Wizara ya Ardhi yafuturisha watumishi wake

NA MUNIR SHEMWETA-WANMM 

WIZARA ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imewafuturisha watumishi wake waliopo wizarani na Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Dodoma. 
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt.Angeline Mabula na Naibu wake, Geofrey Pinda waliwaongoza viongozi wa wizara hiyo kujumuika na watumishi katika futari iliyofanyika Aprili 3, 2023 jijini Dodoma. 

Akizungumza wakati wa futari hiyo, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt.Angeline Mabula aliwaeleza watumishi kuwa, uamuzi wa kuandaliwa futari ya pamoja unalenga kuwaweka pamoja watumishi wa wizara hususani kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani na kwaresma. 
‘’Uamuzi wa kuandaa futari ya pamoja unalenga kuwaweka pamoja watumishi wa wizara yetu na ninaomba tuwe na umoja na kushirikiana katika kazi zetu,’’ alisema Dkt.Mabula. 

Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Geofrey Pinda alishukuru uamuzi wa wizara kukutanisha pamoja watumishi kuanzia ngazi ya chini hadi juu jambo alilolieleza kuwa ni nadra sana kutokea watumishi kukutana kwa wakati mmoja kuanzia kada ya chini hadi juu. 
‘’Niishukuru uamuzi wa kuwakutanisha watumishi wa sekta ya ardhi pamoja maana ni nadra sana watumishi wa wizara kuanzia kada za chini hadi juu kukutana kwa mara moja,’’alisema Pinda.
Kamishna wa Ardhi nchini, Nathaniel Methew Nhonge akitoa neno la shukrani wakati wa futari ya pamoja ya watumishi wa Wizara ya Ardhi jijini Dodoma.(Picha na WANMM).
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Anthony Sanga alihimiza watumishi wa sekta ya ardhi kuwa na umoja wakati wote wa utendaji kazi. 
Aidha, aliwaeleza watumishi wa wizara ya ardhi kuwa, wizara hiyo kwa sasa iko kwenye juhudi za kuboresha mifumo yake ya ulipaji kodi ya pango la ardhi ambapo alieleza kuwa mfumo huo utakapokamilika wamiliki wa ardhi nchini watakuwa wakipata ujumbe utakaowawezesha kulipa kodi bila kufika ofisi za ardhi. 

Hii ni mara ya kwanza kwa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuandaa futari ya pamoja ya watumishi wake tangu serikali ilipohamia rasmi mkoani Dodoma.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news