TUNAHITAJI UMEME, TULIJAZE BWAWA LETU

NA LWAGA MWAMBANDE

LEO Desemba 22, 2022 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt.Samia Suluhu Hassan anazindua ujazaji maji katika Bwawa la Kufua umeme kwenye Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) uliopo Rufiji mkoani Pwani.

Ni baada ya hatua ya kujenga tuta linalosaidia uhifadhi wa maji katika bwawa hilo kukamilika. Mheshimiwa Rais Dkt. Samia anafanya uzinduzi huo katika hafla inayofanyika eneo la mradi kwa kubonyeza kitufe kitakachoshusha mageti yatakayoziba njia ya mchepusho wa maji na kuruhusu maji kuanza kujaa katika bwawa.

Hatua hiyo ya kujaza maji katika bwawa hilo lenye ukubwa wa mita za ujazo 32.3, inatazamiwa kutumia misimu miwili ya mvua kukamilisha kujaa na kuruhusu kuwashwa kwa mitambo ya kufua umeme.

Awali, Waziri wa Nishati, January Makamba alitaja moja ya faida za mradi huo ukiacha kufua umeme ni kwa wakulima wanaolima katika Bonde la Mto Rufiji kwa sababu utazuia mafuriko yaliyokuwa yakisababisha mazao kuharibika na kuanzia sasa maji yatakayoelekea upande wa chini kwa wakulima yatakuwa yamedhibitiwa na kufika kwa kiwango kinachostahili.

Mradi huo unaotarajiwa kufua megawati za umeme 2,115, unatarajiwa kuondoa tatizo la uhaba wa umeme nchini na kupunguza gharama kwa wananchi.

Ongezeko hilo la megawati 2,115 litawezesha Tanzania kujitosheleza kwa mahitaji yake ya umeme na kuwa na ziada ya kuuzwa nje ya nchi. Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasema, hii ni hatua muhimu ambayo kila Mtanzania anapaswa kuiombea heri ili iweze kufanikiwa kwa ufanisi, endelea;


1:Bwawa langu Bwawa lako, hili hasa Bwawa letu,
Ndilo laleta mwamko, kwa maendeleo yetu,
Kuyajaza maji huko, inaanza kazi yetu,
Tunahitaji umeme, tulijaze Bwawa letu.

2:Zoezi ndio laanza, kulijaza Bwawa letu,
Rais ndiye wa kwanza, kulijaza Bwawa letu,
Twalijenga twalitunza, litufae bwawa letu,
Tunahitaji umeme, tulijaze bwawa letu.

3:Kazi iliyofanyika, hiyo kubwa sana kwetu,
Pesa zilizotumika, tokana na kodi zetu,
Twasubiri kwa hakika, tulivune jasho letu,
Tunahitaji umeme, tulijaze bwawa letu.

4:Huu moja ya miradi, ya kimkakati kwetu,
Walishaweka miadi, hawa viongozi wetu,
Kujengwa hadi akidi, tupate umeme wetu,
Tunahitaji umeme, tulijaze bwawa letu.

5:Huku kulijaza maji, yatimie bwawa letu,
Subira tunahitaji, tufanye hesabu zetu,
Lifike tunapohitaji, tupate umeme wetu,
Tunahitaji umeme, tulijaze bwawa letu.

6:Alianza Magufuli, kulijenga bwawa letu,
Kweli ni mradi ghali, kwa rasilimali zetu,
Lakini twaona mbali, hasa mahitaji yetu,
Tunahitaji umeme, tulijaze bwawa letu.

7:Wakati alipokufa, likiwa kitete kwetu,
Kwamba yake maarifa, yatazidi faa kwetu,
Tulidhani itakufa, huo na miradi yetu,
Tunahitaji umeme, tulijaze bwawa letu.

8:Kuja Rais Samia, huyu kiongozi wetu,
Mwanzoni lituambia, atakayofanya kwetu,
Na kutusisitizia, tukamuamini watu,
Tunahitaji umeme, tulijaze bwawa letu.

9:Aliyoanza miradi, yule kiongozi wetu,
Ihesabu kwa idadi, iliyo nchini mwetu,
Itafikia akidi, tufaidi nchi yetu,
Tunahitaji umeme, tulijaze bwawa letu.

10:Kweli serikali yake, Rais Samia wetu,
Yafwata kauli yake, kujenga miradi yetu,
Siyo bwawa peke yake, na mingine hii yetu,
Tunahitaji umeme, tulijaze bwawa letu.

11:Mambo yanaendelea, tunaona reli yetu,
Sasa tunaelekea, itubebe sisi watu,
Dodoma kunanogea, kujengwa makao yetu,
Tunahitaji umeme, tulijaze bwawa letu.

12:Mazuri mengi Tanzania, aleta Rais wetu,
Afya maji Tanzania, zanoga huduma zetu,
Elimu nakutajia, na mengine bora kwetu,
Tunahitaji umeme, tulijaze bwawa letu.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news