Lakini Yanga SC jamani...

NA DIRAMAKINI

YOUNG Africans Sports Club (Yanga SC) imeendelea kujisimika kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara kwa alama 47.

Wanajangwani hao wameendeleza rekodi ya ushindi leo Desemba 25, 2022 baada ya kuamua kusherehekea Sikukuu ya Krisimasi kwa kuicharaza Azam FC ya jijini Dar es Salaam mabao 3-2.

Ni kupitia mtanage wa nguvu ambao umechezwa katika Dimba la Benjamin Mkapa lililopo Halmashauri ya Manispaa ya Temeke jijini Dar es Salaam.

Azam FC walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Abdul Sopu dakika ya 27 akimalizia pasi ya Prince Dube huku Yanga SC wakipata mabao kupitia kwa Fiston Mayele dakika ya 31 na Stephane Aziz Ki dakika ya 33.

Dakika 45 za kipindi cha kwanza, zilitamatika kwa mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania BARA kwenda mapumziko wakiwa wanaongoza kwa mabao.

Aidha, kipindi cha pili Azam FC walipata bao la mapema dakika ya 47 likifungwa na Abdul Sopu na bao la ushindi la Yanga SC lilifungwa na Farid Mussa dakika ya 78.

Matokeo hayo yanawafanya Yanga SC ya jijini Dar es Salaam kufikisha alama 47 na kuiacha Azam FC kwa tofauti ya alama 10 huku wakicheza bila kiungo wao Fei Toto anayedaiwa kusajiliwa na Azam FC, ingawa bado suala hilo limekuwa na mjadala mrefu.
 
Wakati huo huo, Tanzania Prisons imeibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya mahasimu wao wa Jiji, Mbeya City leo Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.

Mabao ya Prisons yamefungwa na Zabona Khamis dakika ya 27 na Samsons Mbangula dakika ya 47, wakati la Mbeya City limefungwa na Baraka Mwalubunju dakika ya 61.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news