UJENZI VITUO VYA MAFUTA: MARUFUKU HII NZURI

NA LWAGA MWAMBANDE

NOVEMBA 10, 2022 Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Angeline Mabula amesitisha utoaji wa vibali vipya vya ujenzi wa vituo vya mafuta na mabadiliko ya matumizi ya ardhi kwa ajili ya ujenzi wa vituo hivyo kwa muda wa miezi mitatu kuanzia sasa.

Waziri ametoa agizo hilo ili kutoa nafasi kwa Wizara ya Ardhi na wizara zinazohusika na utoaji vibali kufanya tathimini ya kina kuhusu ujenzi wa vituo vya mafuta kufuatia kuwepo kwa ujenzi unaokiuka maelekezo ya mipango kabambe iliyopo.

Waziri Mabula ametoa agizo hilo mbele ya vyombo vya habari jijini Dodoma na kuongeza kuwa, baadhi ya wamiliki wamekuwa wakiomba vibali vya ukarabati wa majengo chakavu mijini na baadae kufanya uendelezaji wa maeneo hayo kinyume na mipango kabambe iliyopo.

Ameongeza kuwa, pamoja na kuwepo kwa kanuni husika, kumekuwepo na ujenzi holela wa vituo vya mafuta nchini usiozingatia matakwa ya Sheria ya Mipangomiji na Kanuni zake jambo linalochagiza uwepo wa agizo hilo la kusitisha vibali hivyo.

Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasema,marufuku hiyo ni nzuri ikizingatiwa kuwa, ujenzi wa vituo vya mafuta kiholela ni sawa na kujichimbia kaburi, endelea;

1:Marufuku hii nzuri, wote tupate habari,
Ujenzi huu hatari, unatuletea shari,
Twajichimbia kaburi, hiyo wazi siyo siri,
Ni vituo vya mafuta, vimetapakaa hovyo.

2.Hebu tembea tembea, na uangaze vizuri,
Vituo vimeenea, ni vingi kama magari,
Watu wanajijengea, bila hata tahadhari,
Ni vituo vya mafuta, vimetapakaa hovyo.

3.Tena waweza shangaa, vituo hivyo vizuri,
Hapa pale vyazagaa, kama vile ni mihuri,
Magari yapate njaa, yajipatie mtori,
Ni vituo vya mafuta, vimetapakaa hovyo.

4.Hii mipango ya miji, mingi kwa kweli mizuri,
Kwa barabara na maji, miradi yawa mizuri,
Huko tuna mahitaji, tekeleza kwa hiyari,
Si vituo vya mafuta, vimetapakaa hovyo.

5.Mbona taratibu zipo, zinasomeka vizuri,
Ili kituo kiwepo, umbali wake ni mzuri?
Wa kutazamana upo, umbali mbona hatari?
Ni vituo vya mafuta, vimetapakaa hovyo.

6.Ni Waziri wa Ardhi, katupatia habari,
Vituo vingi maudhi, vyaweza kuleta shari,
Leseni sasa kahodhi, kuzigawa ni sifuri,
Ni vituo vya mafuta, vimetapakaa hovyo.

7.Enyi wenye mamlaka, elewa hilo vizuri,
Wala msitie shaka, katazo hili ni zuri,
Sheli mnapoziweka, lazima pawe pazuri,
Ni vituo vya mafuta, vimetapakaa hovyo.

8.Miezi hii mitatu, tuitumie vizuri,
Kufanya mambo kiutu, tukwepe hizi hatari,
Vituo vya sheli katu, ni bomu siyo sukari,
Ni vituo vya mafuta, vimetapakaa hovyo.

9.Tembea barabarani, ujionee vizuri,
Hapa na hapo njiani, vituo vingi hatari,
Taratibu vitabuni, nazo hawana habari,
Ni vituo vya mafuta, vimetapakaa hovyo.

10.Wasimamia sheria, tusimamie vizuri,
Bila ya kusubiria, amri yake waziri,
Zahama ikitujia, mtaipata shubiri,
Ni vituo vya mafuta, vimetapakaa hovyo.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news