkoa wa Katavi wakati Kamati ya Mawaziri wa Wizara za Kisekta ilipotembelea eneo hilo Oktoba 12, 2022.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Ridhiwani Kikwete aliwaeleza wananchi wa Kasekese katika mkutano wa hadhara kuwa, kwa mujibu wa sheria za ugawaji ardhi hakuna mahali popote panaposema kuwa kiongozi anaweza kugawa ardhi kwa wananchi.
Baadhi ya wananchi wa Kasekese wilayani Tanganyika Mkoa wa Katavi wakifuatilia maelezo ya Kamati ya Mawaziri wa Wizara za Kisekta ilipotembelea eneo hilo Oktoba 12, 2022.

‘’Sheria hizi zote mbili nilizozitaja hakuna hata sheria moja iliyompa mamlaka mkuu wa wilaya au mkuu wa mkoa kugawa ardhi na ndiyo maana nimestuka sana niliposikia kuwa kuna mkuu wa wilaya amewachukua watu na kwenda kuwagawia ardhi, huyo mkuu wa wilaya amewaingiza chaka,"amesema Ridhiwani.
Mawaziri wa Wizara za Kisekta wakipata maelezo ya uvamizi wa eneo la hifadhi la mito miwili eneo la Kasekese kwa Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika mkoa wa Katavi, Onesmo Busweru (kushoto) wakati Kamati ya Mawaziri hao ilipotembelea eneo hilo kujionea hali halisi Oktoba 12, 2022. 

Akigeukia suala la chanzo cha maji cha Milala kilichopo Manispaa ya Mpanda, Waziri Ndaki aliwaambia wananchi wanaoishi eneo hilo kuwa, taarifa za awali zinaonesha kuwa wananchi hao wamevamia chanzo hicho na wanatakiwa kuondoka. 
 
Hata hivyo, alibainisha kuwa, uamuzi wa mwisho wa aidha kubaki ama kuondoka eneo hilo utaamuliwa pale Kamati yake itakapopata ushauri kutoka serikali ya mkoa wa Rukwa.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Ridhiwani Kikwete akizungumza katika mkutano wa hadhara kwenye eneo la Kasekese mkoani Katavi Oktoba 12, 2022 (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI).

Kamati ya Mawaziri nane wa Wizara za Kisekta iliyoanza kazi kwenye mkoa wa Rukwa imemaliza ziara yake mkoani Katavi na inaendelea na ziara hiyo katika mkoa wa Kigoma na baadaye Kagera.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news