Wamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kutoa milioni 250/- kufikisha maji Chimati na Makojo Musoma Vijijini

NA FRESHA KINASA

WANANCHI wa Vijiji vya Chimati na Makojo katika Jimbo la Musoma Vijijini mkoani Mara wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha shilingi milioni 250 kwa ajili ya kujenga miundombinu ya maji ya bomba katika kuhakikisha wanapata huduma ya maji safi na salama karibu na makazi yao.

Shukrani hizo kutoka kwa wananchi wa vijiji hivyo zimetolewa Januari 8,2022 kupitia taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini, Prof. Sospeter Muhongo.

"Tunaishukuru Serikali kutupatia Shilingi milioni 250 kwa ajili ya kujenga miundombinu ya maji ya bomba kati ya vijiji vya Makojo na Chimati. Maji ya Kijiji cha Chimati yatatoka kwenye tenki la ujazo wa lita 100,000 lililojengwa kijijini Makojo na tayari maji ya bomba yanatumika hapo Makojo.

"Chanzo cha maji hayo ni kutoka Ziwani Chitare. Ambapo tenki la kijijini Chitare lina ujazo wa lita 75,000," imeeleza taarifa hiyo.

Aidha, taarifa hiyo imetoa msisitizo kwa wananchi kuendelea kuitunza miundombinu hiyo ya uzalishaji na usambazaji wa maji ya bomba kwenye vijiji hivyo kwa manufaa ya maendeleo ya wananchi hao kwani Serikali inatumia fedha nyingi kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama.

Pia, taarifa hiyo imeelezea matengenezo ya miundombinu. "Kwa muda wa takribani siku tano, RUWASA imekuwa kwenye matengenezo na uboreshaji wa miundombinu ya maji ya bomba vijijini mwetu. Hadi leo hii maji ya bomba yameanza kupatikana tena baada ya matengenezo kukamilika kwenye vijiji vya Wanyere, Mikuyu, Nyambono, Saragana, Kanderema, Bugoji na Kaburabura," imeeleza taarifa hiyo.

"RUWASA wanapongezwa kwa kazi nzuri za kuhakikisha maji yanapatikana vijijini mwetu. Wako kazini hata kwa siku za Jumamosi na Jumapili. Musoma Vijijini tunaendelea kutoa shukrani nyingi sana kwa Serikali yetu inayoongozwa na Rais Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za kusambaza maji ya bomba safi na salama vijijini mwetu," imesema taarifa hiyo.

Magreth Majura ni mkazi wa Makojo akizungumza na DIRAMAKINI kwa njia ya simu amesema kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan imejizatiti kikamilifu kujenga miradi mikubwa ya maji maeneo mbalimbali nchini, jambo ambalo amesema ni la kupongezwa kwani linaimarisha maendeleo kuanzia ngazi ya familia hadi taifa na kuchochea shughuli za kiuchumi na uzalishaji.

"Nitoe uhalisia ndugu mwandishi, tunao mradi wa Mgango-Kiabakari- Butiama ambao unagharimu shilingi bilioni 70.5 huu ni mradi mkubwa sana, pongezi kwa Serikali yetu ya CCM kuzidi kutujalia wananchi wake tunampongeza Rais Dkt.Samia na mbunge wetu Prof. Muhongo mradi huu unakuja kutatua kero ya maji kabisa na pia fedha zilizotolewa shilingi milioni 250 kwa ajili ya vijiji vya Chimati na Makojo hii yote ni dhamira njema ya Serikali. Badala ya mama kutembea umbali mrefu kutafuta maji atayapata karibu,"amesema Magreth Majura.

"Ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za miradi ya maji na miradi mingine, na pia pongezi kwa Mbunge Prof. Muhongo kwa juhudi za kufuatilia kila mradi kwa ajili yetu wananchi tumeona akifanya jitihada mbalimbali kwa ajili ya Mkoa wa Mara kwa kutoa maombi serikalini ya miradi mbalimbali na kushiriki kwa vitendo ikiwemo kuchangia ujenzi wa miradi mbalimbali jimboni mwetu. hii yote ni kuhakikisha kwamba wananchi tunapata Maendeleo," amesema Naomy Peter.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news