Mhe.Othman ataka uelewa wa diplomasia uibue fursa za maendeleo

NA DIRAMAKINI

MAKAMU wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Mheshimiwa Othman Masoud Othman, amesema diplomasia ya nje inahitaji kutumika vyema ili kujenga uelewa, kwaajili ya kufungua fursa zaidi za maendeleo ya Nchi na Taifa kwa ujumla.
Mheshimiwa Othman ameyasema hayo leo, akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dokta Stergomena Tax, aliyefika Ofisini kwake Migombani Jijini Zanzibar, kwa lengo la kujitambulisha na kubadilishana mawazo juu ya mambo mbali mbali ya kazi na maendeleo.

Amesema kuwa diplomasia ni njia muhimu na inayoweza kutumika kuibua fursa zinanazopatikana katika Jamii ya Kimataifa na Nchi za Kigeni, pindipo itatumika vyema katika kujenga uelewa kwa watu, taasisi na hata Serikali, ili kufanikisha njia mbali mbali za kujiletea maendeleo, bali kwa Tanzania na hata Mataifa mengine Barani Afrika, huenda hawajaitumia vyema nafasi hiyo.
Mheshimiwa Othman ameeleza kuwa kukosekana kwa uelewa huo kunapelekea ukosefu wa ufuatiliaji wa matukio muhimu yanayojiri ulimwenguni, ambayo kimantiki ndiyo ambayo yangeliweza kupelekea upatikanaji wa fursa za maendeleo kupitia taasisi mbali mbali za Kikanda na Kimataifa.

Ametolea mfano fursa zinazopatikana kupitia Jumuiya ya Kimataifa ya Haki Miliki za Kitaalamu (WIPO) ambayo yeye amewahi kuitumikia hapo kabla, akiwakilisha Mataifa ya Afrika.
Hivyo ametoa wito kwa Wanadiplomasia kuitumia vyema fursa waliyonayo katika Taasisi na Mataifa ya Kigeni, kujenga uelewa zaidi, ili kuipatia nafasi Tanzania katika kuelewa matukio muhimu yanayojiri kila siku duniani, vivutio, na namna ambavyo ulimwengu unakwenda.

Naye Waziri Tax, amesema kuwa yupo tayari kwaajili ya kazi ya kuitumikia Nchi katika kujenga uelewa kupitia diplomasia, sambamba na kuhakikisha ushirikishwaji wa Zanzibar juu ya Mambo ya Muungano, sambamba na fursa mbali mbali, zikiwemo za Maazimio yanayopitishwa mbele ya Jamii na Jumuiya za Kimataifa.

Waziri huyo ambaye ameteuliwa kushika wadhifa huo kupitia hatua ya hivi karibuni ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kulifanyia mabadiliko madogo Baraza lake la Mawaziri, ameahidi kutekeleza na kuyafanyia-kazi maagizo na miongozo yote, katika kuhakikisha Taifa linafaidika kupitia diplomasia ya nje.
Katika Ujumbe wake, Waziri Tax ameambatana na Maafisa wake mbali mbali, akiwemo Mkurugenzi wa Idara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa Zanzibar, Bi Maryam Haji Mrisho.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news