POSA MTUNGI WA GESI:Wamama gesi wapate, hiyo ni nishati nzuri sana

NA LWAGA MWAMBANDE

SPIKA wa zamani wa Bunge la Afrika, Balozi Getrude Mongela na Waziri wa zamani wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambaye alikuwa ni Mbunge wa Jimbo la Muleba Kusini mkoani Kagera, Profesa Anna Tibaijuka (CCM) wamesema, nishati safi ya kupikia inapaswa kutazamwa kwa kina na ikiwezekana hata zile kamati za kutoa posa ziangalie uwezekano wa kuwepo kwa mtungi wa gesi ili mwanaume kupata mke.

Wameyasema hayo hivi karibuni wakati wakishiriki katika mjadala uliokuwa na mada "Wanawake wenye Ushawishi Kuhamasisha Sauti za Wanawake" ndani ya Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam, ambapo kulifanyika mjadala wa kitaifa wa nishati safi ya kupikia.

Mjadala huo, awali ulifunguliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ambaye alisema, Serikali yake imejiwekea lengo la kuachana na nishati isiyofaa ya kupikia kwa kuanzisha mfuko wa nishati, ambao fungu lake litatengwa mwaka ujao wa fedha.

Prof.Tibaijuka pia alipendekeza halmashauri kuweka utaratibu katika mkopo wa fedha wa asilimia 10 kuwepo na kipengele cha kuwawezesha wanawake kupata mitungi ya gesi, mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasema,wanawake gesi wapate, kwani hiyo ni nishati nzuri kwa matumizi ya kila siku nyumbani, endelea;


1:Posa mtungi wa gesi, mama anatushauri,
Hilo wazo siyo hasi, kama ukilifiriki,
Lengo tutumie gesi, kupikia ni vizuri,
Mnaopanga mahari, weka mtungi wa gesi.

2:Kwa ushauri asante, hilo jema siyo siri,
Ujumbe wote wapate, wanaopanga mahari,
Wamama gesi wapate, hiyo ni nishati nzuri,
Mnaopanga mahari, weka mtungi wa gesi.

4:Lengo mtungi wa gesi, tupikie kawi nzuri,
Mazingira haighasi, miti yabaki vizuri,
Moshi hauwi mkosi, afya zabakia nzuri,
Mnaopanga mahari, weka mtungi wa gesi.

5:Huo mtungi wa gesi, kuusambaza vizuri,
Kumuaga mwali gesi, sherehe ziwe vizuri,
Kumuoza gesi, iwe kati ya mahari,
Mnaopanga mahari, weka mtungi wa gesi.

6:Lengo isambae gesi, kwa kupikia ni nzuri,
Ili tupunguze kasi, nchi tukaleta hari,
Miti kushushwa kwa kasi, na moshi usomzuri,
Mnaopanga mahari, weka mtungi wa gesi.

7:Hebu ngoja nijaribu, kupanga haya mahari,
Kwanza kigoda cha babu, hizo ng’ombe zisubiri,
Mkaja mama ratibu, vyote viletwe vizuri,
Mnaopanga mahari, weka mtungi wa gesi.

8:Mbuzi wale wa mjomba, jua anawasubiri,
Mtungi gesi naomba, kwa uwazi siyo siri,
Hapo ikija mitamba, mengine sina habari,
Mnaopanga mahari, weka mtungi wa gesi.

9:Nishati safi muhimu, ituingie habari,
Kukabili hali ngumu, ambayo yaleta shari,
Tupunguze kwa awamu, kuni mkaa hatari,
Mnaopanga mahari, weka mtungi wa gesi.

10:Zawadi wanakamati, mtungi gesi mzuri,
Zigaweni zile noti, familia iwe nzuri,
Uwe kwetu mkakati, nishati safi ni nzuri,
Mnaopanga mahari, weka mtungi wa gesi.

11:Tibaijuka Mongella, asante kwa ushauri,
Kipikwe tule chakula, kwa nishati hiyo nzuri,
Toka Kyerwa hadi Kyela, mitungi gesi mahari,
Mnaopanga mahari, weka mtungi wa gesi.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news