Serikali yasimama imara kuhusu haki na maendeleo ya mtoto

NA GODFREY NNKO

WAZIRI wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mheshimiwa Dkt.Dorothy Gwajima (Mb) amesema, wizara inaendelea kuratibu na kusimamia utoaji wa haki za msingi kwa mtoto ikiwa ni pamoja na haki ya kuishi, kulindwa, kuendelezwa, kushiriki na kutobaguliwa.

Ameyasema hayo leo Mei 18, 2023 bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya fedha kwa mwaka 2023/24.

Hata hivyo, amesema baadhi ya watoto hawazipati haki hizo na hivyo wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo vitendo vya ukatili katika familia na jamii.

"Moja ya sababu zinazosababisha ukatili dhidi ya watoto hapa nchini ni mwendelezo wa mmomonyoko wa maadili katika jamii unaoambatana na mila na desturi za jamii husika ambazo zinasababisha ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto.

"Mheshimiwa Spika, katika kushughulikia changamoto za vitendo vya ukatili dhidi ya watoto,wizara kwa kushirikiana na wizara nyingine za Kisekta imeendelea kuratibu na kusimamia utoaji wa elimu ya upatikanaji wa haki za watoto na kupinga ukatili dhidi yao kupitia makundi yote katika jamii.

"Katika kufikia kundi kubwa la watoto kwenye shule,wizara imeratibu uundaji wa Madawati ya Ulinzi na Usalama wa Mtoto 1,488 katika shule za msingi 1,070 na sekondari 418 nchini,"amesema Waziri Dkt.Gwajima.

Waziri Dkt.Gwajima amefafanua kuwa, katika kuimarisha upatikanaji wa haki ya watoto ya kushiriki katika kujadili masuala yanayowahusu,wizara inaendelea kuhuisha na kuunda Mabaraza ya Watoto katika ngazi za vijiji na mitaa hadi ngazi ya Taifa.

Amesema, katika kipindi cha Julai, 2022 hadi Aprili 2023, jumla ya mabaraza ya watoto 592 yameanzishwa sawa na asilimia 3.6 ya lengo la kuanzisha mabaraza 16,582.

Vile vile amesema, wizara pia imeendelea kuelimisha na kufuatilia malezi na makuzi ya watoto ikiwa ni pamoja na usalama wa watoto wakiwa nyumbani, shuleni na kwenye jamii.

Katika kipindi cha kuanzia Januari, 2022 hadi Machi, 2023 amesema jumla ya matukio ya ukatili 15,901 yaliripotiwa Polisi.

Aidha, sehemu kubwa ya jamii imekuwa ikioneana muhali kwenye kutoa ushahidi ili kesi itayarishwe vizuri kukidhi vigezo vya kufikishwa mahakamani.

"Hali hii inaathiri kasi ya haki kupatikana, mfano kati ya matukio haya kesi 671 ndiyo zilifikishwa mahakamani ambapo kati ya hizo kesi 368 zilizotolewa hukumu na kesi 303 zinaendelea.

"Mheshimiwa Spika, nitoe wito kwa jamii kuendelea kujitokeza mbele ya vyombo vya utoaji haki kutoa ushahidi ili kesi zote zilizopo kwenye mnyororo wa haki jinai ziweze kufika mwisho na haki ipatikane.

"Natoa pongezi kwa Jeshi la Polisi na mamlaka zingine za uchunguzi na maafisa wa Dawati la Jinsia katika taasisi mbalimbali ambao wamekuwa wakifanya kazi usiku na mchana kuwafikia watuhumiwa na kutoa faraja na huduma kwa manusura,"amefafanua.

Dkt.Gwajima amesema, katika kukabiliana na changamoto zinazoibuka za usalama wa watoto katika mabasi ya shule na kuimarisha malezi, makuzi na usalama wa watoto shuleni, Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imetoa Waraka wa Elimu Na. 1 wa mwaka 2023.

Ni kuhusu uboreshaji wa huduma ya magari au mabasi yanayotumika kusafirisha wanafunzi ikiwa ni pamoja na kuwepo kwa wahudumu wawili ambao ni mhudumu wa kike na wa kiume kwa kila gari mwanzo wa safari hadi mwisho na inaposhindikana wote wawili basi awepo mhudumu wa kike.

"Vilevile, Serikali imetoa Waraka wa Elimu Na. 2 wa mwaka 2023 ulioweka zuio la utoaji wa huduma ya kulaza wanafunzi wa bweni kwa ngazi za elimu ya awali hadi shule za msingi chini ya darasa la 5 isipokuwa kwa kibali maalum kutoka Ofisi ya Kamishna wa Elimu.

"Mheshimiwa Spika, katika azma ya kuongeza uelewa na hamasa ya jamii kwenye ushiriki wa malezi, makuzi na ulinzi wa watoto, wizara imeendelea kusimamia na kuratibu kampeni mbalimbali kuhamasisha jamii kushiriki katika mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili na unyanyasaji wa kijinsia ikiwemo “Twende Pamoja Ukatili Sasa Basi” na “Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii (SMAUJATA)”.

Amesema, utendaji wa SMAUJATA umeamsha ari ya Watanzania wengine wazalendo kuanzisha vikundi vipya vya kuunga mkono ajenda hii vikiwemo taasisi ya Safe Society Platform Tanzania iliyopo Mkoa wa Mara na Foundation for Ambassadors Gender Initiatives (FAGDI) yenye Kampeni yenye kaulimbiu ya “Zijue Fursa, Imarisha Uchumi, Kataa Ukatili, Kazi Iendelee-ZIFIUKUKI”.

Kampeni hii amesema, ilizinduliwa kwa mafanikio makubwa mwezi Aprili, 2023 katika Mkoa wa Dar es Salaam ikihusisha wahariri wa vyombo ya habari,viongozi wa dini, Baraza la Wazee, Machifu na wananchi kwa ujumla.

Waziri Dkt.Gwajima amesema, kufuatia ongezeko la vitendo vya mmomonyoko wa maadili katika jamii Mei 15, 2023 wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Familia, wizara imezindua kampeni mahsusi inayohusisha wadau mbalimbali ili kulinda maadili, mila, desturi na tamaduni zetu. Kampeni hii inaongozwa na kaulimbiu “Taifa Letu, Maadili Yetu”.

Ameendelea kufafanua kuwa, wizara imeendelea kuhusisha wadau wenye ushawishi mkubwa kwa jamii katika kuimarisha vita dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Miongoni mwa wadau hao ni Klabu za Mpira wa Miguu ambapo tayari Yanga SC na Azam FC wameunga mkono vita hii na wengine wanaendelea kujitokeza.

"Vilevile, tunatambua mchango mkubwa wa vyombo mbalimbali vya habari ambavyo vimekuwa mstari wa mbele wakati wote kufikisha sauti ya elimu kwa wananchi na wito kuingia kwenye vita hii.

"Mheshimiwa Spika, Wizara inaendelea kuratibu huduma ya msaada wa simu bila malipo Na. 116 (Child Helpline) kwa ajili ya jamii kutoa taarifa za vitendo vya ukatili dhidi ya watoto.

"Katika kipindi cha Julai 2022 hadi Aprili 2023 jumla ya simu 11,316 kuhusu watoto zilipokelewa. Pia, Wizara imeanzisha “call center” ambayo itaanza kutumika Juni, 2023.

"Vilevile, wananchi takribani 342 walifikisha malalamiko yao kwa kunitumia ujumbe wa simu kupitia namba yangu ya 0734124191 na 0765345777 ambapo niliwaunganisha na maafisa ustawi wa mikoa kwa huduma stahiki.

"Nitumie fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza Maafisa Ustawi wa Jamii na Maafisa Dawati la Jinsia Polisi kwa mchango wao mkubwa wanaoutoa katika kushughulikia vitendo hivi hususan katika kutoa huduma kwa manusura wa vitendo vya ukatili dhidi ya watoto.

"Aidha, natoa wito kwa viongozi na watendaji wote kuendelea kuwa karibu na wananchi ili wapate huduma zote ngazi stahiki na kuepuka kuhitaji rufaa hata kwa masuala yenye ufumbuzi kwa ngazi husika,"ameongeza.

Mitandaoni

Waziri Dkt.Gwajima ameendelea kufafanua kuwa, "Mheshimiwa Spika, kwa sasa tumeanza kushuhudia ukatili mpya wa watoto katika mitandao.

"Kwa mujibu wa Taarifa ya Hali ya Ukatili wa Watoto Mtandaoni (Disrupting Harm Report in Tanzania-2022) inaonesha kuwa asilimia 67 ya watoto wenye umri wa miaka 12-17 hapa nchini ni watumiaji wa mitandao.

"Katika kuongeza uelewa wa athari za ukatili kwa watoto mtandaoni Wizara imeandaa Vijarida vya kuelimisha watoto, wazazi na walimu kwa kutumia lugha nyepesi.

"Nitumie fursa hii kukushukuru wewe binafsi Mheshimiwa Spika kupitia Bunge lako Tukufu kwa kutoa maelekezo kuhusu marekebisho ya sheria za makosa ya jinai katika kuimarisha juhudi za kupambana na mmomonyoko wa maadili.

"Kipekee, namshukuru Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb) Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa maelekezo ya namna ya kushughulikia masuala ya mmomonyoko wa maadili nchini ambapo Wizara yangu imeanza kuyatekeleza,"amesema.

Amesema,wizara inaendelea kutoa elimu kuhusu mila na desturi zenye madhara katika jamii. Pamoja na elimu hiyo, bado kuna baadhi ya jamii zinazoendeleza mila ya ukeketaji katika mikoa mbalimbali nchini.

Dkt.Gwajima amesema, katika kipindi cha Julai, 2022 hadi Aprili, 2023 kampeni ya kutoa elimu kuhusu kutokomeza ukeketaji imefanyika kwenye mikoa minne yenye kiwango cha juu cha ukeketaji ya Manyara, Arusha, Dodoma, na Singida.

"Mheshimiwa Spika, katika kushughulikia changamoto za kundi la Vijana Balehe nchini, Wizara imeendelea kuratibu utekelezaji wa Ajenda ya Kitaifa ya Kuwekeza kwenye Afya na Maendeleo ya Vijana Balehe Nchini (2021/22-2024/25).

"Wizara pia inaendelea kuratibu Programu Jumuishi ya Taifa ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto 2021/22-2025/26 yenye lengo la kutatua changamoto za ukuaji na maendeleo ya watoto wenye umri kati ya miaka 0 hadi 8."

Amesema, katika utekelezaji wa programu hiyo, mwezi Novemba, 2022, wizara iliratibu mafunzo kuhusu sayansi ya malezi na makuzi ya watoto kwa wajumbe 124 wa Kamati za Kudumu za Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Maelezo ya kina kuhusu utekelezaji wa programu hiyo yanapatikana katika aya ya 70 na 71.

"Nitumie fursa hii, kutoa rai kwa Watanzania wote kuwa mstari wa mbele katika kutokomeza vitendo vyote vya ukatili dhidi ya watoto vinavyotokea nyumbani kwa asilimia 60, ndani na nje ya shule kwa asilimia 40.

"Hili litawezekana endapo wazazi na walezi watatimiza jukumu lao la msingi la malezi na makuzi ya watoto kwa kuhakikisha wanatenga muda wa kuwa karibu na watoto wao ili kujua changamoto zinazowakabili.

"Aidha, wazazi wafuatilie mienendo ya watoto wao na kutoa taarifa za viashiria vya ukatili na vitendo vya ukatili vinavyowapata watoto mapema ili mamlaka husika kuchukua hatua kwa wakati. Watoto ni tunu muhimu kwa Taifa letu, tuwalinde ili wakue na kufikia utimilifu wao,"amebainish Waziri Dkt.Gwajima.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news