MIWILI YAKE SAMIA-7:Asante sana Mama

NA LWAGA MWAMBANDE

NDANI ya miaka miwili ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mheshimiwa Dkt.Samia Suluhu Hassan, Serikali imeendelea kuainisha rasilimali mbalimbali za maji zilizopo mijini na vijijini huku ikiwekeza fedha nyingi kuziendeleza, lengo likiwa ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama.

Miradi mingi ya maji imekamilika na mingine inaendelea kutekelezwa kwa kasi,mfano Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt.Samia imepeleka zaidi ya shilingi bilioni 70 kutekeleza mradi mkubwa wa maji wa Butimba mkoani Mwanza.

Mradi huo,utakapokamilika unatarajia kuzalisha zaidi ya lita milioni 48 kwa siku na unatarajiwa kusaidia kuondoa adha ya maji hasa kwa wananchi wanaoishi kwenye miinuko mkoani humo.

Pia, kuna mradi wa maji ya visima Kigamboni ambao unatoa maji lita milioni 70 kwa siku kwa ajili ya wakazi wa maeneo mbalimbali katika Jiji la Dar es Salaam,mradi wa maji wa Shongo-Mbalizi ambao utakuwa na uwezo wa kuzalisha maji lita milioni 8-12.

Mradi huo,utahudumia wananchi zaidi ya 80,000. Mradi huo utaongeza upatikanaji wa maji katika mkoa wa Mbeya kutoka asilimia 44 hadi asilimia 65. Vile vile kuna mradi mkubwa wa maji wa Longido wenye thamani ya shilingi bilioni 15.7 katika Wilaya ya Longido mkoani Arusha.

Lengo la Serikali kwa mujibu wa Wizara ya Maji ni kufikisha huduma ya maji kwa asilimia 95 mijini na 85 vijijini ifikapo mwaka 2025.

Hiyo ikiwa ni kwa uchache, mshairi wa kisasa Lwaga Mwambande anasema, kila Mtanzania ana imani kubwa na uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt.Samia;


188.Maji sote twatumia,
Kunywa pia kufulia,
Na mengine kufanyia,
Heko Rais Samia.

189.Hili umeangalia,
Ndoo unatutulia,
Yaweze kutufikia,
Heko Rais Samia.

190.Miradi imeingia,
Mingine wamalizia,
Lengo liweze timia,
Heko Rais Samia.

191.Maji kujitafutia,
Mwendo mbali kufikia,
Hutaki kuisikia,
Heko Rais Samia.

192.Mama unamwangalia,
Jasho anajivujia,
Maji kujitafutia,
Heko Rais Samia.

193.Kile ulichopania,
Ndoo wanazutumia,
Waweze kujishushia,
Heko Rais Samia.

194.Maji yaweze ingia,
Pale wanajiishia,
Bila ya kusumbukia,
Heko Rais Samia.

195.Mjini waangalia,
Hata vijijini pia,
Maji yatawafikia,
Heko Rais Samia.

196.Dasalamu meingia,
Shida kuiangalia,
Umewathibitishia,
Heko Rais Samia.

197.Maji wanayotumia,
Yatazidi kuingia,
Kila mtu kutumia,
Heko Rais Samia.

198.Na wala hujatulia,
Yale unayawania,
Huku huko wakimbia,
Heko Rais Samia.

199.Shule zakuangalia,
Mazuri wawafanyia,
Na sekta afya pia,
Heko Rais Samia.

200.Miradi walikandia,
Ya kwamba itavilia,
Tunazidi angalia,
Heko Rais Samia.

201.Na hili wasimamia,
Wanaokusaidia,
Husiti tupindulia,
Heko Rais Samia.

202.Muwazi wawaambia,
Yale wanayofulia,
Ili wapate sikia,
Heko Rais Samia.

203.Wale wasokusikia,
Hauko poa Samia,
Mbali unawafagia,
Heko Rais Samia.

204.Macho twakuangalia,
Uongoze Tanzania,
Pazuri weze fikia,
Heko Rais Samia.

205.Yale yanayotujia,
Japo dunia yavia,
Matumaini ni mia,
Heko Rais Samia.

206.Pazuri tutafikia,
Serikali tufanyia,
Na sisi kufurahia,
Heko Rais Samia.

207.Msingi mejichimbia,
Ushatengeneza njia,
Kazi kwako kupitia,
Heko Rais Samia.

208.Mwanamke Tanzania,
Umetuthibitishia,
Kazi unaijulia,
Heko Rais Samia.

209.Waliokuangalia,
Kwa macho ya kusinzia,
Mshangao mewajia,
Heko Rais Samia.

210.Heri tunakutakia,
Nchi kututumikia,
Twende mbele Tanzania,
Heko Rais Samia.

211.Bado tunasubiria,
Miradi kamilishia,
Tuweze kuitumia,
Heko Rais Samia.

212.Reli mpya Tanzania,
Kwa karibu yanukia,
Tutaanza itumia,
Heko Rais Samia.

213.Dar-Moro nakwambia,
Karibu tutatumia,
Wenyewe kusafiria,
Heko Rais Samia.

214.Moro na Dodoma pia,
Pazuri imefikia,
Wengi tutafurahia,
Heko Rais Samia.

215.Makutu-Tabora njia,
Sasa watupaulia,
Wanafanya kazi pia,
Heko Rais Samia.

216.Mwanza-Isaka sikia,
Kazi wanatufanzia,
Nchi watufungulia,
Heko Rais Samia.

217.Tabora-Kigoma nia,
Kuweza kumalizia,
Iwe mpya Tanzania,
Heko Rais Samia.

218.Umeme kwa Tanzania,
Inang’aa nakwambia,
REA ndiyo twatambia,
Heko Rais Samia.

219.Kule ulikoanzia,
Hadi ulipofikia,
Wengi tunafurahia,
Heko Rais Samia.

220.Hata vijijini pia,
Kwenye nyumba twatumia,
Umeme metufikia,
Heko Rais Samia.

221.Miaka ilosalia,
Kote tutamalia,
Umeme kufurahia,
Heko Rais Samia.

222.Pale ulipoingia,
Wengine lifikiria,
Mazuri yataishia,
Heko Rais Samia.

223.Kwa matendo mewambia,
Kazi unaijulia,
Nchi kututumikia,
Heko Rais Samia.

224.Twazidi kuangalia,
Mipango watupangia,
Mazuri yakiingia,
Heko Rais Samia.

225.Dodoma tukirudia,
Pia tunafurahia,
Nyuma hatutarudia,
Heko Rais Samia.

226.Msingi mepigilia,
Makao yanavutia,
Mengi inatufanyia,
Serikali ya Samia.

227.Eapoti nakwambia,
Msalato yaingia,
Kazi yatuzalishia,
Serikali ya Samia.

228.Jiji kulizungukia,
Barabara zatimia,
Misongamano ishia,
Heko Rais Samia.

229.Dodoma hajaishia,
Mambo anatufanyia,
Mbeya nako kafikia,
Heko Rais Samia.

230.Wapi kulikosalia,
Kote anafwatilia,
Iwe bora Tanzania,
Heko Rais Samia.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news