Wizara ya Uwekezaji yawauma sikio SIDO, DIT kuhusu Mpango wa Pili Jumuishi wa Kitaifa wa Lishe (NMNP II)

NA MWANDISHI WETU

KATIBU Mkuu Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara,Dkt. Hashil Abdallah amesema kuwa Wizara hiyo ni moja ya Wizara za Kisekta hapa nchini zinazotekeleza Mpango wa Pili Jumuishi wa Kitaifa wa Lishe (NMNP II) kwa kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji na ufanyaji wa biashara katika sekta ya chakula na lishe.
Dkt. Abdallah ameyasema hayo Disemba 15,2022 alipokuwa katika ziara ya kukagua Teknolojia za kuongeza virutubisho kwenye unga wa mahindi zilizobuniwa na taasisi za SIDO na DIT jijini Dar es Salaam.
Amesema kuwa, katika mpango huo, Wizara ina jukumu la kuhakikisha Sera, Miongozo na taratibu zinaendana na agenda ya nchi katika kupunguza changamoto ya utapiamlo hapa nchini.

"Suala la urutubishaji ni kwa mujibu wa kanuni ya urutubishaji ya mwaka 2011 ambapo inawataka wazalishaji wote wa chakula hasa unga wa ngano, unga wa mahindi, chumvi na mafuta ya kula kuongeza virutubishi vilivyoainishwa kwa mujibu wa sheria,"amesema Dkt. Abdallah.
Akitolea ufafanuzi kuhusu suala la urutubishaji wa chakula (food fortification) kwa viwanda vya kati na vikubwa, amesema kwa sasa asilimia kubwa ya viwanda hivyo wanatekeleza bila changamoto yoyote, ambapo changamoto iliyopo ni kwa wasindikaji wadogo sana na wadogo.

Aidha, amesema kuwa wasindikaji hao, wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya uelewa juu ya umuhimu wa kurutubisha chakula lakini pia wanakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa teknolojia za kuongeza vurutubishi wakati wa uzalishaji.
"Katika kukabiliana na changamoto hiyo Serikali kupitia Taasisi zake za SIDO na DIT wameweza kubuni teknolojia rahisi za kuongeza virutubishi ambazo zitatumiwa na wasindikaji wadogo sana na wadogo. Teknolojia hizi, zitauzwa kwa bei rafiki ili wasindikaji wengi wapate kuzitumia na kutimiza ajenda ya Taifa ya kupunguza utapiamlo kutoka asilimia 31.8 iliyopo sasa, mpaka asilimia 24 kufikia mwaka 2026," amefafanua Dkt. Abdallah.

Ameongeza kuwa jitihada hizo za Serikali katika kukabiliana na changamoto ya upatikanaji wa teknolojia za kuongeza virutubishi kwa wasindikaji wadogo wa chakula zimeungwa mkono na wadau mbalimbali kujitokeza kusambaza teknolojia hizo kwa wasindikaji hao, wakimemo Shirika la GAIN, na kampuni ya SANKU.

"Kwa mujibu wa takwimu za sensa ya viwanda vinavyozalisha unga ya 2022 iliyofanywa na Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara kwa kushirikiana na Shirika la Mpango Chakula Duniani (WFP), kuna viwanda vidogo sana na vidogo 33,721 Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar vinavyo zalisha unga wa mahindi. Kati ya hivyo viwanda, asilimia 2 tu ndivyo vinavyoongeza virutubishi. Hivyo, kwa takwimu hizo ni wazi kuwa hali si nzuri kwa nchi yetu hasa tunapo pambana na changamoto zitokanazo na lishe ikiwemo utapiamlo."ameongeza.
Kwa upande wake Afisa utafiti na uratibu shughuli za urutubishaji wa vyakula kutoka Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC) Selestine Mgoba ameishuku Serikali kwa kuleta mpango huo nakwamba utasaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto ya ukosefu wa virutubisho kwenye vyakula.

"Kwa kawaida ukikoboa unga wa mahindi unakuwa umepoteza asilimia 60 ya vilutubisho vilivypo kwenye hicho chakula pia kuna madini chuma na folic ambayo pia yanapotea hivyo ni vizuri kurutubisha hicho chakula ili kurudisha hivyo virutubisho vilivyopoteamesema Mgoba.

Naye Meneja Mradi Urutubishaji chakula kutoka Shirika lisilo la Kiserilali la Gain Archard Ngemela amesema kuwa anaamini kuwa hatua iliyofikiwa na SIDO pamoja na DIT ya kuleta Mashine za urutubishaji wa chakula kutaleta suluhisho kwa wafanyabiashara wa uzindikaji wogo ambao hasa ndio imekuwa changamoto.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news