HII ILIKUWA MWAKA GANI?

NA ADELADIUS MAKWEGA

KUNA familia moja ilikuwa inaishi kijijini wakati wa ujamaa, wakiwa na maisha ya kimaskini sana, wakiendesha maisha yao kwa kilimo kidogo kidogo na ufugaji wa kuku wa kienyeji.

Kila kunapokucha huamka asubuhi baba, mama na watoto wao wawili shambani na baadae hurudi nyumbani kungoja siku nyingine.

Siku moja waliamka asubuhi kama ilivyo desturi yao wakabeba mundu, majembe na shoka kuelekea huko. Wakafika, wakalima eneo kiasi. Wakiwa wanalima siku hiyo, hali ya hewa ikabadilika gafla, radi zikawa zinapiga na kumulikamulika huku kukiwa na upepo mkali mno.

Jambo hilo liliwatia mashaka, kwa kuwa shamba lao lilikuwa pahala ambapo yalikuwa makazi yao ya awali kabla ya kuhamishwa na vijiji vya ujamaa, hadi kufika hapo ni lazima huvuke mto na ulikuwa umbali wa saa tatu kwa miguu na kama mvua ikinyesha wakiwa bado wapo shambani kurudi nyumbani inakuwa ngumu, kwani kuna mto mkubwa unaojaa maji.

Wakakata shauri kuwa kwa kuwa radi zinapiga kwa mingurumo mingi, mwanga wa umeme wa radi na upepo ni mkali, kwa hakika mvua inaweza kunyesha wakaamua kuchukua vifaa vyao kurudi nyumbani kuokoa uhai wao.

Wakati mazungumzo hayo ya kurudi nyumbani yakifanyika, mama huyu alikuwa anajiuliza je kama tunarudi nyumbani je tutakwenda kula ugali na mboga gani? Naye baba akijiuliza kichwani kuwa kwa kuwa siku hiyo jioni kulikuwa na mechi ya mpira wa miguu baina ya Simba na Yanga, je mvua ikinyesha wakiwa bado hawajafika nyumbani vipi kuhusu yale mabetri yake aliyoyaanika asubuhi yakiloa itakuwaje?.

Baba huyu alitambua kuwa hilo likitokea mechi hiyo ya watani wa jadi ataikosa. Hapo mwanakwetu kila mmoja akili yake ina wazo lake. Afadhali ya mama anafikiria chakula cha familia, lakini baba anawaza ulevi wa mpira. Mama yupo kulia, lakini baba yupo kushoto.

Safari ya saa tatu ni ndefu, ukiwa njiani, kuchimba dawa ni jambo la kawaida mno. Mtoto mdogo mbele, anafuata mama anakuja mtoto mwingine wa kiume, halafu baba nyuma.

Baba alibanwa kidogo, akamdokeza mkewe kuwa naomba nichekupe ili nichimbe dawa, kwa hiyo mama akarudi nyuma na mbele wakabaki watoto wao wawili wakienda taratibu.

Baba alipomaliza akarudi zake huku akiwa tumbo wazi, amefungasha kitu katika shati lake. Mkewe akauliza mume wangu kulikoni tena mbona tumbo wazi? Watoto na watu njiani watakuona, unanivunjia heshima! Mwanaume huyu akasema kuwa mke wangu wewe niache tu.

Baba huyu akawa anapiga miluzii tu, akamwambia mkewe utanielewa baadae. Mama alidhani kuwa mumewe alipokwenda kujisadia pengine alipatwa na tumbo la kuhara kwa hiyo kwenye kifurushi kile amekusanya nguo zake zilizochafuka kwa tumbo hilo.

Mwanakwetu safari yao ilikuwa inaendelea, mama akiwa na ameubinua mdomo mno kwa kitendo cha mumewe kuwa tumbo wazi hadi kijijini wakati hiyo haikuwa tabia yake.

Walipofika nyumbani mama aliingia ndani na baba huyu akamwambia mkewe alete ungo. Kweli mama huyu akatoka na ungo akampelekea mumewe. Kwa desturi za mila za kiafrika ungo, mwiko, chungu na upawa ni vifaa vya mapishi na mara nyingi hutumiwa na wanawake.

Mama akajiuliza leo kulikoni? Alipokabidhiwa ungo huo, baba huyu alitua furushi lake, kumbe ulikuwa uyoga mwingi aliouvuna baada ya kuuona kwa ngekewa wakati akijisaidia, akaujaza katika ungo huo na kumkabidhi mama huyu ili apike.

Mama aliingia mekoni na kuanza matayarisho, akaupika vizuri sana, lakini akiogopa kuuonja kwa kuwa kuna aina za uyoga zenye sumu.

Ulipoiva akauchota kidogo na kumpa paka wake ili ale kama hauna sumu.Paka huyo kwa kuwa na yeye alikuwa na njaa aliufakamia na kuumaliza, mama alipoona baada ya muda paka yu hai, alitenga chungu mekoni na kusonga ugali, ulipoiva walianza kula familia nzima.

Walipomaliza kula, baba akayaanua mabetri yake yaliyokuwa juani na kuyaweka katika redio ya mkulima na kuanza kusikiliza matangazo ya redio ya mpambano huo wa Simba na Yanga.

Mtoto mdogo alielekea kucheza na wenzake, akiwa huko mara akamuona paka wao anajitupatupa chini huku akijigeuzageuza (galagala). Mtoto huyu akamkimbilia mama yake.

“Mama mama mama ! paka wetu anakufa, paka wetu anakufa!”. Ahamadi! baba na mama hawa wakachanganyikiwa, kulikoni tena, redio ikaangukiwa huko na mabetri yakatoka nje.

Familia hii wakakusanyika pamoja, hali ndiyo hivyo, hapa hakuna ubishi tumekula uyoga wenye sumu, kama mnavyoona paka wetu ndiyo anakufa, sasa tunafanyaje?.

“Umbali kutoka hapa hadi kanisani kumuomba padri kusali sala ya mwisho tunaweza tusifike huko, lakini pia padri mwenyewe amekwenda jimboni! Hapa kila mmoja amuungamie mwenzake na tusali sala ya mwisho.” Baba alitoa wazo hilo.

Mama huyo alikubali mawazo ya mumewe na kusema kuwa mke wangu mimi naanza kuungama kwako. Baba akapiga magoti na kumuinamia mkewe na kutaja dhambi zake,

“Mungu wangu na mbele ya mke wangu mimi nimezaa na mwanamke mwingine kijiji cha ng’ambo naomba Mungu unisamehe na mke wangu nisamehe.” Mama bila ya kupoteza muda kuwahi muda wake wa kuungama akamsamehe mumewe.

Mama na yeye akaanza kuungama “Mungu wangu na mbele ya mume wangu, naomba unisamehe sana, huyu mtoto wa mwisho siyo wa mume wangu, ni mtoto wa mwanaume mwingine, sitaki nife na hii dhambi.”

Mwanaume huyu kazi ya kuungamisha ilimshinda, akahamaki,. “Unasemaje wewe mwanamke?”. “Mungu wangu na mbele ya mume wangu, huyu mtoto siyo wa mume wangu, Mungu na mume wangu mnisamehe.”

Wakati mvutano huo wa maungamo ukiendelea, mara mtoto wa jirani akaja huku akiwa amevibeba vitoto vidogo vya paka. Akisema: “Paka wenu kazaa, chukueni vitoto vyake, hivi hapa.”

Maneno haya yalileta faraja kubwa ambayo si ya kawaida. Mvutano huo ukatulizwa na neno hilo. Mama akarudi zake jikoni kuandaa chakula cha jioni na Baba huyu akachukua redio yake ya mkulima na kuiweka betri vizuri, akaiwasha kusikiliza mpambano huo wa Simba na Yanga matokeo yake.

Mwanakwetu Simba alishamchakaza Yanga magoli sita kwa bila. Baba huyu ambaye alikuwa shabiki wa Simba alikuwa na furaha mara tatu, kwanza uyoga waliokula haukuwa na sumu, pili amesamehewa dhambi zake na tatu Simba ilishinda mechi hiyo.

Mwanakwetu amani ilirudi katika familia hiyo.Msomaji wa matini hii nimalizie kwa swali kwako. Je, hii ilikuwa mwaka gani?. Nakutakia siku njema.

makwadeladius@gmail.com
0717649257

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news