Waziri Kairuki atoa wito Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC)

NA MWANDISHI WETU

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI), Mheshimiwa Angellah Kairuki ameisisitiza Baraza la Wafanyakazi wa Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC) kuendelea kuchapa kazi kwa uaminifu na uadilifu.

Mheshimiwa Kairuki ametoa wito huo leo Machi 16, 2023 wakati akifungua Baraza la Wafanyakazi wa Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC) katika Ukumbi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi jijini Dodoma.

"Mwenyekiti wa Baraza amefafanua kwa kina kuhusu Muundo wa Tume na pia ameeleza kuwa katika muundo huo kuna uhitaji wa Makatibu Wasaidizi wa Wilaya ambao bado hawajateuliwa.

"Pia ameeleza hatua za kukamilisha Muundo wa Maendeleo ya Utumishi na Mshahara ya Watumishi wa Tume zinaendelea kwa Katibu Mkuu- UTUMISHI ambapo natambua hicho ndiyo kigezo muhimu kinachohitajika ili teuzi hizo ziweze kufanyika.

"Natambua pia kuwa, Makatibu hao ndiyo wanaotekeleza majukumu ya kisheria ya Tume kwa mujibu wa Sheria ya Tume ya Utumishi wa Walimu Sura 448. Natambua hicho ni kilio chenu kikubwa na hivyo, naomba niwasihi muendelee kuchapa kazi kwa uaminifu na uadilifu na suala hili tutaendelea kulifuatilia kwenye mamlaka zinazohusika,"amefafanua Waziri Kairuki.

Pia ameipongeza tume hiyo kwa kuwa na Baraza la Wafanyakazi ikiwa ni mahali ambapo watumishi wanaweza kuwasilisha kero zao na kuzitafutia ufumbuzi pamoja na kujadili masuala mbalimbali ya tume kwa ajili ya ustawi wa taasisi.

Aidha,Mheshimiwa Waziri amewapongeza wajumbe wote wa baraza waliochaguliwa na wanaoingia kwa nafasi zao huku akiwataka watumie nafasi hizo kuwawakilisha wenzao ipasavyo ambao hawakupata fursa ya kuwepo kwenye baraza hilo.

"Mwenyekiti wa baraza ameeleza kuwa, kwa mwaka 2022/2023 tume imewezeshwa fedha za kitanzania kiasi cha shilingi bilioni 3.1 kupitia Mradi wa BOOST kutekeleza majukumu yake.

"Nimejulishwa kuwa, kupitia fedha hizo za mradi, tume imeweza kufanya mapitio na kuhuisha Kanuni za Maadili na Utendaji Kazi katika Utumishi wa Walimu, kununua vitendea kazi vikiwemo magari (16) na vifaa vya TEHAMA.
"Aidha,tume imewezeshwa pia kuhuisha Sheria na Kanuni zote zinazohusu mzunguko wa Utumishi wa Mwalimu na hatua za mwisho za kukamilisha andiko kwa ajili ya kikao cha wadau zinaendelea. Yote haya yamefanywa na Rais wetu kwa lengo la kuboresha elimu nchini,"ameongeza Mheshimiwa Waziri Kairuki.

Katika hatua nyingine, Mheshimiwa Waziri Kairuki amesema, hivi karibuni alifanya ziara katika baadhi ya mikoa na kuongea na walimu.

Amesema, walimu waliwasilisha kwangu kero kubwa wanazokabiliana nazo ikiwa ni pamoja na baadhi ya walimu kucheleweshwa kubadilishiwa Muundo wa Utumishi, kutopandishwa madaraja au cheo kwa wakati, kupandishwa daraja la aina moja (kujirudia) tofauti na matarajio yao.

"Niliiagiza tume kufuatilia kwenye tange za walimu ili kuwabaini walimu hao. Nawapongeza sana kwa kufanyia kazi maelekezo yangu kwa wakati na kuwezesha taarifa za uchambuzi wa madai hayo ya walimu yanawasilishwa kwenye mamlaka zinazohusika na linaendelea kufanyiwa kazi.

"Nichukue pia nafasi hii kupongeza Tume na Menejimenti yake kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kusimamia na kuhakikisha kuwa tume inatekeleza majukumu yake ipasavyo kwa kuzingatia sheria, kanuni,taratibu na miongozo inayotolewa na Serikali. Kipekee pia, nawashukuru watumishi wa tume kwa namna mnavyojitoa katika kutekeleza majukumu ya tume na hivyo kufanya kazi ya viongozi wanaowasimamia kuwa nyepesi,"amesisitiza.
Mbali na hayo, Mheshimiwa Angellah Kaiuruki amezindua Mfumo wa Kielektroniki wa Kupokea Malalamiko ya walimu kwa muda mfupi na akapongeza Tume ya Utumishi wa Walimu ( TSC) kwa kuanzisha mfumo huo ambao utakuwa suluhusho la changamoto za walimu ambao ni zaidi ya asilimia 50 ya watumishi.

Kabla ya kuzindua wa Mfumo huo unaojulikana kama Teacher’s Service Commission Management Information Systems (TSC-MIS) jijini Dodoma kwenye mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Tume, Waziri Kairuki aliipongeza TSC kwa kusimika mfumo huo ambao pamoja na faida nyingine nyingi utapokea na kutatua changamoto za walimu kwa haraka.

“Naipongeza TSC kwa kutatua changamoto za walimu tangu kuanzishs kwake 2016, lakini kwa kusimika mfumo huo itahaharikisha kupokea na kutatua changamoto za walimu popote walipo bila kulazimika kufika ofis za tume,” alisema.

Pia aliwapongeza vijana wa kitanzania watalaamu wa Teknolojia ya Habari (IT) waliojenga mfumo huo wakiwamo watalaamu kutoka OR-Tamisemi, TSC OR-Utumishi na mtandao wa mawasiliano serikalini (e-govt), Chuo cha Mzumbe na Chuo Kikuu cha Sokoine.

Akizungumzia faida za mfumo huo wa Kielektoniki (TSCMIS), Katibu wa TSC, Paulina Nkwama alisema, mfumo huo unaondoa mfumo wa zamani ambao haukutoa taarifa sahihi za walimu, na hazikupatikana kwa wakati na ulitumia gharama nyingi na muda mwingi walimu kufika makao makuu.

“Lengo la mfumo huo ni kuberesha na kurahisisha utendaji kazi wa shughnuli za kila siku katika kuwahudumia walimu na wadau mbalimbali,” amesema Nkwama.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news