Makunga:Naona mwanga katika mabadiliko ya Sheria ya Habari

NA DIRAMAKINI

MWENYEKITI mstaafu wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Theophil Makunga amesema kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan imeonesha nia njema kuipa hadhi tasnia ya habari nchini.

Ameyasema hayo leo Novemba 10, 2022 jijini Dar es Salaam wakati akiendelea na uchechemuzi juu ya mchakato unaoendelea wa mapendekezo ya Sheria ya Habari nchini.

Wadau wa Haki ya Kupata Habari nchini (CoRI) likiwemo Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), wameendelea kufanya uchechemuzi kwa nyakati tofauti kwa lengo la kuongeza ufahamu kuhusu mapendekezo ya mabadiliko ya sheria ya habari.

Sheria ya Huduma ya Habari ya mwaka 2016,Sheria ya Mawasiliano ya Elektroniki na Posta (EPOCA) ya 2010 ambayo inasimamia radio, TV na Mitandao ya Kijamii, Sheria ya Haki ya Kupata Habari ya mwaka 2016 na Sheria ya Makosa ya Mtandao ya 2015 zikiwemo kanuni za maudhui mtandaoni za mwaka 2018 ziliyogawanywa katika vipengele mbalimbali, ni miongoni mwa maeneo ya vipaumbele vya wadau hao ambao wanataka maboresho ili kuongeza ufanisi katika tasnia hiyo.

"Naona kuna mwanga, kwenye jambo hili,tayari Serikali imekwishaonesha nia ya kuzungumza na vyombo vya habari ili kuviondoa au kuvirekebisha vipengele na vifungu ambavyo vinabana vyombo vya habari, hiyo nia ya Serikali ipo, na kama ipo kuna matumaini makubwa.

"Wanaweza (Serikali) kukubaliana na sisi ili tubadilishe, tuondoe vile vifungu ambavyo tunafikiria vinatubana, vile vile kuvirekebisha ili kazi ya uandishi wa habari iwe rahisi.Mimi naona huko mbele ya safari Serikali iko makini inahitaji kubadilisha baadhi ya vifungu vile ambavyo vinatubana,"amefafanua Makunga.

Mwenyekiti huyo mstaafu wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Theophil Makunga anasema kuwa, licha ya changamoto za hapa na pale pia sheria imekasimisha mamlaka makubwa kwa mtu mmoja.

"Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo kwa mujibu wa Sheria ya Huduma ya Habari ya mwaka 2016 imempa mamlaka makubwa sana kufanya kazi dhdi ya vyombo vya habari na ukiangalia hiyo sheria kifungu cha 50, kifungu kidogo cha ( i ) inampa mamlaka yeye kufungia, kufanya usajili wa magazeti.

"Kwa sababu ile sheria nyingine kuhusu radio, televisheni imeenda TCRA (Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania). Lakini kwenye magazeti Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo amepewa hayo mamlaka, sisi tunasema amepewa mamlaka mengi sana kwa mfano kuhusu usajili kila mwaka unatakiwa ulipie usajili, sasa kulipia kuna leseni nyingine mfano leseni ya biashara ukiipata sasa kwenye chombo cha habari ukitaka kuanzisha gazeti lako lazima usajiliwe, sasa tunaona likishasajiliwa liachiwe ili mradi linafanya kazi kwa mujibu wa sheria.

"Lakini sasa Mkurugenzi amepewa yale mamlaka ya kusajili, kufungia vyombo vya habari kwa wakati wote yeye anapofikiria vinakwenda kinyume, hapo tunaona ni kuminya uhuru wa vyombo vya habari, waandishi wa habari watakuwa wameminywa kufanya kazi kwa uhuru, sababu ile sheria inawanyima haki kufanya kazi kwa uhuru wao," amesema Makunga.

Amefafanua kuwa, "Tupo kwenye jamii ambayo siku hizi maoni yako wewe sio lazima yafanane na maoni au mtazamo wako. Kwa hiyo hata vyombo vya habari hivi hivi vimekuwa na maoni tofauti tofauti, lakini je ule mtazamo unaenda kinyume na kanuni na utaratibu wa kufanya kazi ya uandishi wa habari au sheria za nchi?.

"Sasa kama sheria za nchi zinakaa na kuongoza shughuli za uandishi wa habari, isimpe mamlaka mtu mmoja kufanya hiyo shughuli bali iipe taasisi kama kuna kosa linahusu mambo ya mahakama basi mahakama ndio iamue isije ikawa Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo yeye ndiye kila kitu anachunguza, anapeleka mashitaka na kama shahidi na yeye yule yule anatoa hukumu.

"Hapo kunakuwa zile kanuni za utata mtu mmoja tu anafanya hivyo vitu vyote kwa hiyo kunakuwa hakuna uendeshaji wa shughuli. Yeye anaweza akakosea sasa akikosea kuna kifungu kinaruhusu kwenda kumshitaki? Ni hakuna analindwa sana na hiyo sheria.

"Tukasema apunguziwe mamlaka ambayo anapewa na hiyo sheria ya huduma za vyombo vya habari ya mwaka 2016 mambo mengi sana yapelekwe kwenye mahakama kama kuna haja ya kufanya hivyo,"amefafanua Makunga.

Kuhusu jinsi ambavyo vyombo vya habari vya Tanzania vinavyojiendesha, Makunga amefafanua kuwa, "Ukiangalia uendeshwaji wa vyombo vya habari vya Tanzania asilimia zaidi ya 50 ya matangazo yanayotolewa kwenye vyombo vya habari yanatoka serikalini, kwa hiyo uendeshwaji wa vyombo hivi vya habari unategemea sana matangazo toka serikalini, sasa unapompa mamlaka Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo achague vyombo gani serikali itangaze unaminya vyombo vingine kusavivors na kujiendesha.

"Idara za Serikali ziwe huru kutangaza kwenye vyombo vya habari bila kupitia mtu mmoja. Halafu inapita kwa mtu mmoja kwa mfano kama kuna gazeti ambalo ni critical kwa serikali halafu halipewi matangazo na kama halipewi matangazo uendeshwaji wa kile chombo utakuwa mgumu sana ni kama vile kuliua kwa kutolipa matangazo.

"Kifungu cha 50 hata huko nyuma kwenye Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976, kosa la defamation unapelekwa mahakamani ulipe fidia. Sasa kulifanya jinai ni kama kitisho kwa waandishi wa habari kutokuwapa nafasi kufanya kazi yao vizuri kwa sababu wao wana misingi yao ya kufanya kazi ambayo wanafundishwa kwenye vyuo.

"Kwa nini Serikali iwe na mashaka kuhusu utendaji kazi mpaka uitungie sheria kosa linalofanywa na chombo cha hanari liwe jinai? Sababu wenyewe kupitia taaluma yao wana namna ya kufanya kazi,hiki kiwe hivi na hiki kisiwe hivi, kwa hiyo mashaka ya serikali mimi siyaoni kwamba wanahamisha defamation kuwa jinai.

"Kama wadau wa Vyombo vya habari hiyo sheria ifutwe kabisa badala yake irudi nyuma kama ni defamation iwe hivyo,"amesema Makunga.

Hivi karibuni,Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Damas Ndumbaro alipokutana na uongozi wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) na wadau wa Haki ya Kupata Habari (CoRI) jijini Arusha alisisitiza, changamoto za kisheria zinazoikabili taaluma hiyo kwa sasa,wakati mzuri wa kuzifanyia kazi ni huu.

“Rais tuliye naye sasa, Mheshimiwa Samia (Suluhu Hassan) ameonesha moyo na nia kubwa ya kutetea na kutoa haki za vyombo vya habari na waandishi wa habari nchini.

“Kwa sasa mazingira ni mazuri na yanaruhusu. Lisukumeni suala hili sheria zibadilishwe sasa hivi, maana mkisubiri miaka 10 ijayo, huwezi kujua atakayekuja baada ya hapo atakuwa na mtazamo gani juu ya vyombo vya habari,”amesema Dkt.Ndumbaro.

Rais Samia tangu aingie madarakani mwanzoni mwa mwaka jana aliudhirishia ulimwengu kuwa, tasnia ya habari ni muhimu kwa ustawi bora wa maendeleo ya jamii na Taifa.

Aidha, alianza kwa kuitaka Wizara ya Habari kuvifungulia vyombo vya habari vilivyofungiwa huko nyuma huku akisisitiza wahusika wafuate sheria, jambo ambalo lilifanyiwa kazi hatua kwa hatua.

Pia, alitaka kanuni ziweke wazi makosa na adhabu zake ili kusiwe na ubabe kwa kuwa Serikali inaamini katika uhuru wa vyombo vya habari nchini.

“Nasikia kuna vyombo vya habari mlivifungia, vifungulieni, lakini wafuate sheria na miongozo ya Serikali, wafungulieni tusiwape mdomo wa kusema tunaminya uhuru wa vyombo vya habari, na kanuni ziwe wazi tusifungie vyombo vya habari kibabe,” Rais Samia aliagiza Aprili, mwaka jana katika hafla ya kuwaapisha makatibu na manaibu makatibu wakuu wa wizara mbalimbali Ikulu jijini Dar es Salaam.

Aidha, miezi kadhaa baadaye Rais Samia Suluhu Hassan alitoa maelekezo ya kufanyiwa marekebisho sheria za habari ambazo zinaonekana kuwa kikwazo katika taaluma hiyo.

Mheshimiwa Rais Samia aliyasema hayo Mei 3, mwaka huu wakati akiwahutubia Wadau wa Vyombo vya Habari kwenye maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari ikiongozwa na kauli mbiu ‘Uandishi wa habari na changamoto za kidigiti' katika ukumbi wa Gran Melia Hotel jijini Arusha.

“Nimeelekeza sheria zirekebishwe, lakini kwa majadiliano pande zote na si tu kwamba sisi tunataka nini. Nimemwelekeza Waziri sheria za habari zirekebishwe kwa kushirikisha wadau wote,"alielekeza Mheshimiwa Rais Samia.

Aidha, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mheshimiwa Nape Nnauye amesema,Serikali ilishindwa kupeleka mapendekezo ya mabadiliko ya sheria ya habari bungeni katika Bunge la Novemba, mwaka huu, kwa sababu baadhi ya taratibu hazikukamilika.

Mheshimiwa Nape ameyasema hayo Novemba 9, 2022 wakati akizungumza na uongozi wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) na Wadau wa Haki ya Kupata Habari (CoRI), jijini Dodoma.

Amesema,Serikali ilitarajia kupeleka mapendekeo hayo, lakini haikufanya hivyo kwa kuepuka mivutano kutoka kwa wadau wa habari.

Kwenye kikao hicho na CoRI, Waziri Nape amesema,Serikali ipo tayari kupeleka mapendekezo ya Sheria ya Habari kwa watunga sheria, baada ya kikao cha wadau wa habari na serikali kitakachofanyika Novemba 22, 2022, jijini Dar es Salaam.

‘‘Serikali tupo tayari kupeleka mabadiliko ya sheria ya habari bungeni baada ya kikao cha mwisho. Baada ya kikao hicho tutakubaliana tuliyokubaliana na ndio yataenda,"amesema Nape.

Amesema, haikuwa vyema kupeleka mapendekezo ya sheria ya habari bungeni wakati kuna maeneo wadau wa habari na serikali walikuwa hawajakubaliana.

‘‘Sisi kama serikali hatujakaa kimya, bado tupo vizuri kwenye mchakato huu. Nia ya serikali mpaka sasa bado ni njema. Isingefaa kwenda na mabadishano bungeni. Mpaka sasa kuna maeneo ambayo bado hatujakubaliana na kikao hicho cha mwisho ndio kitatoa mwelekeo wa mapendekezo yote,"amebainisha Waziri Nape.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news