KITEMA:Siigize ufukara, huku umebarikiwa ndugu

NA LWAGA MWAMBANDE

WAKATI wa uhai wake,Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP, Dkt.Reginald Mengi amewahi kusisitiza kuwa, katika maisha, “Unaweza kuushinda umaskini kama uko tayari kulipa gharama. Gharama hiyo ni kufanya kazi kwa bidii”.

Pia unapofanikiwa, unapaswa kuhakikisha unazingatia maadili mema ambayo yatakuunganisha na watu ili kuepuka kuyooshewaa kidole kutokana na namna ambavyo unajiweka licha ya utele ulio nao.

Maneno hayo machache ya Hayati Dkt.Reginald Mengi yalikuwa na nguvu na ujumbe mkubwa kwa wale wenye nia ya dhati ya kujikwamua kutoka lindi la umaskini hadi kuwa tajiri.

Ni tamanio la kila mmoja wetu kuwa na wingi wa vitu vya thamani na wa vyanzo vya mapato ambavyo vitatuwezesha kukidhi matarajio na malengo ya maisha yetu kwa ustawi bora wa familia na Taifa kwa ujumla.

Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasisitiza kuwa, pale ambapo Mungu amekubariki achana na uchakavu, onekana katika hali ya kuwapa hamasa wengine ili nao waweze kustawi kama wewe, badala ya kukumbatia ukale, endelea;

1. Vipi wavaa kitema, hali uwezo unao?
Wafurahi kukusema, hata mbele ya wanao?
Mungu kakupa neema, kitema wachie hao,
Siigize ufukara, huku umebarikiwa.

2. Hizo nguo kuukuu, siyo zako ni za wao,
Ambao yule mkuu, hajashusha nema kwao,
Wewe kakupa makuu, mbona wawa kama wao?
Siigize ufukara, huku umebarikiwa.

3. Uchumi wako ni mwema, unayapata mafao,
Hebu vaa nguo njema, kiwa nje ya makao,
Nyumbani vaa kitema, unapovuna mazao,
Siigize ufukara, huku umebarikiwa.

4. Au umeshaingizwa, kwenye ndumba zao hao,
Ambao wameelezwa, kitema ni vazi lao,
Kama hivyo umeponzwa, umeuacha mbachao,
Siigize ufukara, huku umebarikiwa.

5. Tajiri kwenye kitema, unaleta mshangao,
Ona watu wakusema, umevaba ndumba zao,
Ni bora ukachutama, ukwepe maneno yao,
Siigize ufukara, huku umebarikiwa.

6. Miguuni pekupeku, waso na viatu hao,
Hata kununua luku, kwako giza kama kwao,
Mbona sasa twakushuku, huo wa kwako mkao?
Siigize ufukara, huku umebarikiwa.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news