Twitter yamtoa kifungoni Donald Trump

NA DIRAMAKINI

AKAUNTI ya Twitter ya Rais wa zamani wa Marekani, Donald Trump imerejeshwa chini ya mmiliki wa kampuni hiyo ya mitandao ya kijamii, bilionea Elon Musk.
Hivi karibuni,Musk alikamilisha ununuzi wake wa kampuni hiyo kwa kuweka mezani dola bilioni 44, kulingana na mwekezaji katika kampuni hiyo.

Musk ambaye huwa anajiita mtetezi wa kuzungumza kwa uhuru awali alikuwa akikosoa sera za udhibiti za Twitter, habari ambazo zilipokelewa kwa hisia tofauti na watumiaji wa Twitter na wafanyakazi.

Baadhi ya watumiaji, hasa wale walio upande wa mrengo wa kulia wa Marekani, walisema sauti za kihafidhina zinakaguliwa kwenye jukwaa hilo, shtaka ambalo Twitter ilikanusha.

Kabla ya kumrejesha Trump, Musk alipiga kura kwa watumiaji wa Twitter siku ya Ijumaa na Jumamosi akiwauliza iwapo Trump anafaa kurejeshwa, na walio wengi walimpigia kura Trump.

Jumamosi jioni, Musk alitweet, "Watu wamezungumza. Trump atarejeshwa. Sauti ya watu ni sauti ya Mungu (Vox Populi, Vox Dei),"alibainisha Musk.
Musk alikuwa amesema hapo awali hatafanya maamuzi yoyote makuu ya maudhui au kurejesha akaunti kabla ya kuitisha baraza la kudhibiti maudhui lenye mitazamo tofauti.

Twitter lilikuwa jukwaa la kwanza kumpiga marufuku Trump baada ya wafuasi wake kuishangaza Dunia kwa kufanya maandamano na vurugu baada ya kuvamia Bunge la Marekan, kutaka kubadili matokeo ya uchaguzi wa rais wa Novemba 3,2020 yaliompa ushindi Joe Biden.

Uvamizi huo ulidaiwa kuchochewa na Donald Trump ambapo polisi katika eneo la Capitol walijibu maandamano hayo kwa kutumia bunduki na mabamu ya kutoa machozi wakati mamia ya waandamanaji walipovamia na kutaka kulilaazimisha bunge kubatilisha ushindi wa Biden dhidi ya rais Donald Trump, muda mfupi baada ya Warepublican wenzake na Trump kuanzisha juhudi ya dakika za mwisho kutupilia mbali matokeo ushindi wa Biden.

Aidha, uongozi wa Twitter wakati huo ulisema,tweets za Trump pia zilikiuka sheria zake dhidi ya kutukuza ghasia.

Hatua hiyo ilifuatiwa haraka na zile zinazofanana na hizo kutoka kwa Facebook, Instagram, YouTube, Snapchat, Twitch na kampuni zingine za mtandao.

Sasa, Twitter imekuwa ya kwanza kurejesha akaunti ya rais huyo wa zamani, na kumpa fursa ya kupata tena kipaza sauti chenye nguvu ambacho alikitumia kwa miaka mingi kushambulia maadui wa kisiasa, kuwarubuni mashabiki na kuendesha mzunguko wa habari wa kila siku, na pia kufikia hadhira ya karibu asilimia 90.

Mara nyingi, licha ya kuwafikia wafuasi milioni kadhaa pia tweet zake zilikuwa zikikuzwa katika Twitter na katika vyombo vya habari vya kawaida.

Tweet ya mwisho ya Trump ilikuwa ya Januari 8, 2021. Ikiwa Trump atakubali mwaliko wa kurejea Twitter ni suala jingine.

Wakati wa hotuba ya Jumamosi kwa Muungano wa Kiyahudi wa Republican, Trump alisema,"Sioni sababu yake," kulingana na Bloomberg News.

Baada ya uhamisho wake kutoka kwa mitandao ya kijamii ya kawaida, Trump na baadhi ya washirika wake walizindua tovuti pinzani ya kijamii iitwayo Truth Social (Ukweli wa Kijamii).

Musk ambaye alinunua Twitter kwa dola bilioni 44 baada ya miezi kadhaa ya mabishano ya kisheria juu ya kama atapitisha mpango huo, ameapa kufungua uwezo wa kampuni hiyo kwa kuendeleza uhuru wa kujieleza.

Kabla ya ununuzi wake, Musk alikuwa amekosoa sheria za jukwaa dhidi ya unyanyasaji, matamshi ya chuki na madai ya uwongo kuhusu uchaguzi na afya ya umma, akisema inapaswa kuruhusu hotuba zote za kisheria.

Katika wiki za kwanza za umiliki wa Musk wa Twitter, wengi wa wafanyakazi na wakandarasi ambao wana jukumu la kuhakikisha kuwa maudhui zenye mashaka hazichukui nafasi katika jukwaa waliachishwa kazi au waliacha kazi.

Musk pia amesema, anapinga wazo la kupigwa marufuku kudumu kwa mitandao ya kijamii, na katika mkutano mwezi Mei, alielezea uamuzi wa Twitter wa kupiga marufuku Trump kuwa ni mkiukaji wa maadili huku akidai huo ni upambavu uliokithiri.

"Nadhani hilo lilikuwa kosa kwa sababu lilitenga sehemu kubwa ya nchi na halikusababisha Donald Trump kutokuwa na sauti,"alisema.

Bado, Musk amesisitiza kwamba tovuti hiyo itasisitiza kile alichokiita "tweets hasi au chuki". Tayari amebatilisha marufuku kwenye akaunti nyingine zenye utata, ikiwa ni pamoja na mwandishi wa mrengo wa kulia na mwandishi wa podikasti Jordan Peterson na tovuti ya kihafidhina ya kejeli The Babylon Bee.

Kurejeshwa kwa Trump kwenye Twitter kunakuja wakati wa wasiwasi mkubwa juu ya uwezekano wa ghasia za kisiasa zinazochochewa na mgawanyiko unaokua na maneno makali kutoka kwa Republican ambao wanaendelea kukataa kwamba Trump alishindwa katika uchaguzi wa urais wa 2020.

Uamuzi wa Twitter, unatajwa kuwa huenda ukawa na athari zaidi katika jukwaa lake, hasa kwa tangazo la Trump kwamba anagombea tena urais mwaka 2024.

Kwa upande wa Facebook bado wanafanya tathimni iwapo itamfungulia Trump, mwezi Januari 2023 ingawa YouTube imesema itamruhusu Trump kuchapisha video tena wakati hatari ya vurugu inapungua, lakini haijatoa ratiba yoyote kwa sasa.(Bloomberg/NPR)

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news