LAAC yaridhika ukarabati Shule ya Sekondari ya Wasichana Mtwara

NA ASILA TWAHA

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) imeridhishwa na usimamizi wa fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ukarabati wa Shule ya Sekondari ya Wasichana Mtwara.
Pongezi hizo zimetolewa Machi 29, 2023 na Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa , Mhe. Ester Bulaya (Mb) wakati wa ziara ya kamati ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara mkoani Mtwara.

Amesema , usimamizi ulioneshwa na uongozi wa shule hiyo ni mfano wa kuigwa kwa viongozi wote waliopewa dhamana ya usimamizi wa fedha za Serikali zinazotolewa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuwataka kuwa wazalendo, waadilifu na waaminifu kwa mamlaka walioaminiwa.

Ameutaka uongozi wa shule hiyo kuongeza jitihada katika kuhakikisha wanasimamia na kuitunza shule hiyo na kukuza zaidi taaluma kwa kuwa Serikali imeshapeleka fedha kwa ajili ya kuboresha shule hiyo.

Mhe. Bulaya ametoa wito kwa wanafunzi kuonesha jitihada katika masomo kwa kusoma kwa bidii na kuheshimu walimu ili waendelee kuwa na ari na moyo katika kutekeleza majukumu yao ili kupatikane viongozi wenye uwezo,elimu,weledi waaminifu na waadilifu.

“Someni kwa bidii najua humu kuna watu wa fani mbalimbali mkiamua mnaweza, ifanyeni shule hii iwe bora na ninyi ndio mtaifanya ionekane bora kwa kusoma kwa bidii na ufaulu wenu na kuifanya iweze kuwa bora kama shule nyingine,”amesisitiza.

Awali akisoma taarifa ya ukarabati wa shule hiyo Mkuu wa Shule hiyo, Mwalimu Sikujua Mangisye amesema, shule ilipokea shilingi milioni 776.6 na kutekelezwa kwa ukarabati wa majengo 38 ikiwemo kubadilisha sakafu kwa baadhi ya mejengo, kupiga ripu, kupaka rangi, kutanua milango na madirisha kwa baadhi ya majengo, kuweka paa jipya kwa baadhi ya majengo, mifumo ya maji taka na safi na kuongeza mashimo ya maji taka na mfumo wa umeme kwenye majengo 38.

Pia ameushukuru uongozi wa Shule ya Sekondari Mtwara Ufundi kwa kuwapatia fedha shilingi milioni 80 ambapo waliweza kuunganisha na kiasi cha shilingi milioni 82 kilichobaki kwao na kufanya jumla ya shilingi milioni 162 kuanza ujenzi wa mradi wa mabweni mawili ambapo yatawasaidia wanafunzi.

Kwa upande wa Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI), Dkt.Charles Mahera ameupongeza uongozi wa shule kwa usimamizi wa fedha na kuhakikisha ukarabati unatekelezwa kama maagizo na muongozo wa Wizara ulivyotaka na kuwataka kuendelea kusimamia na kufanya suala la elimu linakuwa bora katika mazingira yote ya kujifunzia na kufundishia.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news