UVUNGUNI HADHARANI:Hata nusu alama ina maana kubwa katika matokeo ya mwanafunzi

NA ADELADIUS MAKWEGA

DESEMBA 11, 2022 mwanakwetu alipita njia wakati anakwenda kanisani na kurudi, akikutana na picha ya twiga wawili wakiwa wamependeza mno, huku twiga hao wakionekana ni twiga waliochukuliwa mbuga za Mikumu, Serengeti na Selous na kuwekwa hapo.

Mwanakwetu akisema kuwa hiyo ni mboga kabisa, umelo ukamjia, lakini baadaye alibaini kuwa macho yake yanamfanyia danganya toto kula kunde mbichi-wale walikuwa twiga wa saruji waliotengenezwa vizuri.

Jambo hilo lilimpa faraja kubwa sana akakata shauri na kuwapiga picha bibi na bwana wa twiga wa saruji muda huo huo.

Akiwa hapo kigulu na njia kuelekea nyumbani kwake mwanakwetu akakumbuka tukio moja la mwaka 2003 akiwa mwalimu wa shule moja binafsi ya kimataifa yenye shule ya msingi na sekondari jijini Dar es Salaam, wakati huo mwanakwetu akifundisha Kiswahili darasa la saba hadi kidato cha nne na mama mmoja akifundisha somo hilo darasa la tatu hadi la sita.

Shule hii ilikuwa na wanafunzi kutoka mataifa mengi huku mwalimu Mwita Mwikabe akifundisha Basic Mathematics ambaye baadaye aliwahi kuwa Naibu Waziri wa Wizara kadhaa ikiwamo TAMISEMI, wakati huo mwalimu Mwikabe akiwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Novemba 2003 mitihani ya kufunga shule ilifanyika na kusahihishwa na kurejeshwa kwa wanafunzi wote na jioni walirudi nayo makwao wale waliokuwa hawakai bweni.

Kazi iliyobaki ilikuwa ni kwa walimu wa madarasa kutayarisha ripoti za wanafunzi, tambua kuwa mwanakwetu hakuwa mwalimu wa darasa.

Zoezi hilo likiendelea shuleni hapo akafika mgeni na kupokelewa na Mkuu wa Shule (Principal) akazungumza naye alafu wakaitwa walimu wawili; mwalimu wa Kiswahili darasa la tatu na Profesa Simbaulanga ambaye yeye alikuwa ni mjuzi wa lugha ya Kifaransa na akisomesha vyuo na taasisi mbalimbali na wakati huo Profesa Ulanga alishastaafu serikalini.

Walizungumza huko ofisini alafu wakatoka zao na mgeni huyo kuondoka zake, huyu Profesa Simbaulanga alikuwa ni Mpogoro huku akizungumza vizuri Kipogoro na kwa kuwa mwanakweu ni Mpogoro profesa huyu alipenda sana kuongea kwa lugha hiyo, lakini mwanakwetu ni fukara kabisa wa lugha hii.

Profesa huyu akimuhimiza mwanakwetu kujifunza lugha ya kwao naye mwanakwetu akijitahidi kuokotezaokoteza maneno ya lugha hii.

Profesa Simbaulanga akamwambia mwanakwetu, unafahamu kuwa nilikuwa natambua wewe unafundisha Kiswahili hadi darasa la tatu, mwanakwetu aliuliza kwa nini? Profesa Simbaulanga alijibu kuwa leo tuliitwa kwa Principal, alifika Profesa Masamba Masamba aliulizia mbona mtoto wake anayesoma darasa la tatu amewekewa makosa katika swali mojawapo la somo hilo?.

“Mtoto wa Profesa Masamba mwenye jina la Masamba Masamba alipokea karatasi za mitihani na kuwapelekea wazazi wake nyumbani, akaziweka mezani na baba yake aliporudi alikagua karatasi moja baada ya nyingine na kubaini kuwa katika somo la Kiswahili mwanafunzi huyu aliwekewa alama ya mkasi isivyo halali.”

Shuleni hapa pakawa na gumzo kubwa, kila mwalimu akiogopa kufuatwa na Maprofesa na wahadhiri Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

“Hata nusu alama ina maana kubwa katika matokeo ya mwanafunzi.” Profesa Simbaulanga alimwambia mwanakwetu.

Kweli alama hiyo ilirekebishwa katika matokeo ya jumla na Masamba Masamba akapata ripoti yake ya kumaliza darasa la tatu na kuingia darasa la nne.

Maisha ya kufundisha shuleni hapo yaliendelea mwanakwetu alikuwa na wanafunzi rafiki zake wengi tangu shuleni ya msingi na sekondari. Shule ya msingi marafiki wa mwanakwetu walikuwa ni Upendo Kisai na Masamba Masamba.

Masamba Masamba (Mtoto wa Profesa Masamba) mara nyingi alikuwa anashiriki vipindi vya watoto wa RTD na wakati huo mwanakwetu alikuwa mpenzi wa kusikiliza redio hii ya umma, mwanakwetu alipofika shuleni hapo kusomesha ndipo alipokutana na Masamba Masamba ambaye alikuwa mwanafunzi mcheshi sana na anayejiamini mno.

Mwanakwetu kabla ya tukio hilo aliwahi kuzungumza na Masamba Masamba namna alivyokuwa akishiriki vipindi hivyo na alivyokuwa anajibu maswali redioni na baada ya tukio hilo akamtania Masamba Masamba akisema naona umekwenda kutusemea kwa baba yako. Masamba Masamba akacheka sana akasema kimombo,

“No teacher what I did, it was just like a pupil of grade one, I took a wooden giraffe under the table and kept it on top of the table where my Daddy just saw it-Mwalimu nilichofanya ni kama mtoto wa darasa la kwanza kumchukua twiga wa mbao kutoka chini ya meza na kumuweka juu ya meza naye baba akamuona.”

Mwanafunzi huyu aliendea kumwambia mwanakwetu kuwa, baba yake ni mkali sana na anafuatilia mno mambo yake ya shule na alipobaini hilo ndiyo akaenda shuleni na yeye alitambua hilo baada ya mwalimu Rehema, mwalimu wa darasa kumuita.

Mwanakwetu upo?

Nakuuliza swali msomaji wangu, je na wewe una soma haya yanayoandikwa andikwa ? Nakushauri yapitiepitie yale yote yanayowekwa mezani mwako usihangaike kumfuata Masamba Masamba, watafute wale waliosababisha alama vema kuwa mkasi ambayo ina madhara makubwa hapo mbeleni, ukiwafuata watarekebisha hilo na mara zote watasema,

“Jamani wazazi wanayafuatilia. Hata nusu alama ina maana kubwa katika matokeo ya mwanafunzi.” Hakika mwanafunzi huyu aliweza kumtoa twiga wa mbao uvunguni kumuweka hadharani

makwadeladius @gmail.com
0717649257

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news