SIASA ZA UTASHI WA KICHWA

NA ADELADIUS MAKWEGA

NOVEMBA 9, 2022 nilipigiwa simu na ndugu yangu mmoja kutoka Mahenge Mjini, kwanza akinijulia hali, alafu akiniambia naona Mwanakwetu sasa umetupatia habari za Kingunge Ngombale Mwiru, nikasema naam, huyu alikuwa mzee wetu aliyetufundisha siasa.

“Zile matini zako za Kingunge nimemuelewa msimamo wake katika dini, na hata msimamo wa kanisa, nilitamani Kingunge angepona, tumuone anavyoingia kanisani na rozali mkono na biblia .” Nikamjibu kuwa hilo tulishalikosa, Mungu alilifanyia maamuzi yake.

Ndugu yangu huyu akaniomba sasa tumzike Kingunge Ngombale Mwiru, tuzitazame siasa za Ulanga na Morogoro yetu. Nikamjibu sawa na tayari nilishamzika, nikamuuliza sasa nimfufue nani? Aliniuliza kwani unazifuatilia siasa za Ulanga kwa karibu? Nikamjibu kila siku jioni ninajua kinachofanyika Ulanga, kule wapo ndugu zangu wengi na ndiyo asili yangu. Hata hapa tunavyazungumza na wewe nayapata ya Ulanga mengi na kapu langu linajaa.

Ndugu yangu huyu akasema Mwanakwetu ulitakiwa ukaoe kwa akina Dafroza Binti Tilani wa Mawasiliano ungeyapata mengi ya Ulanga, nikamtania itabidi anifanyie mpango huo, akacheka sana akasema wapi Mwanakwetu,

“Kwa kuwa umeshamzika Kingunge sasa tuwajadili waasisi wa Ulanga, wako wengi sana kama Kasapila, Itatiro, Celina Kombani, Mponda na Dkt. Juma Ngasongwa. Marehemu Celina alitilia mkazo watoto wasome, alisaidia sana vijana kupata vyuo na waliotilia maanani wapo mbali sasa na wanaendesha maisha yao, Itatiro alisimamia ujenzi wa posta na benki, Kasapila ndiye aliyesimamia kwa karibu sana ujenzi wa Uwanja wa Mapinduzi kwa kutumia nguvu za wananchi na hakuletewa pesa na mtu, Naye Alhaj Dkt Juma Ngasongwa ndiye aliyepambana mno kuingizwa katika Ilani ya Chama ca Mapinduzi Daraja la Kilombero na alichokifanya mheshiwa Mponda sikumbuki.”

Nikamuuliza Mponda haukumbuki, alinijibu ndiyo. Nikamuuliza swali juu ya Mbunge wa Malinyi wa sasa mheshimiwa Antipas Mngungusi, ndugu huyu akanijibu kuwa,

“Kijana huyu anafanya sana na siasa zake ni za utashi, ni kijana mzuri sana kwa siasa za kesho na anauwezo mkubwa, hizo ni siasa za utashi wa kichwa.”

Ndugu huyu akaniambia kuwa siasa za utashi wa kichwa zinatakiwa sana na kila mmoja anatakiwa kulitambua hilo, na kuzilinda kwa sasa na baadaye, japokuwa walio wengi siasa hizi hawazitaki. 

Akisema kuwa kwa sasa watu wanataka siasa za pesa na watu njaa imekuwa kubwa. Akaniuliza swali ili tuondokana na siasa za njaa tunatakiwa tufanye nini? Hapo Mwanakwetu nilikaa kimya makusudi na yeye ndugu yangu huyu alikaa kimya, Mwanakwetu nikarejea swali lake kwake, sasa ili tuweze kuhama kutoka katika siasa za pesa na kwenda katika siasa za utashi tunafanyaje?
“Kwanza kabisa lazima watu wachukie kufanya siasa tegemezi na wafanye siasa za kujitegemea na hiyo ndiyo siasa ya CCM inavyotakiwa iwe. Watu watoke katika utegemezi wahamie katika kujitegemea. Tuache kuomba misaada, tufanye kazi. Kila unayemuona anacho tambua kuwa amepambana kukipata. Mathalani huyu mbunge wetu wa Ulanga mheshimiwa Salimu Hasham si anafanya kazi migodini anapata pesa? 

Wewe mpiga kura kama unasubiri ili aje kukupa wewe kila siku, kama angekuwa amekaa tu hiyo pesa unayodhani atakupa ataitoa wapi ? Wewe unapopewa pesa tambua kuwa mwezako ameifanyia kazi. Wewe unapokaa kusubiri mheshmiwa Mbunge wako wajimbo akupatie chochote tambua kuwa na yeye anafanya kazi.”

Ndugu huyu akiniambia kuwa anamwambia sana Mbunge wa Ulanga kuwa yeye hampingi kwa maendeleo yake anayoyafanya kwa maisha yake na biashara zake bali yeye anampinga sana tena sana kwa namna anavyozifanya siasa zake. Ndugu huyu akaniambia kuwa kuwa Mbunge wa Ulanga kwa namna anavyofanya biashara zake anampenda sana na anamuunga mkono kwa asilimia 100.

”Hiyo ari yako ya namna anavyozitafuta pesa kama kiongozi, inatakiwa kuwasadia wapiga kura wake, ihamishie kwa hata watu wako wa karibu na jamii ione kuwa wamebadilika kwa kuwa jirani na wewe.” Hivyo ndivyo walivyofanya akina Nyerere kiongozi akilima kwa kutumia mbolea na wananchi wanaiga hilo, akifuga ufugaji wa kisasa na jamii inafanya hivyo.

Akasema anatamani sana siasa za uhalisia kwa jamii na watu wazione na kuziheshimu. Akisema inatakiwa viongozi kuhamasisha watu walime matikiti maji, walime vitunguu na ukilima vitunguu hekari saba tu hauwezi kukosa milioni kadhaa, hiyo hautoikosa ni baada ya miezi mitatu tu utakuwa umeipata, kwanini tusifanye hivyo? Wabunge wawe wadhamini wa wapiga kura wao, jamii ijifunze kwa vitendo.

Kama ukifanya hivyo hakuna mtu ambaye atatumia muda wake kumtafuta mbunge kwenye simu, hakuna atakayesema mbunge hapatikani.

Hizi siasa za bwana tunaomba, hodi tunaomba lazima tuzibadilishe. kipindi cha uchaguzi siyo kipindi cha mavuno, jamani tufanye kazi. Kama siasa za pesa basi akina John Rupia wangekuwa marais wa Tanganyika.

makwadeladius@gmail.com
0717649257

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news