TANZANIA, BORA KUISHANGILIA-4: Dar es Salaam ingia,Mambo mengi yajazia

NA LWAGA MWAMBANDE

HISTORIA inaonesha kuwa, Jiji la Dar es Salaam lilianza kama kijiji kidogo cha wavuvi kilichojulikana kama Mzizima.

Kijiji hicho kilianzishwa na Wabalawa ambao walichanganyika na Wazaramo kuelekea kwenye maeneo ya Bara la Afrika Mashariki na ambazo zilijulikana kama ‘Caravan Routes’.

Ujenzi wa Makao ya Sultani pamoja na bandari ulianza rasmi mwaka 1865 katika eneo la Kijiji cha Mzizima. Ujenzi huo ulikamilika mwaka 1866 na Sultani Majid bin Said kuhamia Dar es Salaam mwaka huo.

Mara baada ya Sultani Majid bin Said kuhamia Dar es Salaam mji ulianza kupanuka na uchumi wake kukua kwa kasi kubwa japo kwa kipindi kifupi ambapo Sultani Majid bin Said alifariki mwaka 1870.

Kifo cha Sultani huyo kilisababisha kudidimia kwa maendeleo ya mji wa Dar es Salaam. Hali hiyo ilianza tena kubadilika mwaka 1884 kufuatia kuanzishwa kwa koloni la Wajerumani la Afrika Mashariki.

Mwaka 1891 Serikali ya kikoloni ya Kijerumani iliamua kuhamisha makao makuu ya utawala wake katika Afrika Mashariki kutoka Bagamoyo na kuyaweka Dar es Salaam.

Hata hivyo, baada ya Wajerumani kushindwa na Waingereza katika Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia mwaka 1916, Mji wa Dar es Salaam uliendelea kuwa makao makuu ya utawala wa koloni la Waingereza nchini Tanganyika hadi ilipojipatia uhuru wake mwaka 1961.

Dar es Salaam iliendelea kuwa makao makuu ya Tanganyika huru na hatimaye kuwa makao makuu ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hadi mwaka 1972 wakati Serikali ilipoamua kuhamishia makao yake makuu mjini Dodoma. Jiji la Dar es Salaam liliendelea kubaki kuwa maarufu kwa kuwa Jiji kuu na kitovu cha biashara nchini Tanzania.

Aidha, Dar es Salaam ni kati ya mikoa 26 ya Tanzania Bara na mikoa 31 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Umepakana na Mkoa wa Pwani pande zote barani na Bahari ya Hindi upande wa Mashariki.

Picha na planetware.

Eneo la mkoa ambalo ni jiji la Dar es Salaam ndilo kitovu cha shughuli za biashara nchini Tanzania, na ni kati ya majiji yanayokua haraka zaidi duniani. Huku ukikadiriwa kuwa na ukubwa wa kilomita za mraba 1,800 pamoja na visiwa vidogo vinane na eneo la bahari kati ya Pwani na visiwa hivyo. Eneo la nchi kavu pekee ni kilomita za mraba 1,393.

Mkoa huu unaundwa na wilaya tano ikiwemo ya Kinondoni,Ilala,Temeke, Kigamboni na Ubungo. Zikiwemo Halmashauri za Jiji la Dar es Salaam, Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, Ilala,Temeke, Ubungo na Kigamboni. Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anakupitisha Dar es Salaam kupitia ushairi uweze kujifunza mengi. Endelea;


1. Dar es Salaam ingia,
Ndio hasa Tanzania,
Fika utajisikia,
Ya kwamba uko nyumbani.

2. Kila kabila sikia,
Ujualo Tanzania,
Riziki wajipatia,
Dar es Salaam jijini.

3. Joto lake sikizia,
Ngozi afya lautia,
Weusi wa kutitia,
Twang’ara hadi usoni.

4. Mji peke Tanzania,
Mambo mengi yajazia,
Mengi ya kufurahia,
Karibuni sana jijini.

5. Ilala, Temeke pia,
Wilaya zimetulia,
Kinondoni nakazia,
Jiji letu lasheheni.

6. Kigamboni tangulia,
Ukitaka jifungia,
Fukwe zake zavutia,
Kubarizi tatamani.

7. Ubungo linaanzia,
Jiji unapoingia,
Miundombinu sifia,
Kama uko ghorofani.

8. Dasalamu ikilia,
Tanzania inalia,
Jiji likifurahia,
Tanzania burudani.

9. Uchumi wa Tanzania,
Dasalamu yachangia,
Sabi-na-tano ya mia,
Kodi yenda hazinani.

10. Viwanda viko mamia,
Bandari imetulia,
Kutoka na kuingia,
Dasalamu i njiani.

11. Sipitali kubwa pia,
Dasalamu zavutia,
Muhimbili kianzia,
Regency na Aga-Khani.

12. Kama sitakutajia,
Haki nitakuibia,
Sipitali kubwa pia,
Ni ile ya Saratani.

13. Mnazi Mmoja pia,
Zanzibar ya Tanzania,
Ni kubwa ninakwambia,
Kule kote Visiwani.

14. Hizi na zingine pia,
Wagonjwa zatutibia,
Na kwenda kwenda India,
Huko kunashuka chini.

15. Badala yake sikia,
Wagonjwa wanatujia,
Huduma zinavutia,
Hata nchi za jirani.

16. Tiba kisisitizia,
Kwa weledi Tanzania,
Pesa itatupatia,
Hata zile za kigeni.

17. Zingine kubwa sikia,
Hata sijakutajia,
Itoshe kukuambia,
Kiafya tuko makini.

18. Biashara kubwa pia,
Hapo zimejichindia,
Azam nakutajia,
Viwanda vimesheheni.

19. Mali nyingi kuingia,
Dasalamu zapitia,
Bidhaa za ndani pia,
Na kwenda ughaibuni.

20. Barabara Tanzania,
Dar ndiyo zaanzia,
TAZARA wajipitia,
Juu juu siyo chini.

21. Ubungo nakuambia,
Foleni historia,
Hilo tunafurahia,
Hakika panashaini.

22. Kilimo wakisikia,
Kidogo wajifanyia,
Madalali wako mia,
Wanaishia lakini.

23. Ujanja ulizidia,
Kwa miaka nakwambia,
Wakuja kuwaibia,
Bila wao kubaini.

24. Serikali kuingia,
Kazi kusisitizia,
Ujanja unaishia,
Sasa ni kazi kazini.

25. Maendeleo sawia,
Dasalamu yajazia,
Vyote utajipatia,
Vya bei juu na chini.

26. Barabara mesikia,
Hoteli ngekutajia,
Viwanja mpira pia,
Hapa Dar ni nyumbani.

27. Bahari mabaharia,
Daraja limetulia,
Kigamboni twaingia,
Kwa feri na darajani.

28. Pwani ya bahari pia,
Nguzo tumesimikia,
Haziwezi kutitia,
Daraja la baharini.

29. Jiji lazidi vutia,
Miundombinu sawia,
Ulaya twaifikia,
Siku zijazo usoni.

30. Makao makuu pia,
Ya nchi lishikilia,
Uhuru lipoingia,
Sasa Dar mkoani.

31. Huyu namsimulia,
Wengi awakilishia,
Wale walosimamia,
Kile walikiamini.

32. Bibi Titi nakwambia,
Uhuru lipigania,
Hadi tulipofikia,
Nchi kuwa na Amani.

33. Haki alipigania,
Wanawake angalia,
Chini wasijeishia,
Maendeleo nchini.

34. Wanawake jumuia,
Kiti alikikalia,
TANU akawavutia,
Kwa kujiunga chamani.

35. Yeye twamfurahia,
Hapa kwetu Tanzania,
Sababu lipigania,
Haki na yake Imani.

36. Azimio kusikia,
La Arusha nakwambia,
Vitu hakufurahia,
Vilivyokuwemo ndani.

37. Kile alikichukia,
Kushindwa kuvumia,
Watu kujipangishia,
Nyumba kupigwa chini.

38. Azimio kuzuia,
Viongozi kutumia,
Nyumba kujipangishia,
Aligoma asilani.

39. Kamati kuu sikia,
Ya TANU kaachilia,
Na kwake akabakia,
Akidumu maishani.

40. Kesi kwake kaingia,
Uhaini nakwambia,
Adhabu ikaingia,
Kifungo maisha ndani.

41. Nyerere hakutulia,
Bali alimwachilia,
Ugenini katulia,
Hadi kwenda kaburini.

42. Bibi Titi nakwambia,
Sana twamkumbukia,
Kwanza kwanza nakwambia,
Kuwaswaga wakoloni.

43. Na bado hajaishia,
Bado twamsikia,
Barabara jina pia,
Dar es Salaam jijini.

Lwaga Mwambande (KiMPAB
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news