Waziri Simbachawene azindua Programu ya Education Plus

NA MWANDISHI WETU

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera Bunge na Uratibu, Mhe. George Simbachawene amezindua Programu ya Education Plus inayolenga kuhakisha vijana balehe (wasichana na wavulana) wanawezeshwa kuishi maisha salama, yenye afya, na tija-bila ukatili wa kijinsia, VVU na UKIMWI.
Akizindua programu hiyo Novemba 30, 2022 wakati wa hafla ya kuhitimisha Wiki ya Vijana katika kuelekea Siku ya UKIMWI Duniani mkoani Lindi, Waziri Simbachawene amesema amefarijika kwa jitihada za Taasisi ya TACAIDS pamoja na wadau katika utekelezaji wa afua za masuala ya UKIMWI nchini.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu, Mhe. George Simbachawene akizindua Mpango wa Education Plus katika kilele cha shughuli za vijana kuelekea Maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani ambayo Kitaifa yatafanyika mkoani Lindi. (Picha na OWM).

Ametumia fursa hiyo kuwaasa vijana wote nchini kuzingatia jitihada za Serikali katika mapambano ya VVU na UKIMWI kwa kuendelea kujilinda na kulinda wengine huku wakijiepusha na tabia hatarishi.

“Rai yangu kwa vijana wote nchini, hususani wasichana, fanyeni kila muwezalo ikiwa ni pamoja na kuzingatia maudhui ya kampeni mbalimbali ili kujikinga na maambukizi ya VVU. Wale mlio shuleni na vyuoni hakikisheni mnaweka mkazo katika elimu na kujiepusha na tabia zote hatarishi zinazopelekea kupata maambukizi ya VVU,”amesema Waziri Simbachawene.
Aidha, aliwasihi vijana walio nje ya shule na vyuo, kuzitumia fursa zilizopo katika kuviwezesha vikundi vya vijana kujiinua kiuchumi hii itasaidia kujiepusha na tabia za kukaa vijiweni na kushawishika kujiingiza katika vitendo vinavyopelekea kuwa katika hatari ya kupata maambukizi ya VVU.

Akieleza hali ya maambukizi nchini Waziri Simbachawene amesema katika kuelekea lengo la sifuri ya maambukizo mapya, kama nchi maambukizo mapya yameendelea kushuka mwaka hadi mwaka, japokuwa sio kwa kasi ya kuridhisha. Kwani, hadi sasa takwimu zinaonesha kuwa takribani watu 54,000 waliambukizwa VVU mwaka 2021 nchini. Hii ni sawa na takribani watu 4,500 kwa mwezi au watu 150 kwa siku.

“Vijana wenye umri wa miaka 15-24 ndio kundi ambalo linaonyesha kuwa na kiwango kikubwa cha maambukizo mapya, kwani katika watu wote wanaopata maambukizo mapya ya VVU kila mwaka, takribani asilimia 30 ni vijana wenye umri wa miaka 15-24 (yaani katika kila watu 10 wanaopata maambukizo mapya ya VVU watatu ni vijana wa umri huu),”amesisitiza.

Katika kundi la vijana wa miaka 15-24 wanaopata maambukizo mapya, takriban amesema, asilimia 70 ni wasichana. Katika mwaka 2021, kulikuwa na maambukizi mapya 212 kila wiki kwa kundi la wasichana wa miaka 15-24 hivyo inamaanisha maambukizi mapya 30 kila siku.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news