ROMBO ITATUMIA SOKO LA KIMATAIFA KUUZA NDIZI ILI KUONGEZA KIPATO CHA WAKULIMA-PROF.MKENDA

NA MATHIAS CANAL-WEST

NDIZI ni zao kubwa la biashara na chakula hivyo likitumika vizuri litabadili uchumi wa wakulima na nchi kwa ujumla wake.

Katika kuimarisha Sekta ya Kilimo hususani zao la ndizi imeelezwa kuwa kuna umuhimu wa kutumia soko la Kimataifa kuuza ndizi ili kuongeza kipato cha wakulima.
Mbunge wa Jimbo la Rombo ambaye pia ni Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe.Prof.Adolf Mkenda amesema hayo Oktoba 3,2022 katika Kata ya Masera wilayani Rombo Mkoa wa Kilimanjaro wakati akizindua mafunzo ya siku saba ya uzalishaji wa zao la ndizi na maadhimisho ya wiki ya huduma kwa wateja yanayoongozwa na kauli mbiu isemayo "Ndizi kwa Afya bora na Kipato Zaidi".
Prof.Mkenda amesema kuwa,hapa Tanzania ndizi ni zao la kupika na matunda hivyo kama likizalishwa na kutumika vizuri litabadili uchumi wa nchi.

Waziri Mkenda amewema kuwa kitafanyika kikao maalumu "Roundtable" kwa wadau wa ndizi Wilayani Rombo ili kujadili mikakati ya kukuza kilimo cha kisasa cha ndizi.

Ameongeza kuwa, kupitia zao hilo bado hakujapatikana mapato ya kutosha kutokana na kutokuwepo soko la uhakika.
"Ni lazima tuangalie ndizi kama zao la biashara ambalo litatupa chakula cha uhakika, Tulifanya mkutano wa zao la ndizi Moshi na tulipanga kufanya mkutano wa kitaifa wa mkakati wa kukuza zao hilo nchi nzima, lakini ndizi bado ni uti wa mgongo wa uchumi wa wilaya ya Rombo,” amesema.

Amesema, zao la ndizi ni muhimu kwa sababu linatoa uhakika wa chakula licha ya kuwa kahawa ni muhimu lakini kama haina soko huwezi kuila kama ilivyo ndizi.
“Usipopata soko la ndizi maana yake huwezi kuwa na chakula nyumbani, hivyo kuwataka watu kutambua kuwa zao hilo ni kubwa la kibiashara,"amesema.

Ametoa mfano kuwa nchi ya Amerika Kusini ya Ecuador inauza ndizi kwa wingi na Taifa hilo linapata zaidi ya Dola za Marekani Bilioni mbili kwa mwaka ambapo inakuwa zaidi ya fedha ambazo Tanzania inapata kwa kuuza kahawa nje ya nchi.
Amesisitiza kuwa, kama ndizi zitalimwa kwa wingi na tija kutakuwa na uhakika wa chakula nchini, na zitasaidia maeneo yenye ukame na zitauzwa ndani na nje ya nchi.

Katika hatua nyingine ameipongeza Taasisi inayojishughulisha na Kilimo cha maua, matunda na mbogamboga (TAHA) kwa kudhamini mafunzo hayo ambayo yatafanyika kwa siku saba kwa lengo la kuwaongezea uelewa na uwezo wakulima kuzalisha kwa wingi na kwa tija.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news